dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Monday, May 25, 2015

CUF yapuliza kipenga urais wa Zanzibar.


Image result for seif sharif hamad
Katibu mkuu wa CUF Maalim Seif

Chama cha Wananchi (CUF) kimepuliza kipenga cha urais kwa upande wa Zanzibar, kwa kuwataka wanachama wake wenye sifa kujitokeza kuchukua fomu za kuteuliwa kuwania nafasi ya urais wa Zanzibar kuanzia leo.
Kadhalika, CUF kimesema wamekubaliana na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kuwa mgombea wa urais Zanzibar atatoka chama hicho.
Aidha, pia Jimbo la Kikwajuni kwa nafasi ya ubunge wamekubaliana kumsimamisha mgombea kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa CUF, Omar Ali Shehe, alitangaza kufunguliwa kwa milango hiyo jana, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za CUF zilizoko Vuga, mjini hapa.
 Alisema utoaji wa fomu hizo za kugombea urais katika uchaguzi mkuu ambao unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu utaanza leo. 
“Tunawataka wanachama wenye sifa kujitokeza kuchukua fomu za kugombea urais, wasimuachie katibu wetu mkuu,  Maalim Seif Sharif Hamad pekee yake ili kuondoa minong’ono kuwa kiongozi huyu pekee ndiye anayegombea urais katika chama hiki,” alisema Shehe.
Alisema uchukuaji wa fomu utachukua wiki moja na kwamba Mei 31, mwaka huu, ndiyo mwisho wa uchukuaji na urejeshaji wa fomu hizo.
 Mkurugenzi huyo alifafanua kuwa fomu hizo zitatolewa kwa makatibu wa wilaya ndani ya chama hicho na gharama yake ni Sh. 500,000.
 “Tunawaomba wanachama wetu kila mwenye sifa bila ya kujali jinsia, anayetaka kugombea nafasi ya urais wa Zanzibar asisite, ajitokeze kugombea nafasi hii,” alisema.
 Alisema baada ya uchukuaji na urejeshaji wa fomu kukamilika, hatua itakayofuata ni wagombea kupelekwa katika Kamati ya Utendaji Taifa ili kupigiwa kura ya maoni na baada ya hapo watapelekwa Baraza Kuu la chama hicho ambalo ndilo litakalojiridhisha kama mgombea anafaa.
 “Hata kama atajitokeza mtu mmoja tu kuchukua fomu ya urais ni lazima apitie katika hatua ya mkutano wa kamati tendaji kupigiwa kura ya ndiyo au hapana, kisha atapelekwa Baraza Kuu kujadiliwa,”  alisema Shehe.
 Alisema ana imani kuwa watu wengi watajitokeza kuchukua fomu ya kugombea urais badala ya kumuachia Maalim Seif peke yake. Alisema chama hicho kina watu wengi wenye sifa za kugombea nafasi hiyo tofauti na inavyoelezwa na baadhi ya watu na mahasimu wao kisiasa.
 Akizungumzia kuhusu vijana wawili wa chama hicho wanaoshikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kumtukana na kumkashifu Rais wa Zanzibar na Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi, mkurugenzi huyo ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Chake Chake, alithibitisha vijana hao walikuwa wakisambaza ujumbe wa sauti kwa kuwapa tahadhari viongozi hao na siyo kuwatukana au kuwakashifu. 
“Vijana hawa wametumia uhuru wao wa kuongea kwa kuwaonya viongozi ili haki iweze kutendeka na kama polisi wameamua kuwakamata basi wawakamate na wengine wanaomtukana Maalim Seif tena hadharani katika mikutano ya hadhara ambayo ipo chini ya uangalizi wa jeshi hilo,” alisema.
 Alidai Jeshi la Polisi ni chombo cha ubaguzi na kwamba limekuwa likipendelea na kuegemea upande wa chama tawala kwa lengo la kuidhoofisha CUF.
“Kinachotushangaza ni kuwa jeshi hili limewakatalia hata kuwapa dhamana vijana hao wakati dhamana ni haki ya kila mtu,” alisema.
 Mwishoni mwa wiki Jeshi la Polisi liliwashikilia watu wawili, Ali Said Abdallah (21) mkazi wa Kiwani Kisiwani Pemba anayedaiwa kusambaza ujumbe wa sauti katika mitandao ya kijamii kwa kumtisha Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein na Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi kwa kuwataka wasiende Pemba kwani hakuna wafuasi wao na endapo CUF haitashinda katika uchaguzi mkuu atawahamasisha wafuasi wenzake kuzitambua nyumba za askari polisi na familia zao waliopo Pemba na kuwateketeza kwa moto. 
Mwingine ni Hussein Mageni Hussein (27) mkazi wa Pangawe Fuoni Unguja, ambaye anadaiwa kumpigia simu na kumtumia ujumbe wa maandishi kwa simu yake ya mkononi Balozi Seif na  kumtukana na kumtolea maneno ya kashfa.

CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment