dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Thursday, February 4, 2016

Nyuma ya pazia sakata la Standard Bank

Wateja wakiwa ndani ya jengo la Benki ya Standard kupata huduma. Picha ya mtandao
By Mwandishi wetu, Mwananchi
Ufisadi kwa kiasi kikubwa unahusishwa na watu wenye madaraka ya kisiasa, taaluma, wenye uwezo wa kifedha na kiuchumi ambao hutumia uwezo huo kujineemesha na kujipatia mafao na masilahi wasiyostahili, hasa kwa njia za kihalifu na kuvunja sheria za nchi na kimataifa.
Hata hivyo, taasisi na mashirika makubwa ya uchumi ya Kimataifa yanatumiwa na wajanja kuendeleza vitendo vya uhalifu na kifisadi. Pale mashirika na taasisi yanapobanwa na ufisadi wao kutambuliwa, hutafuta njia za kutokea. Kama kawaida hutatafutwa mbuzi wa sadaka (bangusilo) ili kutuliza mizimu.
Taaasisi ya Kimataifa ya Uchunguzi na Uraghibishaji dhidi ya Vitendo va Rushwa (Corruption Watch) imefanya uchambuzi wa kina na kutoa angalizo, mapitio na maoni kuhusu kuhusika kwa benki ya kimataifa ya Standard iliyoko London katika ufisadi ambao benki hiyo imekiri na kujishtaki kwa vyombo vya uchunguzi wa makosa makubwa ya jinai (SFO).
Uamuzi huo umefanywa kwa msingi wa sheria za Uingereza (Deferred Prosecution Agreement). Kwa mujibu wa sheria hiyo, taasisi au shirika la biashara linapogundua kwamba ndani yake kuna makosa ya jinai yaliyotendeka, huchukua hatua za kutafuta makubaliano na upande wa mashtaka ili tuhuma ziainishwe na mahakama itoe adhabu kwa kuzingatia kwamba mhusika anachotaka kufanya ni kurekebisha tabia yake na arudi katika njia iliyochaguliwa ya kutii sheria.
Mambo mengi yameandikwa na watu wameshangaa kwa Tanzania kujikuta katika kashfa na ufisadi mwingine wa mabilioni ya fedha kuchotwa kwa ushiriki wa Benki ya Standard kwa kupitia benki yake ya hapa nchini. Mpango wenyewe ulikuwa kwamba Standard inunue dhamana ili upatikane mkopo wa Dola 600 milioni za Marekani (sawa na Sh1.4 trillioni) kwa Serikali ya Tanzania kwa ajili ya shughuli za maendeleo.
Kesi hii, ambayo ina mchakato mrefu tangu mwaka 2011, imehusisha mawaziri wawili: Mustafa Mkullo na marehemu Dk William Mgimwa kwa nyakati tofauti. Kilicho wazi ni kwamba Tanzania inahitaji utaalamu wa kujifunga katika mikataba mikubwa ya kimataifa; iwe ya madini, uchimbaji gesi na ununuzi, benki na kampuni za kimataifa zinatambua udhaifu huo na licha ya kuutambua, kila mara yako kwenye maabara ya kubuni bidhaa mpya kwa madhumuni ya kujiongezea faida katika biashara zao, bila kujali gharama watakayopata washirika na wateja wao.
Katika hili la Benki ya Standard, kuna mambo muhimu ambayo ni muhimu wasomaji wayajue. Yale ambayo Benki ya Standard imeyafanya kuyaandika na kuyasambaza ni upande mmoja wa shilingi. Lakini kwa kuyazingatia na kujua matukio na kuyapa matukio hayo tafsiri kama ilivyofanya Corruption Watch ndiyo njia sahihi ya kuwahabarisha Watanzania na Serikali ya Awamu ya Tano kwamba nyuma ya pazia la sakata la Benki ya Standard kuna mengi yamefunikwa.
Tunayaandika na kuyaelezea ili yajulikane, haki itendeke na Tanzania isiendelee kuwa uchochoro wa mtaji wa kimataifa.
Mambo ya kuzingatia katika mfululizo wa makala haya ni kama ifuatavyo: Benki ya Kimataifa ya Standard ambayo inamiliki na kudhibiti benki za Standard na Stanbic Tanzania ni mojawapo ya taasisi kubwa za kibenki duniani yenye kufanya shughuli zake kubwa kwenye Jiji la London.
Shughuli zake nyingine kubwa ziko pia New York, Frankfurt, Hong Kong na Johannesburg nchini Afrika Kusini. Ina leseni ya kufanya biashara ya kimataifa ya kibenki jijini London na kwingineko. Kimuundo na kiutawala, habari, shughuli na ruksa kwa kila kitu kinachofanyika kinapelekwa London kwa uamuzi na maelekezo.
Hakuna kinachoweza kufanyika bila ya ruksa kutoka London. Hivyo lilipotokea hili la tuhuma na madai kuhusiana na kutoa rushwa ili Benki ya Standard ipewe zabuni na Serikali ya Tanzania, benki hiyo ilijua wapi pa kukimbilia ili kujikosha.
Benki hiyo ilikimbilia kwenye vyombo vya sheria vya Uingereza (Serious Fraud Office) SFO na “kujishtaki” kwa msingi wa sheria ijulikanayo kama Deferred Prosecution. Sheria hii inatoa nafasi kwa mhusika kukiri mbele ya vyombo vya uchunguzi wa makosa ya jinai na kutoa maelezo yote ya hujuma bila kushurutishwa na mwishowe kukubali kushitakiwa, kwa mategemeo kwamba mhusika atapewa adhabu isiyo kubwa ili aweze kurekebisha tabia na kurudi kwenye mstari.
Swali la kujiuliza ni kwa nini Standard iliamua kujishtaki au “kujilipua” kwa Kiswahili cha kileo? Bila kuingia kwa undani, ni wazi benki hiyo ilijua fika kwamba kama ingelishtakiwa kwa njia za kawaida, kosa la kutoa rushwa ili kupata zabuni ni kubwa kwa sheria za Uingereza na hivyo adhabu yake ni kubwa.
Hapa tunafikiria adhabu ambayo inaweza kutolewa kuwa ni pamoja na kufungiwa leseni ya kufanya biashara ya kifedha katika Jiji la London. Adhabu nyingine ambazo zinaweza kutolewa ni pamoja na kutozwa faini kubwa kama inavyofanyika Marekani. Vilevile kuamriwa kurejesha mkopo wa Dola 600 milioni na gharama nyingine kwa wale wafanyabiashara binafsi walionunua dhamana.
Kubwa ya yote ni pamoja na uwezekano wa kukwama kwa mpango wa uliokuwa umeshatayarishwa wa kuiuza Benki ya Standard kwa Wachina kwa sababu benki ingeingia matatani na thamani yake kwenye soko kupungua. Kwa kifupi hayo ndiyo mambo yaliyokuwa yanaisumbua Benki ya Standard hadi ikabuni mkakati wa kujikwamua.
Mkakati wa Benki ya Standard ulisukwa kiufundi. Benki iliamua kujishtaki kwa SFO. Mkakati huu ulilenga kuhamisha kosa kutoka Benki ya Standard Kimataifa na kutwisha zigo benki zake za Stanbic na Standard zilizoko Tanzania, kwa madai kwamba maofisa wake wakuu walificha habari, hasa kuhusu shirika binafsi la kitaaluma la masuala ya fedha (EGMA), ambalo linadaiwa liliingizwa kinyemela katika mchakato wa Benki ya Standard kutafuta zabuni na katika majadiliano.
Kutokana na Standard kujishtaki, matatizo mengi tuliyoyaainisha hapo mwanzoni yametafutiwa ufumbuzi. Kwanza, mahakama katika uamuzi wake imetamka wazi kwa kukubaliana kwamba benki hiyo ya kimataifa na wala maofisa wake hawakuwa na hatia ya kuhusika moja kwa moja katika uvunjaji wa sheria kwa kutoa rushwa kwa maofsa wa Serikali ya Tanzania ili benki ipate zabuni ya kuipatia Serikali mkopo huo wa Dola 600 milioni.
Hata hivyo, mzigo wa nani alitoa rushwa kwa maofsa wa Tanzania zimetupiwa taasisi za mamlaka nchini Tanzania. Wale maofisa wa Benki ya Standard na Stanbic Tanzania eti ndiyo wana hatia.
Kwa kiasi kikubwa ripoti ya Corruption Watch inaibua maswali kuhusu jinsi Benki ya Standard ilivyotoa habari nusu na zinazojikanganya kuhusu kuhusika kwake katika mchakato mzima na kwa hakika ni wazi kwamba wale ambao sasa wanatajwa katika hukumu ya Jaji wa Mahakama ya Uingereza katika kesi ya Benki ya Standard kujishitaki kwa uvunjifu wa sheria yawezekana kabisa ni mbuzi wa kafara hasa kwa kuzingatia nani ana mamlaka na kwa lipi katika biashara hizi kubwa za kimataifa? Je, ni makao makuu au matawi yake?
Kampuni binafsi ya EGMA ilitoka wapi katika mchakato? Tanzania kweli imefidiwa ipasavyo kwa uamuzi wa mahakama ya Uingereza? Haya ni maswali tutakayojibu katika matoleo yajayo ya makala haya.     

No comments :

Post a Comment