dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Wednesday, April 13, 2016

Ombaomba Dar Wamjibu Makonda, Wasema Hawaondoki MJINI Ng'oo


OMBAOMBA katika jiji la Dar es Salaam wamemjibu Mkuu wa Mkoa, Paul Makonda wakisema hawawezi kuondoka kwa vile ‘mjini kila mtu ana kazi yake’.

Wamesisitiza kuwa hawawezi kuondoka Dar es Salaam kwa sababu wamekuja kutafuta kipato.

Baadhi ya ombaomba walitoa kauli hiyo kwa nyakati tofauti jana, baada ya Gazeti hili kutaka maoni yao kuhusu tamko la Makonda kwamba atafanya operesheni ya kuwakamata Aprili 18 mwaka huu.

“Mimi siwezi kurudi Dodoma kwa sababu nauli ni kubwa. Nilikuja jana kwa kulipa Sh 20,000 sasa mimi nitapata wapi fedha nyingine? Kama anataka tuondoke atupatie nauli.“Kama hawezi kutupatia nauli atupeleke popote sisi tutaendelea kuomba tuweze kujipatia kipato kwa ajili ya kujikimu maisha.

“Kama unavyoniona mimi na familia yangu nimekimbia Dodoma kutokana na mafuriko… sasa wakiniambia nirudi nitaenda wap?.

Pamoja na kunipatia nauli wanifanyie mpango wa nyumba ya kuishi,” alisema mmoja wa ombaomba hao, Amina Ramadhani aliyekuwa eneo la Mnazi Mmoja.

Mwingine aliyekuwa amekaa na watoto wake wanne na ambaye hakutaka jina lake litajwe alisema: “Kila mmoja na kazi yake hapa mjini.

“Sisi tutaendelea kuomba kwa sababu ndiyo kazi yetu inayotupatia kipato cha kuendeshea familia zetu”.

Ombaomba mwingine ambaye naye alikuwa eneo la Mnazi Mmoja na pia hakutaka kutaja jina lake alisema viongozi wa Serikali nao ni wazazi kwa hiyo wanapaswa kuangalia namna ya kuwasaidia.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Makonda alisema muda wa ombaomba katika jiji umekwisha hivyo amewataka kufungasha virago vyao na kurudi makwao.

Alisema amefanya utafiti na kugundua kuwa asilimia 80 ya ombaomba wanatoka nje ya Mkoa wa Dar es Salaam na asilimia 20 ni wakazi wa jiji.

Makonda alieleza masikitiko yake kuwa ombaomba hao wamekuwa wakiwatumia watoto wao kuomba ili kujipatia kipato.

“Ombaomba wote wafahamu kwamba mji unapaswa kuwa safi na wale wanaokaa katika makutano ya barabara au nje ya maduka ya watu kwa ajili ya kuomba, watambue kwamba muda huo umekwisha, wanapaswa kurudi katika mikoa yao.

“ Wafanyabiashara wengi wamekuwa wakiwalalamikia ombaomba wanaolala kwenye milango ya biashara zao kwamba hujisaidia hapo hapo hali inayochafua mazingira na kusababisha usumbufu mkubwa.

“Sasa ninasema ombaomba hawa wamekuja kwa nauli zao hivyo wataondoka kwa nauli zao… nitakayemkamata katika operesheni yangu nitakayoifanya Jumatatu nitamchukulia hatua za sheria ikiwa ni pamoja na kumfikisha mahakamani,” alisema Makonda.

Naye Kamanda wa Polisi Kanda ya Dar es Salaam, Simon Sirro, alisema ombaomba ni wengi katika jiji na wanaopaswa kufuatilia watu hao ni viongozi wa Serikali za mitaa lakini wamekaa kimya.

“Wenyeviti wa Serikali za mitaa ni wajibu wao kuwashauri watu hawa hivyo tunawaomba wafanye hivyo kabla mkuu wa mkoa hajaanza kufanya operesheni hiyo,” alisema.

Wakati huo huo, Makonda amewataka wote waliojenga maghorofa bila kutenga maeneo ya kuegesha magari, wayabomoe la sivyo watafute maeneo mengine kwa ajili ya maegesho.

“Majengo makubwa yanapaswa kuwa na maegesho. Ninashangaa kuona magari yameegeshwa ovyo ndani ya jiji hasa pembezoni mwa barabara hali inayosababisha watembea kwa miguu kukosa maeneo ya kupita kutokana na magari hayo.

“Hii ni hatari kwa sababu mtu anaweza kugongwa kutokana na uzembe wa watu wasiozingatia sheria,” alisema Makonda.

Pia aliwataka wamiliki wa baa kufuata sheria za leseni zao na kufunga muda waliopangiwa

No comments :

Post a Comment