dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Sunday, April 3, 2016

Tendwa: CCM hii inaweza kuanguka

Aliyekuwa Msajili wa vyama vya siasa nchini, John Tendwa akizungumza na waandishishi wa gazeti hili, jijini, Dar es Salaam hivi karibuni. Picha na Said Khamis
By Fidelis Butahe, Mwananchi
Dar es Salaam. Tangu mwaka 1995 vyama vya upinzani vimekuwa vikisimamisha wagombea urais katika Uchaguzi Mkuu bila ya mafanikio, lakini John Tendwa anawataka wasikate tamaa kwa kuwa CCM inaweza kuanguka.
Tendwa, ambaye alikuwa Msajili wa Vyama vya Siasa, amesema demokrasia nchini inakuwa kwa kasi na hivyo kuna siku upinzani unaweza kushinda lakini itategemea na mahitaji ya wakati huo sambamba na kuibuka na hoja ambazo CCM watakuwa wameshindwa kuzitekeleza.
Mwanasheria huyo, ambaye alistaafu Agosti mwaka 2013, alitoa kauli hiyo katika mahojiano maalumu na waandishi wa gazeti hili ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
“Niwambieni ukweli kama CCM isingekuwa na mgombea mzuri anayeweza kujieleza na wasingekuwa na ilani nzuri ambayo wameweza kuiuza, huwezi kujua pengine Ukawa ingeweza kuchukua madaraka,” alisema Tendwa ambaye alishikilia nafasi ya Msajili wa Vyama kwa miaka 13.
Katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 25 mwaka jana, CCM ilimsimamisha Dk John Magufuli kugombea urais akipambana vikali na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa wa Chadema ambaye aliungwa mkono na vyama vinavyounda Ukawa.
Katika uchaguzi huo uliokuwa na msisimko mkubwa, Dk Magufuli alishinda kwa kupata kura milioni 8.8 (asilimia 58.47), akifuatiwa na Lowassa aliyepata kura milioni 6.07 (asilimia 39.97), zikiwa ni zaidi ya mara mbili ya kura ambazo wapinzani wamewahi kupata tangu uchaguzi wa vyama vingi urejeshwe mwaka 1995.
“Kama unataka kuzingatia demokrasia hakuna nchi duniani ambayo unakuta chama kinaongoza milele. Mfano Marekani kuna vyama vya siasa zaidi ya 53 ila vikubwa ni Democratic na Republican ambavyo licha ya kuungwa mkono na vyama vidogo, pia vyama hivyo vinapokezana kuongoza nchi,” alisema Tendwa.
“Kwa nini Dar es Salaam wabunge wengi wa CCM wameshindwa? Kwa mara ya kwanza tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa miaka 23 iliyopita, Jiji limekwenda upinzani na hivi karibuni Naibu Meya atachaguliwa na huenda akawa wa upinzani kwa sababu wana wapigakura wengi labda kuwe na ushirikiano.”
“Kama huo ndiyo mwanzo, nini kitafuata baadaye?” alihoji na kusisitiza kuwa ushindi huo wa upinzani katika jiji hilo ni somo tosha.
Tendwa alisema hayo wakati Rais Magufuli anaonekana kutekeleza mambo mengi ambayo wapinzani walikuwa wakipigia kelele kwenye serikali zilizopita, kama kuboresha bandari, kubana matumizi kwa punguza safari za nje za viongozi na kupambana na rushwa na uzembe kazini.
Hata hivyo, mbinu zake za kutekeleza hayo zimekuwa zikikosolewa, hasa utumbuaji majipu ambao wapinzani wamekuwa wakieleza kuwa haufuati taratibu, kubana matumizi kwa kufuta safari za nje na kupunguza mishahara ya vigogo wa taasisi kubwa za Serikali. Pia, uamuzi wa hivi karibuni wa Shirika la Changamoto za Milenia (MCC) kuinyima Tanzania mkataba wa miradi ya maendeleo kutokana na kuamini kuwa uchaguzi wa Zanzibar haukuwa shirikishi, umechukuliwa na wapinzani kama Serikali kushindwa kusimamia demokrasia.
Tendwa hakuacha kugusia sakata la uchaguzi wa meya wa Dar es Salaam ulioahirishwa mara tatu kabla ya Rais Magufuli kuingilia kati, akitaka CCM na Ukawa kutoendelea kuyumbisha na kushauri kila upande kuwa tayari kukubali matokeo.
“Ilikuwa vizuri rais kuingilia maana hii ni nchi yetu na hili ni jiji letu. Kama upinzani wamepita waache, wapite na tukubali kuwa hiyo ndiyo demokrasia. Kama CCM imeshindwa, mkubali,” alisema huku akibainisha kuwa CCM ndiyo chama chake.
Alisema baada ya Meya wa Jiji, Isaya Mwita kupatikana ni wazi kuwa Dar imepata meno na kuvitaka vyama vya siasa kuachana na dhana kuwa Serikali iliyopo madarakani ni ya CCM.
“Kila chama kina wajibu wa kushirikiana na wananchi katika kusukuma maendeleo na wasibweteke kwamba CCM wapo peke yao kwa kuwa upinzani kuna viongozi pia,” alisema Tendwa.
“Kwa sasa Jiji lipo upinzani hivyo wafanye kazi maana hii ndiyo serikali yao ya kwanza na waonyeshe umahili ili wakienda katika uchaguzi wawe na sera ya kusema.” Alipoulizwa kuhusu viongozi kuhama vyama kama ilivyokuwa wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 2015, Tendwa alisema: “Kuhama chama ni afya katika demokrasia. Nchi ya Marekani haina wanachama waanzilishi wa vyama na ndiyo nchi inayosifika kwa demokrasia duniani.”
Alisema watu wanabadilika kutokana na mambo wanayooona kuwa na manufaa kwao kwa wakati husika huku akitoa mfano wa vyama vikubwa viwili vya nchi hiyo.
Alikitoa mfano wa mbunge wa Bunda, Ester Bulaya aliyeihama CCM na kujiunga na Chadema, Tendwa alisema wanasiasa waliohama wameongeza ushindani wa kisiasa.
“Ni wakati wake (Bulaya) wa kufanya yale aliyokuwa akiyakosoa yaonekane kwamba ni sahihi na kweli wapigakura waseme kuwa ameyatekeleza,” alisema.

No comments :

Post a Comment