dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Friday, October 28, 2016

Muuguzi ammwagia kemikali mzazi!

MKAZI wa wilayani Itilima mkoani Simiyu, Matilda Maghembe (16) amelazwa katika Hospitali Teule ya Mkoa ya Somanda mjini Bariadi, baada ya kudaiwa kumwagiwa mwilini dawa ya kimiminika aina ya Lysol na muuguzi katika Zahanati ya Sunzula baada ya kujifungua.

Kutokana na madhara hayo, Matilda, mkazi wa kijiji cha Sunzula amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) katika Hospitali ya Somanda.

Tayari Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amemwagiza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu kufuatilia tukio hilo la Oktoba 16 mwaka huu, baada ya kupata taarifa na kuona picha kupitia mitandao ya kijamii.

Chanzo cha hasira za muuguzi huyo ambaye jina lake halijafahamika, kimetajwa ni kushindwa kuelewana katika malipo na mama wa Matilda, Hungwa Mahangwa (50) anayedaiwa kuombwa Sh 6,000 na muuguzi, ilhali mama huyo akiwa na Sh 5,000.Wakizungumza katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa mkoani hapa alikokuwa amelazwa Matilda kabla ya kuhamishiwa Hospitali ya Somanda, ndugu wa mgonjwa huyo wamemtuhumu muuguzi wa zahanati hiyo kwa kitendo cha kinyama alichokifanya.

Walidai Matilda alifika katika zahanati hiyo na kujifungua salama mtoto wa kiume Oktoba 14, mwaka huu na kutakiwa kurudi siku iliyofuata ili kutolewa gozi aliyowekewa baada ya kuonekana alikuwa akivuja damu baada ya kujifungua na kuruhusiwa kurudi nyumbani.

Walidai hawakurudi siku ile waliyoelezwa na hivyo kurudi Oktoba 16, mwaka huu akiwa amefuatana na mama yake mzazi, jambo ambalo lilionesha kutomfurahisha muuguzi huyo ambaye alianza kuwatolea lugha chafu ya matusi.

“Tulielezwa tumrudishe katika zahanati hiyo mgonjwa siku iliyofuata, lakini tulizidisha siku moja maana tulikosa usafiri sasa tulipofika alianza kututolea lugha ya matusi,” alisema mama wa Matilda.

Alidai walikubali kumpokea mgonjwa huyo na kuanza kumpatia matibabu akiwa kitandani ndipo muuguzi huyo alipoomba fedha Sh 6,000, lakini wao wakawa na Sh 5,000 jambo ambalo lilionekana kutomfurahisha na hivyo kuingia chumba kimojawapo na kutoka na kopo lililokuwa na dawa hiyo na kummwagia mwilini mgonjwa huyo aliyelia kwa uchungu na hatimaye kupoteza fahamu.

Alisema baadaye bintiye alizinduka, lakini alikuwa akilia kutokana na maumivu baada ya kuungua vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake zikiwemo makalio, mapaja na sehemu za siri na hivyo muuguzi huyo kuwashauri wampeleke katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa kwa matibabu zaidi kwa madai kuwa ameishiwa maji.

Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Dk Luguga Vedastus alikiri kumpokea mgonjwa huyo tangu Oktoba 21, mwaka huu na hivyo kabla ya rufaa alitaka ajiridhishe kwa kupata taarifa zaidi kutoka kwa mwenzake wa Itilima, lakini wakati akiendelea na mawasiliano, alipigiwa simu kutoka wizarani wakitaka kufahamu kwa undani suala hilo.

Akizungumzia sakata hilo, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dk Magenda Kihulya alikiri tukio hilo na kueleza dawa aliyomwagiwa inatumika kusafishia sakafu ili kuua wadudu wanaoeneza magonjwa ya kuambukiza kama kipindupindu na haifai kwenye mwili wa binadamu, kwani ni kali kama tindikali.

“Ni kweli tukio lipo na mgonjwa tunaye hapa hata sisi hatukuwa na taarifa hizi tumepigiwa simu toka wizarani hivyo tunachokifanya tunaondoka na mgonjwa hadi mjini Bariadi kwa matibabu zaidi huku tukiendelea kutafuta muuguzi aliyefanya kitendo hiki,” alisema.

No comments :

Post a Comment