dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Monday, November 7, 2016

‘Makaburi’ 7 magumu kwa JPM kuyafukua!



Rais John Magufuli 

Dar es Salaam. Kauli ya Rais John Magufuli kwamba hawezi kuyafukua makaburi yote, imetafsiriwa na wachambuzi wa duru za kisiasa kuwa pengine alilenga kashfa nzito za kifisadi zilizowahusisha vigogo katika Serikali zilizopita.

Rais alitoa kauli hiyo Ijumaa katika mkutano na waandishi wa habari uliolenga kutathmini mwaka mmoja wa utawala wake tangu aapishwe Novemba 5 mwaka jana.

Rais Magufuli, ambaye amejipambanua kuwa ni mtu anayepambana na ufisadi bila ya kuogopa mtu, alikuwa akijibu swali aliloulizwa na mwandishi wa kituo cha televisheni cha TBCI, Anna Kwambaza aliyetaka kufahamu kiongozi huyo wa nchi anaona tofauti gani katika matarajio aliyokuwa nayo kabla ya kuingia Ikulu na hali halisi aliyoikuta.

“Siwezi kuyafukua makaburi yote kwa sababu kuna mengine nitashindwa kuyafunika. Ninachofanya ni kutekeleza katika kipindi changu yale ambayo nilitakiwa kuyatekeleza kwa ajili ya wananchi, ndiyo maana naomba tushikamane,” alisema.

Kauli hiyo imekuja wakati Rais akiwa ameshachukua hatua kadhaa dhidi ya watendaji wanaotuhumiwa kuhusika katika ufisadi uliofanywa wakati wa utawala wa Serikali zilizopita na sasa amefanikisha kuanzishwa kwa Mahakama ya mafisadi kufanikisha juhudi zake.

Kauli za wachambuzi


Lakini kauli kwamba hataweza kufukua baadhi ya makaburi kwa kuwa anaweza asifanikiwe kuyafunika, imepokelewa kwa hisia tofauti na wachambuzi waliofuatwa na Mwananchi kutoa maoni yao.

Wachambuzi hao walitaja kashfa kama za uchotaji wa fedha kutoka akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) iliyokuwa Benki Kuu, ununuzi wa Rada, mkataba wa ufuaji umeme wa dharura kwa kampuni ya Richmond, uchotaji fedha kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow, Meremeta, Kagoda na hata fedha zilizolenga kusaidia wananchi, maarufu kama “mabilioni ya JK”.

“Ili awe na uhusiano na viongozi waliomtangulia, hawezi kuyafukua (baadhi ya makaburi), au yeye mwenyewe kuonekana alihusika wakati akiwa waziri katika uongozi uliopita,” alisema Richard Mbunda kutoka Idara ya Sayansi ya Siasa ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

“Nadhani mazingira hayo ndiyo yanachangia asiweze kuyafukua.”

Mbunda alisema makaburi kama hayo yanatengeneza mazingira ya kumgusa moja kwa moja na mengine kumchonganisha na viongozi waliomtangulia.

Maoni kama hayo yalitolewa na Profesa Mohammed Bakari kutoka Idara ya Sayansi ya Siasa ya UDSM aliyesema makaburi yanatokana na changamoto ya kimfumo.

“Au inawezekana waliohusika walimsaidia hata kisiasa hadi hapo alipofika ndani ya chama chake. Labda angekuwa upinzani ndiyo angeweza kuyafukua,” alisema.

Hata hivyo, katika mtazamo mwingine alisema ni kawaida kwa kiongozi anapoingia madarakani kutojihusisha zaidi na mambo yaliyofanyika katika kipindi kilichopita licha ya kufanyia mwendelezo wa mambo ya msingi kama vita dhidi ya rushwa.

Mwanaharakati wa haki za binadamu na mtetezi wa masuala ya kijinsia nchini kutoka Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Gemma Akilimali alisema kwa kuwa Rais ameshajipambanua kupambana na udhaifu, hatakiwi kuacha baadhi ya makaburi.

Alisema kufanya hivyo kunaweza kuathiri watu wanaoendelea kutuhumiwa kuhusika na kashfa hizo.

“Tafsiri ya makaburi hayo ni kwamba nchi ilikuwa imekufa, imejaa wafu, sera za nchi zimezikwa, sheria hazifanyi kazi na nchi iliendeshwa kiholela. Sasa kama amekuwa akilaani mikataba mibovu ya madini, na yeye ameshajipambanua kuwasaidia Watanzania, anawezaje kuacha makaburi hayo?” alihoji.

Rada


Miongoni mwa kashfa zilizotajwa kuwa ni makaburi ambayo Rais Magufuli hawezi kuyafukua ni ununuzi wa Rada ya kuongoza ndege kutoka Kampuni ya Bae System Uingereza. Rada ilinunuliwa kwa gharama kubwa zaidi ya uhalisia.

Uingereza ndiyo iliyobaini mchezo mchafu na kufanya uchunguzi uliosababisha Tanzania irejeshewe dola 29.5 milioni za Kimarekani (Sh73 bilioni) Novemba 2013, lakini waliohusika hawajachukuliwa hatua yoyote.

Tanzania ilinunua rada hiyo kwa dola 40 milioni za Kimarekani (Sh54 bilioni).

Aliyekuwa Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Andrew Chenge alijiuzuru kutokana na ununuzi huo kufanywa wakati akiwa Mwanasheria Mkuu.

Escrow

Pia, sakata la uchotwaji fedha kutoka akaunti ya Escrow limetajwa kama moja ya makaburi hayo. Katika sakata hilo lililoibuka bungeni mwaka 2014, Sh306 bilioni zilizokuwa kwenye akaunti ya Escrow iliyofunguliwa kusubiri mgogoro wa kimkataba baina ya Tanesco na kampuni ya ufuaji umeme ya IPTL kumalizika, zilichotwa katika mazingira yasiyoeleweka.

Fedha hizo zilichotwa ziliingizwa benki za Mkombozi na Stanbic na baadaye kuonekana kugawiwa kwa wanasiasa, wakiwemo mawaziri, majaji, viongozi wa dini na watumishi wa Serikali.

Hata hivyo, waliofahamika ni wale walioingiziwa mgawo kwenye akaunti zilizokuwa benki ya Mkombozi, lakini waliopewa fedha taslimu baada ya mabilioni kuchotwa Stanbic, hawajafahamika wala kuchukuliwa hatua.

Mei mwaka huu, Kambi ya upinzani iliibua sakata hilo bungeni huku ikihoji sababu za Rais John Magufuli kutotekeleza maazimio ya Bunge ya kumwajibisha Profesa Sospeter Muhongo, aliyejiuzulu kutokana na kashfa hiyo na badala yake kumteua tena kuwa Waziri wa Nishati na Madini.

Richmond

Licha ya Dk Harrison Mwakyembe kusema wakati wa kampeni Agosti mwaka jana akiwa jimboni kwake Kyela kuwa moto wa kashfa ya Richmond haujazimika, hadi sasa hakuna hatua zinazoonekana kuchukuliwa.

Dk Mwakyembe, ambaye alikuwa mwenyekiti wa Kamati ya Bunge iliyochunguza sakata la kuipa Richmond zabuni ya kufua umeme wa dharura mwaka 2008, aliliambia Bunge wakati wa majumuisho ya mjadala kuwa kamati yake haikusoma taarifa kamili ya suala hilo kwa hofu kuwa Serikali nzima ingeondolewa na kuomba uchunguzi mpya ufanyike ili yaibuliwe mengi zaidi.

Sakata hilo lililotokea mwaka 2008 baada ya Tanzania kukumbwa na upungufu mkubwa wa umeme mwaka 2006 na Serikali iliingia mkataba na Richmond Development Company LLC wa Sh172 bilioni. Edward Lowassa, aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, alijiuzulu na amekuwa akisema kuwa ushiriki wake ulitokana na maagizo kutoka juu.

Sakata la EPA

Wakati wa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2005 wafanyabiashara wakubwa wakidaiwa kushirikiana na vigogo wa Serikali, walidaiwa kuwa kuchota Sh133 bilioni kutoka akaunti ya EPA.

Hatua zilichukuliwa kwa baadhi ya maofisa wa Benki Kuu na wafanyabiashara wadogo ambao baadhi wamefungwa, lakini watuhumiwa wengine waliofanikisha ukwapuaji fedha hizo ama wameshinda kesi zao au wanaendelea na maisha uraiani baada ya kutakiwa na Rais Jakaya Kikwete kurejesha fedha hizo.

Kupitia sakata hilo, aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu, Daudi Balali alifukuzwa kazi na Rais Kikwete na akarudi Marekani ambako alikuwa na uraia wa nchi hiyo na baadaye akafariki dunia na kuzikwa huko.

Mabilioni JK

Mara baada ya uchaguzi mkuu wa 2005, Rais Kikwete alikuja na mpango maarufu wa mabilioni ya JK alizoahidi kwenye kampeni. Sh50 bilioni ziliwekwa benki ya NMB kwa ajili ya kukopesha wafanyabiashara wa kati ili kuendeleza biashara zao, lakini sehemu ya fedha hizo hazikurejeshwa na hakuna hatua zilizochukuliwa.

Taarifa ya Dk Mary Nagu, Waziri wa Uwezekezaji na Uwezeshaji aliyoitoa mwaka 2012, ilisema ni Sh43 bilioni tu kati ya Sh50bilioni zilizorejeshwa serikalini na wafanyabiashara waliokopa.

Aprili 24, mwaka huu, Takukuru ilinukuliwa na vyombo vya habari ikieleza kuanza kuchunguza fedha ambazo hazikurejeshwa.

Kashfa ya Kagoda

Katika sehemu ya Wizi wa EPA ulibainika wizi wa Sh40 bilioni uliofanikishwa na kampuni ya Kagoda Agriculture kwa kisingizio cha kufanya kazi za usalama.

Sh40 bilioni zilizokwapuliwa zilitoka BoT.

Sakata la Meremeta

Mwaka 2011 ulifanyika uchunguzi wa Bunge kuhusu ufisadi wa zaidi ya Sh205.9 bilioni unaodaiwa kufanywa kupitia kampuni ya Meremeta iliyokuwa ikimilikiwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Hoja inayotakiwa kufanyiwa kazi na Kamati ya Bunge ni kuchunguza uhalali wa malipo ya dola milioni 132 za Kimarekani (wastani wa Sh205.9 bilioni kwa viwango cha sasa vya kubadilishia fedha vya wakati huo) ambazo zilitoka BoT kwenda Ned Bank ya Afrika Kusini, ikiwa ni malipo ya mkopo wa dola 10 milioni za Kimarekani, uliokuwa umechukuliwa na Kampuni ya Meremeta Ltd, lakini hadi bunge linamaliza muda wake hakukuwa na taarifa juu ya kilichobainika na baadaye ilielezwa kuwa masuala hayo ni ya kijeshi.

/Mwananchi.

No comments :

Post a Comment