Waziri wa Afya Zanzibar, Mahmoud Thabit Kombo akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake Mnazimmoja katika kilele cha maadhimisho ya siku ya ugonjwa wa kisukari duniani. Picha na Makame Mshenga wa Maelezo Zanzibar.
Na Ramadhani Ali – Idara ya Maelezo, Zanzibar
Waziri wa Afya Zanzibar, Mahmoud Thabit Kombo amesema hadi sasa hakuna dawa yoyote duniani iliyothibitishwa kutibu ugonjwa wa kisukari.
Kadhalika, amewashauri watu waliyopata maradhi hayo kuwa karibu na madaktari kupata nasaha na miongozo sahihi itakayowasaidia katika kuimarisha afya zao.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Zanzibar, katika kilele cha kuadhimisha siku ya ugonjwa wa kisukari duniani, Waziri Mahmoud amesema ugonjwa huo ni hatari na ni miongoni mwa magonjwa makuu matano yanayoongoza kwa kuuwa watu wengi Zanzibar.
Hata hivyo, hakuyataja magonjwa mengine yanayoongoza kwa kuuwa watu wengi Zanzibar, lakini amesema kwa kawaida ugonjwa wa kisukari huchelewa kujitokeza dalili zake na zinapojitokeza tatizo tayari linakuwa kubwa.
Waziri huyo, amewataka wananchi kujenga utamaduni wa kupima afya zao mara kwa mara ili kama kuna dalili zozote wapate ushauri wa kitaalamu na hatimae kuepusha athari zaidi.
Mahmoud amesema kuwa maradhi ya kisukari yanaweza kukingwa kwa asilimia 80 iwapo wananchi watajiepusha na vihatarishi vinavyopelekea kupata ugonjwa huo.
Ametaja changamoto inayojitokeza katika maradhi hayo hivi sasa ni kuwa hata watoto wadogo nao wamekuwa wakipata ugonjwa huo kwa kasi.
Waziri huyo amesema kwa mujibu wa takwimu, wastani wa watoto 230 wamesajiliwa katika Hospitali ya Mnazimmoja na Abdalla Mzee na zaidi ya watoto 20 wamepoteza maisha kati ya mwaka 2010 hadi 2015.
Amesema tatizo jengine lililojitokeza kwa mujibu wa vipimo vilivyofanywa katika wizara nane za serikali, imegundulika kuwa idadi kubwa ya wafanyakazi wanakabiliwa na tatizo la kisukari.
Aidha, Waziri Mahmoud amewataka wananchi kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi na kuwa na utaratibu mzuri wa ulaji chakula kwani ni moja kati ya tiba nzuri ya ugonjwa wa kisukari.
No comments :
Post a Comment