dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Friday, June 30, 2017

Kisa cha Mwanamke aliyebakwa saa kadhaa kabla ya harusi yake!

Wakati Terry Gobanga, wakati huo akiitwa Terry Apudo alipotoweka katika harusi yake hakuna mtu aliyedhani kwamba alitekwa nyara ,kubakwa na kutuwa kandakando ya barabara akipigania uhai.
Lilikuwa janga la kwanza kati ya mawili kumkabili muhubiri huyo kijana .Lakini ni manusura.

Harusi iliopangwa ilitarajiwa kuwa harusi kubwa.

Nilikuwa muhubiri hivyobasi wanachama wote wa kanisa walitarajiwa kuhudhuria.
Mchumba wangu, Harry na mimi tulikuwa na furaha tulikuwa tunafunga ndoa katika kanisa la All Saints Cathedral mjini Nairobi na nilikuwa nimekodisha rinda zuri sana la harusi.

Lakini usiku kabla ya ndoa yetu ,niligundua kwamba nina baadhi ya nguo za Harry .

Hakuweza kuja katika harusi bila tai kwa hivyo rafiki yangu mmoja ambaye alikuwa amekubali kubaki nami usiku wa kuamkia harusi alikubali kumpelekea mapema alfajiri.

Niliamka mapema na kumpeleka hadi katika kituo cha kupanda basi.
Nilipokuwa nikirudi nyumbani ,nilipita karibu na mtu mmoja ambaye alikuwa ameketi kati boneti ya gari na akanishika kutoka nyuma na kuniingiza katika viti vya nyuma vya gari hilo na kuondoka mahali hapo.
Yote haya yalifanyika katika chini ya sekunde moja .Nilifunguliwa mdomo na kuwekwa kipande cha nguo mdomoni.

Nilikuwa nikirusha mikono na miguu nikitaka kupiga kelele.Nilipofanikiwa kutoa kitambara hicho nilipiga kelele: Ni siku yangu ya harusi! hapo ndipo nilipopigwa ngumi .

Mmoja ya wanaume hao wakaniambia nishirikiane nao ama niuwawe.Wanaume hao walinibaka kwa zamu .

Nilihisi nitafariki ,lakini bado niliendelea kupigania uhai wangu, hivyobasi mtu mmoja alipotoa kitambara kilichokuwa mdomoni mwangu nilimuuma uume wake.

Alipiga kelele kwa uchungu na mmoja wao akanidunga kisu tumboni.
Baadaye walifungua mlango na kunitupa kando ya barabara huku gari likiendelea kwenda.Nilikuwa mbali na nyumbani ,nje ya jiji la Nairobi .

Ilikuwa zaidi ya saa sita baada ya kutekwa.Mtoto mmoja aliniona nikirushwa nje ya gari na akamweleza bibiye.

Watu walikuja mbio .Wakati maafisa wa polisi walipokuja walijaribu kuangalia iwapo bado ninapumua ,lakini hawakupata.

Wakifikiri nimefariki walinitia katika blanketi na kuanza kunipeleka katika chumba cha kuhifadhi maiti .

Lakini njiani nilikohowa. Polisi mmoja alisema: Bado hajafariki ,hivyobasi wakabadilisha njia ya kuelekea katika chumba cha kuhifadhi maiti na kunipelekea katika hospitali kuu ya serikali nchini Kenya.

Niliwasili nikiwa na mshangao mkubwa, nikizungumza mambo nisioelewa.Nilikuwa nusu uchi nikivuja damu huku sura yangu ikiwa na majeraha kutokana na kipigo nilichopata.

Lakini kuna kitu kimoja kilichomshtua mwanamke aliyekuwa akisimamia matibabu ,kwa sababu aligundua mimi ni bibi harusi.

''Twendeni kanisani tuone iwapo wanamkosa bibi harusi'', aliambia wauguzi.

Kwa bahati kanisa la kwanza waliloulizia ni All Saints Cathedral jijini nairobi ambapo waliambiwa kwamba kulikuwa na harusi mwendo wa saa nne Asubuhi lakini bibi harusi hakuonekana.

Wakati nilipokuwa nikisubiriwa kuingia kanisani ,wazazi wangu walikuwa na wasiwasi.
Watu walitumwa kunitafuta .Kulikuwa na uvumi. Wengine walishangazwa. Je alibadili nia? Wengine walisema haiwezekani kwamba yeye alifanya hivyo.

Baada ya saa chache walilazimika kuondoa mapambo ili kutoa nafasi kwa sherehe ya pili.
Harry alikuwa amewekwa katika eneo moja ambapo alikuwa akisubiri.Wakati waliposikia kule nilikokuwa wazazi wangu waliwasili katika hospitali wakiwa na watu wote
.Harry alikuwa akibeba rinda langu la harusi. Vyombo vya habari vilikuwa vimeambiwa kuhusu kisanga hicho na pia viliwasili katika hoispitali.

Nilipelekwa katika hospitali nyengine ambapo nilipata haki yangu ya faragha.
Hapo ndipo madaktari waliponishona na kunipa habari mbaya. Jereha la kisu katika tumbo langu lilikuwa ndani ya kizazi changu.

''Kwa hivyo hutaweza kushika mimba''.Nilipewa dawa ya kuzuia mimba pamoja na ile ya kuzuia virusi vya ukimwi.

Ubongo wangu ulikataa kukubali kile kilichotokea. Harry aliendelea kusema kuwa angependa kufunga ndoa nami.

''Nataka kumuuguza ili kuhakikisha kuwa anapata afya njema, katika nyumba yetu'',alisema.
Ukweli usemwe, sikuwa katika hali ya kuolewa ama kukataa kwa sababu akili yangu ilikuwa imejawa na nyuso za watu watatu walionibaka na kila kitu kilichotokea.

Siku chache baadaye, wakati nilipoanza kupata fahamu niliweza kumuangalia katika macho yake.
Niliendelea kusema pole. Nilihisi kana kwamba nilikuwa msaliti.

Watu wengine walisema kuwa ilikuwa tatizo langu kwa kuondoka nyumbani alfajiri. Iilkuwa uchungu mwingi sana lakini familia yangu na Harry walinisaidia.

Polisi walishindwa kuwakamata wabakaji. Nilienda katika gwaride la kuwatambua watu hao katika vituo vya polisi lakini sikufanikiwa na nilihisi uchungu kila wakati nilipoenda.

Mwishowe nilienda katika kituo cha polisi na kusema ''Wajua nini'': Sitawahi kurudi tena nataka kuachana na tatizo hilo.

Miezi mitatu baada ya shambulio hilo niliambiwa sikuwa na viini vya ukimwi na nikafurahia sana, lakini wakaniambia ni sharti nisubiri miezi mitatu baadaye nithibitishe.

Lakini mimi na Harry tayari tulikuwa tumeanza mipango ya harusi yetu ya pili.
Ijapokuwa nilikasirishwa na vyombo vya habari ,mtu mmoja alisoma habari yangu na kutaka kukutana nami.

Jina lake ni Vip Ogolla ambaye pia naye alikuwa manusura wa ubakaji.
Tulizungumza na aliniambia kwamba yeye na rafikize walitaka kunifanyia sherehe.''Jiachilie fanya chochote utakacho'',alisema.

Nilichagua keki ya aina yake .Keki ya ghali. Mbali na rinda ambalo lilikuwa nimekodisha sasa nilinunua na kuwa langu.

Mnamo mwezi Julai 2005, miezi saba baada ya mipango ya harusi yetu ya kwanza, mimi na Harry tulifanikiwa kufunga ndoa na tukaenda katika kusherehekea fungate yetu.

Siku 29 baadaye tulikuwa nyumbani wakati wa msimu wa baridi kali usiku mmoja.
Harry aliamua kuwasha jiko la makaa na kulipeleka katika chumba chetu cha kulala.
Baada ya chakula cha jioni aliliondoa kwa sababu chumba chetu kilikuwa na joto.
Nilijiingiza chini ya shiti huku yeye akifunga mlango.Wakati alipokuja kitandani aliniambia anahisi kisunzi, lakini hatukufikiria sana kuhusu hilo.
Ilikuwa baridi sana na hatukuweza kulala hivyobasi nilichukua blanketi jingine.
Lakini Harry akasema hakuliona kwa sababu hakuwa na nguvu nyingi. Mimi nami sikusimama.
Tulihisi kwamba kuna kitu kibaya.Tulilala nakumbuka nikimuita, mara nyengine aliitikia mara nyengine hakuitika.
Nilijilazimisha kushuka kitandani ambapo nilitapika na kupata nguvu .Nilitambaa hadi katika simu.
Niliwaita majirani zangu nikawaambia kwamba kuna kitu kibaya mume wangu haitiki.
Alikuja haraka, lakini ikanichukua muda mrefu kutambaa hadi katika mlango wa mbele ili kumfungulia huku nikiendelea kupoteza fahamu.
Niliwaona watu wengi wakiingia, wakipiga kelele. Na nikapoteza fahamu kwa mara nyengine.
Niliamka hospitalini na kuuliza kule ambapo mume wangu yuko.
Waliniambia kwamba wanamtibu katika chumba chengine.
Nilisema: Mimi ni muhubiri nimepitia mengi katika maisha yangu, nataka muniambie ukweli.
Daktari alianiangalia akaniambia mumeo hakufanikiwa.Sikuamini.
Kurudi kanisani kwa mazishi ya Harry lilikuwa tatizo kuu.
Mwezi mmoja uliopita nilikuwa katika kanisa hilo na rinda langu jeupe huku Harry akisimama mbele yangu akionekana mtanashati.
Sasa nimevaa mavazi meusi na Harry anaingizwa kwa jeneza.
Watu walidhani nimelaaniwa na kuwazuia watoto wao kunifikia. ''Ana bahati mbaya inayomfuata '',walisema.
Wakati mmoja karibia nikubali kwamba nina bahati mbaya.
Wengine walinituhumu kwa kumuua mume wangu.
Hilo liliniathiri sana nilikuwa na huzuni hadi kuchanganyikiwa.
Ukaguzi wa matibabu ulionyesha kile kilichotokea. Wakati moshi wa jiko ulipojaa chumbani alikosa hewa safi na kuaga dunia.
Nilihisi Mungu amenitenga. Sikuamini kwamba watu walikuwa wakicheka na kuendelea na maisha yao.
Siku moja nilikuwa nimeketi katika roshani nikiwaangalia ndege waliokuwa wakiruka na kusema: Mungu inawezekanaje unawalinda ndege hawa na sio mimi?

Wakati huo nilikumbuka kwamba kuna saa 24 kwa siku, nikiwa nimekaa ndani nikiangalia pazia , hakuna mtu anayeweza kukurejeshea saa hizo 24.

Kabla ugundue ni wiki moja , mwezi na mwaka umepotea. Huo ndio ulikuwa ukweli.
Niliambia kila mtu kwamba sitaweza kuolewa tena.

Mungu alimchukua mume wangu, na fikira za upweke zilikuwa nyingi na zenye uchungu mwingi, Kitu ambacho singependelea mtu yeyote kupitia.

''Uchungu huo ni mwingi, unahisi katika kucha zako.lakini kulikuwa na mtu mmoja Tonny Gobanga''.
Ambaye aliendelea kunitembelea. Alikuwa akinishinikiza kuzungumza kuhusu mume wangu na kufikiria kuhusu siku njema naye.

Siku moja hakunipigia simu kwa siku tatu na nilikasirika sana. Na hapo ndipo nilipogundua kwamba nimempenda.

Tonny alinichumbia na kutaka kunioa lakini nikamwambia anunue jarida ,asome stori yangu na kuniambia iwapo bado ananipenda.
Alirudi na kuaniambia kwamba bado angetaka kunioa.

Lakini nikasema: Sikiza kuna kitu chengine-siwezi kupata watoto kwa hivyo siwezi kuolewa nawe.
''Watoto ni baraka kutoka kwa mungu'', aliniambia. ''Iwapo tutawapata tutamshukuru mungu iwapo hatutawapata nitapata muda zaidi wa kukupenda''.

Nilifikiria ...''tamko zuri la kuvutia ! Hivyobasi nikakubali tufunge ndoa.
Tonny alienda nyumbani kuwaelezea wazazi wake ambao walifurahia hadi waliposikia stori yangu.
''Huwezi kufunga ndoa naye- amelaaniwa'',walisema. Babangu wa kambo alikataa kuhudhuria harusi yetu, lakini tuliifanya.

Tulikuwa na wageni 800 wengi walihudhuria ili kuniona.
Harusi hiyo ilifanyika miaka mitatu baada ya harusi yangu ya kwanza na nilikuwa muoga.
Wakati tulipokuwa tukiapishwa kanisani nilifikiri: Nimerudi tena hapa Mungu, tafadhali usimchukue mume wangu.

Wakati umati ulipokuwa ukituombea nililia kama mtoto.Mwaka mmoja baada ya ndoa yetu, nilijihisi vibaya na nikaenda kumuona daktari na kwa mshamgao mkubwa alinimbia Kwamba nina mimba.
Wakati miezi ilipoendelea kusonga nilitakiwa kupumzika kabisa, kutokana na kidonda kilichopo katika kizazi changu.

Lakini kila kitu kilimalizika vyema na tukapata mtoto wa kike ambaye tulimwita Tehille.
Miaka minne baadaye, tulipata mtoto mwengine kwa jina Towdah. Leo nimekuwa rafiki mkuu wa babangu wa kambo.

Niliandika kitabu ''Crawling out of darkness'' kuhusu yalionipata ili kuwapa watu motisha wa kujitoa katika majanga.
Pia nilianzisha shirika kwa jina Kara Olmurani.
Tunashirikiana na manusura wa ubakaji- kama ninavyowaita na sio waathiriwa wa ubakaji.
Tunatoa ushauri na usaidizi.Tunataka kununua nyumba ambayo tunaweza kuwaweka na kuanza tena maisha kabla ya kukabili ulimwengu.

''Nimewasamehe walio nishambulia .Haikua rahisi lakini nilibaini kwamba ninajiumiza zaidi na watu ambao hawajali''.

Imani yangu pia inanitaka kuwasamehe na kutolipiza kisasi na badala yake kulipa kwa kufanya mema.
Kitu muhimu ni kuomboleza. Pitia kila hatua. Jiumize hadi pale unapohisi kufanya kitu kuhusu hali yako.
Lazima uendelee kusonga mbele, tambaa iwapo unaweza. Lakini elekea katika hatma yako kwa sababu inakusibiri na ni lazima uende kuichukua.
/Muungwana.

No comments :

Post a Comment