dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Friday, December 21, 2012

Maazimio ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF)

Baadhi ya wahariri wa vyombo vyahabari mbali mbali nchini wakibadilishana mawazo muda mfupi baada ya kumaliza kikao chao huko Tanga
Baadhi ya wahariri wa vyombo vyahabari mbali mbali nchini wakibadilishana mawazo muda mfupi baada ya kumaliza kikao chao huko Tanga
Kwamba wahariri wameipitia kwa kina Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) na kubaini kuwa hakuna kifungu au neno lolote linalotamka UHURU WA VYOMBO VYA HABARI; Kwamba tumesikitishwa na kitendo cha Katiba ya Tanzania kutotambua vyombo vya habari kabisa katika Katiba hii baada ya mabadiliko ya 14 ya Mwaka 2005;
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
MAAZIMIO YA MKUTANO WA JUKWAA LA WAHARIRI
(EDITORS RETREAT) ULIOFANYIKA TANGA
13-16, DESEMBA 2012
Wahariri wa Vyombo vya Habari nchini walikutana jijini Tanga kuanzia Desemba 13 – 16, 2012 kwa nia ya kupitia utendaji wa vyombo vya habari kwa muda wa mwaka mmoja uliopita.
Wahariri wamejadili masilahi mapana yanayogusa nchi hii katika tasnia ya habari na kusisitiza msimamo wa pamoja wa kujenga umoja, amani, upendo na mshikamano kwa taifa letu kwa masilahi ya utangamano wa nchi.
Mbali na ajenda za kitaaluma, wahariri wamejadili kwa kina ajenda ya msingi iliyobeba kaulimbiu ya Mkutano wa Wahariri wa Mwaka huu ambayo ni: KATIBA MPYA NA UHURU WA VYOMBO VYA HABARI
Baada ya mjadala wa kina, wahariri kwa pamoja wamekubaliana yafuatayo:
KUHUSU KATIBA NA SHERIA ZA HABARI
Kwamba wahariri wameipitia kwa kina Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) na kubaini kuwa hakuna kifungu au neno lolote linalotamka UHURU WA VYOMBO VYA HABARI;
Kwamba tumesikitishwa na kitendo cha Katiba ya Tanzania kutotambua vyombo vya habari kabisa katika Katiba hii baada ya mabadiliko ya 14 ya Mwaka 2005;
Kwamba kwa masilahi ya tasnia ya habari na uhuru wa vyombo vya habari na maendeleo ya nchi, tunataka Katiba Mpya inayoandaliwa iwe na Ibara Maalum inayotoa Uhuru wa Vyombo vya Habari (Freedom of the Media);
Kwamba kwa masilahi ya uwazi na maendeleo ya taifa hili, Wahariri wanataka Katiba Mpya iwe na ibara inayotoa Haki ya Kupata Habari kwa wananchi wote bila kubaguliwa wala kuwekewa vikwazo (Right to Information);
Kwamba Serikali sasa ikubali na kutunga sheria Huduma kwa Vyombo vya Habari (Media Service Bill) ambayo mapendekezo yake tayari yamepitishwa na wadau wa habari na kuwasilishwa Serikalini.
Pamoja na maazimio haya, TEF itaratibu maoni ya wahariri na waandishi wengine wa habari na kuyawasilisha kwenye Tume ya Katiba. Lakini pia tutashirikiana na taasasi nyingine za habari zinazoratibu maoni ya wanahabari ili kuhakikisha michango ya sekta yetu inazingatiwa katika katiba mpya.
Wahariri kwa kauli moja tunasisitiza nia yetu ya kushirikiana na Serikali kufanya kazi kwa weledi kwa masilahi ya taifa na maendeleo ya pamoja ya taifa letu na watu wake.
UTENDAJI WA VYOMBO VYA HABARI
Wahariri pia walijadili utekelezaji wa maazimio ya mkutano wa Arusha wa 2011 na kusisitiza umuhimu wa kuimarisha utendaji wa vyombo vya habari hasa katika vyumba vya habari kwa kufanya yafuatayo;
Kuimarisha usimamizi wa vyumba vya habari ili kuhakikisha kwamba taarifa na habari zote zinazoandikwa na kutangazwa zinazingatia maadili, kanuni na miongozo ya kitaaluma.
Kuepusha vyombo vya habari kuwa vyanzo cha migogoro na migongano baina ya watu, dini, vyama vya siasa, makabila, na/au taasisi zozote zile za kijamii.
Kuepuka kufanya kazi za dola kwa kutumia lugha kushtaki, kuhukumu na kutoa mapendekezo ya adhabu na badala yake kuripoti matukio halisi kwa ufasaha (facts with clarity) na kutoa nafasi kwa upande wa pili kujibu pale wanapotuhumiwa (right to reply).
Kuimarisha umoja miongoni mwa wahariri na vyombo vya habari kwa kuepuka kushambuliana na kutumika kama jukwaa la kukanusha taarifa zilizoandikwa na chombo kingine cha habari.
WAANDISHI NA UANDISHI WA HABARI
Wahariri walibaini udhaifu katika uandishi wa habari na kwamba habari nyingi hazikidhi vigezo vya kitaaluma hivyo kusababisha malalamiko kutoka kwa walaji. Hivyo waliazimia;
Kuwajenga waadishi wa habari chipukizi (mentoring) ili waweze kupata uzoefu wa kuwawezesha kukua kitaaluma, pamoja na kuwasaidia kubobea katika maeneo maalum (specialization).
Wahariri washawishi wamiliki/waajiri kutenga bajeti kwa ajili ya mafunzo kwa waandishi wa habari, pamoja na kutumia fursa zinazotolewa na mfuko wa kufadhili vyombo vya habari (Tanzania Media Fund – TMF) ili kupata fedha za kuwaendeleza waandishi wa habari na kuimarisha utendaji katika vyumba vya habari.
Wahariri wasimamie maslahi ya waandishi wa habari ndani ya vyumba vyao vya habari ili kupunguza uwezekano wa waandishi hao kurubuniwa kwa fedha au zawadi nyingine.
RADIO NA TELEVISHENI
Wahariri walibainisha kwamba hawaridhishwi na aina ya uandishi na utangazaji unaofanywa na vituo vingi vya redio nchini na kwamba kuna ukiukwaji wa maadili ya taaluma, hivyo waliazimia yafuatayo:
Kuwashauri waajiri au/na wamiliki wa vyombo vya habari kuzingatia vigezo vya kitaaluma pale wanapoajiri mameneja wa vipindi na watangazaji katika vituo vya redio.
Kurekebisha vipindi vya usomaji wa magazeti kwenye Televisheni na Radio kwa kuwataka waache mtindo wa kusoma kila kitu, na badala yake wafanye udondozi tu.
VYUO VYA UANDISHI WA HABARI
Wahariri pia walijadili suala la utoaji wa elimu ya uandishi wa habari nchini hasa kuhusu mitaala inayotumiwa na vyuo vya uandishi wa habari vya kati na kuazimia kuwa;
Kwa kuwa mchakato wa kuandaa mtaala mmoja kwa vyuo vya uandishi wa habari umekamilika basi vyuo hivyo viaze kuutumia ili kuhakikisha elimu inayotolewa inazingatia matakwa na vigezo vya kitaaluma.
Kwamba mtaala huo ulioandaliwa kwa pamoja baina ya NACTE, MCT, wawakilishi wa vyuo vya habari na wadau wengine wa habari, utekelezaji wake unahitaji maandalizi ambayo ni pamoja na kuwa na walimu wenye sifa na uwezo wa kufundisha taaluma ya habari.
Kuanzia Januari 2013, TEF tutasubiri ipite miezi sita na baadaye tutafanya utafiti ili kubaini iwapo vyuo vyote vya Uandishi wa Habari vya Kati vitakuwa vimeanza kutumia mtaala huo kwa ajili ya kufudisha.
Kwa vyuo ambavyo havitakuwa vimekidhi matakwa ya kitaaluma, wahariri walikubaliana kutokuwapokea kwa ajili ya mafunzo ya vitendo (field attachment) wanafunzi wake wa uandishi wa habari.
Ufuatiliaji huo pia unavifikia vyuo vya uandishi wa habari ambavyo vimekuwa vikichanganya mafunzo hayo na kozi nyingine nyingi, ili kuwezesha kuchukua hatua stahili dhidi ya wanafunzi na wahitimu wa vyuo hivyo.
IMETOLEWA NA
JUKWAA LA WAHARIRI TANZANIA (TEF)
DAR ES SALAAM
DESEMBA 16, 2012

No comments :

Post a Comment