dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Monday, January 21, 2013

Tumfuate Maalim Seif au sera ya CUF?


“Inawezekana Maalim Seif ameungana na misimamo ya kundi la Uamsho linalotaka Muungano uvunjike kabisa… pengine anataka mkataba ili Muungano uwe rahisi kuvunjika…”

“Inawezekana Maalim Seif ameungana na misimamo ya kundi la Uamsho linalotaka Muungano uvunjike kabisa… pengine anataka mkataba ili Muungano uwe rahisi kuvunjika…”
MUUNGANO wa Tanganyika na Zanzibar umeendelea kuzua mijadala tangu ulipoanzishwa Aprili 26, mwaka 1964. Mijadala zaidi imeibuka hasa wakati huu wa mchakato wa mabadiliko ya Katiba, ambapo kumekuwa na mwamko mkubwa wa wananchi kuhoji uhalali wake, hasa visiwani Zanzibar.
Katika muungano huo, Tanganyika na Zanzibar zilikuabaliana kuunda nchi moja huru kwa mujibu wa Ibara ya Kwanza ya Hati za Muungano.
Bunge la Jamhuri ya Tanganyika lilitunga Sheria ya Muungano Namba 557, katika sura ya nne ya sheria hiyo lilitangaza kuundwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Kwa upande wa Zanzibar, Baraza la Mapinduzi lililokuwa Bunge la wakati huo halikutunga Sheria ya Muungano, jambo ambalo limekuwa chanzo cha mjadala mkali juu ya Muungano wenyewe. Katika Hati za Muungano za awali, kulikuwa na mambo 11 yaliyokubaliwa lakini yamekuja kuongezeka na kufikia 22, jambo ambalo pia limezua maswali mengi.
Pamoja na majaribu mengine yaliyoupata Muungano, mojawapo ni lile la mwaka 1992, baada ya kundi la wabunge 55 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano kutaka kuanzishwa kwa Serikali ya Tanganyika.
Licha ya kuwakemea na kulizima kundi hilo, Mwalimu Nyerere akiwa rais mstaafu wakati huo, aliwashukia na kumbebesha lawama aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, John Malecela kwa kushindwa kumshauri vyema Rais Ali Hassan Mwinyi.
Mwaka 1995 Mwalimu Nyerere aliona Muungano unazidi kutikisika na kuwapo hatari za kuvunjika na alitoa angalizo kwamba hakuna Mtanganyika wala Mzanzibari atakayepona kwa dhambi hiyo, huku akiweka wazi kuwa huo ulikuwa ni ufa mkubwa.
Lakini majaribu zaidi yameendelea na kuchochewa hivi karibuni baada ya mabadiliko ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ambayo yamekwenda kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano, hasa kwa kuitangaza kuifanya Zanzibar ambayo ni sehemu ya Muungano kuwa nchi kamili. Mabadiliko hayo yamekuja wakati yakiibuka makundi ya Wazanzibari yanayopinga Muungano hadharani, mojawapo likiwa la Uamsho.
Hata hivyo, Chama cha Mapunduzi (CCM) pamoja na kuendelea kusisitiza msimamo wake wa uwepo wa Serikali mbili yaani ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, wanachama wake mmoja mmoja wamekuwa wakipinga msimamo kwa lugha na mbinu tofauti.
CCM chenye msimamo wa Serikali mbili za sasa, vyama vingine vya siasa vina sera zake, vingi vikifanana kwa kukubaliana na Serikali tatu – Tanganyika, Zanzibar na Muungano. Mojawapo ya vyama vinavyounga mkono Muungano wa Serikali Tatu ni Chama cha Wananchi (CUF), ambacho hata hivyo, mtendaji wake mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad ameibuka kivingine akipigia debe Muungano wa aina tofauti.
Msimamo wa Maalim Seif
Wakati CUF kikijikita katika kupigania kurejeshwa kwa Serikali ya Tanganyika na kufanya ziwepo Serikali tatu, Katibu Mkuu wake, ambaye pia ni Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar, Seif Sharif Hamad ameibuka akisema kuwa anaamini katika Muungano wa Mkataba.
Msimamo huo aliutoa mara ya kwanza katika mkutano wake alioufanya katika Uwanja wa Kiabandamaiti, Unguja, na amekuwa akiurudia katika mikutano yake mbalimbali.
Kwa vyovyote msimamo huo unatofautiana na ule wa chama chake. Katika sera zake CUF kinasisitiza, “CUF inatambua umuhimu wa Muungano uliopo baina ya Tanganyika na Zanzibar, inataka pawepo Muungano wa ukweli unaozingatia maslahi ya wananchi wote. “… Sera ya CUF kuelekea muundo wa Muungano ni Serikali Tatu, yaani ile ya Zanzibar, ya Tanganyika na nyingine ndogo ya Muungano.”
Hata hivyo Maalim Seif anaweka bayana kuwa anaamini katika Muungano wa Mkataba.
“Mimi binafsi ni muumini wa Muungano wa Mkataba…Nasema hadharani na sisemi leo tu, mimi ni muumini wa Muungano wa Mkataba na inshaalah Mwenyezi Mungu atauleta huo,” anasema.
Katika kuwaaminisha wafuasi wake, maalim anasema, “Kama kuna mtu alikuwa na wasiwasi kwamba Maalim kapewa king’ora (uongozi serikalini)… Mimi king’ora nilishakipanda tangu mwaka 1984, si mara ya mwanzo hii…Kama ninyi hamjui ninyi vijana hamjui,” anasema
Muungano wa Mkataba ni upi?
Wakijadili kuhusu muundo huo wa muungano baadhi ya wanazuoni wanatilia shaka muundo huo wa Muungano.
Mwalimu wa Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Chris Peter Maina anasema aina hiyo ya Muungano haieleweki.
“Mimi sijui wanapozungumzia mkataba wanamaanisha nini, labda wao wenyewe watueleze. Unajua masuala ya mikataba yanaelezwa vizuri kwa lugha ya Kiingereza, kwa mfano kuna maneno kama ‘contract’, ‘conversion’ na ‘treaty’. Sasa labda watueleze wanataka mkataba wa aina gani hapo…” anasema Profesa Maina.
Naye mhadhiri wa siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Gaudence Mpangala pia anautilia shaka mfumo huo wa mkataba. “Mimi sielewi kuhusu huo Muungano wa Mkataba, nimekuwa mtazamaji wa chaguzi mbalimbali za Zanzibar kupitia Temco, siku zote nawasikia CUF wakitangaza sera ya Muungano wa Serikali tatu, sijawahi kusikia mkataba,” anasema Profesa Mpangala na kuongeza:
“Inawezekana Maalim Seif ameungana na misimamo ya kundi la Uamsho linalotaka Muungano uvunjike kabisa… pengine anataka mkataba ili Muungano uwe rahisi kuvunjika…”
Muungano wa Mkataba umekuwa ukitajwa katika maoni ya baadhi ya wananchi wa Zanzibar mbele ya Tume ya Kurekebisha Katiba na katika mijadala mbalimbali, na ufafanuzi wake ni kuwa na Serikali mbili za Zanzibar na Tanganyika kila ikiwa na mamlaka kamili, kasha zikawekeana mkataba wa ushirikiano katika masuala mbalimbali, kama ilivyo Jumuiya aya Afrika Mashariki au Umoja wa Ulaya.
Akielezea kuhusu mfumo huo wa Muungano, Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro anasema: “Mkataba unamaanisha kuwa nchi moja inataka ushirikiano na nchi nyingine katika masuala labda ya elimu, afya, fedha, majeshi na mengineyo. Lakini kila nchi inakuwa inajitegemea kama nchi huru.”
Kiongozi huyo pia anadokeza: “Kulikuwa na hati za Muungano, hizo ndiyo mkataba wenyewe. Sasa watu wanapouliza tena mkataba ni nini siwaelewi,” anasema Mtatiro.
Msimamo wa CUF
Kuhusu tofauti ya mawazo ya Maalim Seif na sera ya chama, Mtatiro anasisitiza msimamo wa chama hicho kuwa ni Serikali tatu – Tanganyika, Zanzibar na Muungano, lakini anaongeza kuwa kila kiongozi ndani ya chama hicho ana uhuru wa maoni.
“Ni kweli Maalim Seif ni kiongozi mkubwa wa chama, lakini yeye pia ni mwanachama, hivyo ana haki ya kutoa maoni yake kama wanachama wengine.
“Kwa hivi sasa Tume ya Katiba inaendelea kukusanya maoni ya Katiba, haitaishia tu kwa wananchi wa kawaida, itaenda hadi kwa Rais Jakaya Kikwete, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na viongozi wengine nao watatoa maoni yao,” anasema Mtatiro na kuongeza:
“Siyo lazima mawazo yetu wote yafanane, hata mimi ukiniuliza, sikubaliani na Muungano wa Mkataba bali napendekeza Muungano wa Serikali Tatu kama inavyoonyeshwa kwenye sera yetu ya chama.
“Lakini ukimuuliza hata Jussa (Ismail), yeye anapendekeza Muungano wa Mkataba.”
CHANZO: MWANANCHI na imeandikwa na Elias Msuya

1 comment :

  1. Inavyo onekana na Wazanzibari walio wengi,hilo koti la MUUNGANO kwa mazingira ya sasa,linawabana na linahitaji ama kufumuliwa na kurekibishwa au livuliwe ili wapumue,vinginevyo ni kuwapunguzia uvutaji pumzi na hatimae kilio.Waliosoma wa ngazi za juu wanaelewa nini Wazanzibari wanataka lakini wanatumia lugha zao kujaribu kuzunguka mbuyu.

    ReplyDelete