Kwa muda wa zaidi ya miezi mitatu kumekuwa na hali isiyoleta faraja katika visiwa hivyo baada ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (Zec), kufuta uchaguzi mkuu mwishoni mwa mwezi wa 10 kwa madai kwamba uligubikwa na kasoro nyingi.
Baada ya kutokea sintofahamu hiyo pamoja na kuwapo vikao vya vilivyohusisha viongozi wa CCM na Cuf vya kutafuta suluhu ya kisiasa visiwani humo bado hali ya kisiasa imezidi kuwa ya wasiwasi.
Baadhi ya wanasiasa wakongwe visiwani Zanzibar wamesimama na kusema bado hawaamini kama msimamo wa Cuf kujiweka kando na uchaguzi kama utadumu kabla ya machi 20 mwaka huu siku ambayo Zec imetangaza kurudiwa uchaguzi huo.Wanasiasa hawa wanasema chama makini cha siasa kinapoamua kujiweka nje ya ulingo na ushiriki wa kisiasa ni kwenda kinyume na madhumuni ya kuundwa kwake na azma ya kuingia kwenye medani za utawala.
Chama hicho kimeamua kujiengua katika uchaguzi huo kwa hoja kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec) Jecha Salim Jecha alifuta matokeo ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka 2015 bila kufuata sheria.
CUF bado kinaamini na kuitaka Zec kurudi kazini ili kukamiiisha uhakiki na kutangaza matokeo ili mshindi wa urais wa Zanzibar atagazwe kwa sababu uchaguzi huo umetajwa na waagalizi wa ndani na nje kama ulikuwa huru na wa haki.
Mwanasiasa Mkongwe nchini, Ali Ameir Mohammed (CCM) anasema CUF wanafanya ujanja wa kisiasa wa kutafuta kuwazubaisha wapinzani wao wakubwa Chama tawala CCM wasifanye maandalizi na matayarisho mazito kabla ya kufanyika uchaguzi huo.
Mwanasiasa huyo mkongwe katika siasa za Zanzibar anasema, chama chochote cha siasa duniani lengo lake kuu na madhumuni ni kukamata madaraka ya dola kupitia masanduku ya kura.
Mohammed ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, wakati wa rais Mstaafu Benjamin Mkapa , anasema chama cha siasa kinachosusia uchaguzi ni sawa na kukataa au kupingana na matakwa ya demokrasia wakati ndiyo msingi unaotoa haki.
“Siyo kweli kama CUF wamesusia uchaguzi ila wanafanya mbinu ya kuwazubaisha mahasimu wao CCM ili wajibweteke kisiasa bila kufanya matayarisho makubwa ya kufikia ushindi katika uchaguzi huo.”anasema Mohammed
Anaeleza kuwa uchaguzi huo unarudiwa kwa kupitia wagombea wale wale waliojitokeza katika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka uliopita na CCM watakuwa wajinga kama watalala kwa kuamini akilini mwao kama Cuf hawashiriki uchaguzi huo.
Kuhusu Mabalozi kutoridhishwa na hatua ya kurudiwa uchaguzi wa Zanzibar anasema, lazima wafahamu kuwa Zanzibar ni nchi huru ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na inayo katiba yake na sheria zake.
Anasema kitendo hicho cha Mabalozi kutoa msimamo ni sawa na kuingilia mambo ya ndani ya Zanzibar jambo ambalo siyo kazi yao iliyowaleta nchini.
Mohammed anasema wanadiplomasia wanatakiwa kudumisha ushirikiano kati nchi yake na ile lakini siyo siyo kujipa kazi ya usimamizi na ufuatilia wa mambo ya ndani ya nchi.
Mzee Mohammed anasema vurugu zinazotokea katika mataifa ya Syria, Libya, Iraq na Yemen yamechochewa kwa kiwango kikubwa na baadhi ya nchi za Magharibi.
“Waafrika tusikubali kuingiliwa mambo yetu ya ndani kama ambavyo wao mataifa makubwa wasivyokubali kuingiliwa mambo yao ya ndani, uchaguzi wa Zanzibar unarudiwa kwa mujibu wa katiba na sheria na wala siyo utashi ama ubabe wa mtu .”anasema
Anasema msimamo wa CUF umelenga kuamsha hali ya vurugu ili uchaguzi usifanyike kitendo ambacho kinaweza kurudisha nyuma taswira na maudhui ya kuundwa kwa serikaki ya umoja wa kitaifa.
Katibu mstaafu wa Jumuiya ya Wazazi ya CCM, Dadi Khamis Suleiman anasema Zanzibar inaelekea kubaya kutokana na uamuzi wa Cuf kususia uchaguzi wa marudio wa Zanzibar.
Dadi anasema amuzi waliochukua haukuzingatia misingi ya uzalendo na huenda Zanzibar ikapoteza utulivu na uendelezaji wa umoja wa wananchi wake.
Anasema maridhaino ya kisiasa yaliyofikwa mwaka 2009 na vyama vyote kukubaliana kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa SUK ambayo ilishirikisha vyama vya Cuf na CCM mwaka 2010.
Anasema ili chama cha siasa kiweze kuwa na sifa ya kuingziwa SUK ni lazima kiwe kimepata asilimia 10 ya kura katika uchaguzi.
Mwanasiasa huyo anasema haikuwa mwafaka kwa viongozi waliokuwa wakishiriki mazungumzo ya kutafuta suluhu ya kisiasa kuyageuza siri na kushindwa kuwataarifu wanachama wao wakati jambo hilo linahusu maslahi ya nchi na wananchi wake.
Mwanasiasa mwingine mkongwe Zanzibar na aliyekuwa Waziri wa kwanza wa Katiba na Sheria, Hassan Nassor Moyo anasema uamuzi wa Cuf kususia uchaguzi ni mzito na unahitaji muda kutafakari kabla ya kutoa maoni kutokana na uzito wake.
Anasema kwa mwanasiasa yoyote makini anahitaji kuangalia upepo wa kisiaasa unavyokwenda baada ya Cuf kutoa msimamo wa kutoshiriki uchaguzi wa marudio mwezi ujao.
“Zanzibar inapita katika wakati mgumu lakini ni mapema kutoa maoni kabla ya kusoma upepo wa kisiasa unavyovuma Zanzibar.’”anasema Moyo
Askari mstaafu wa Jeshi la Polisi wakati wa ukololoni (PMF) Suleiman Ali Sukari anasema uwamuzi wa Cuf kujitoa katika uchaguzi wa marudio ni sahihi kwa sababu Zec imeshindwa kuheshimu misingi ya demokrasia.
Anasema uchaguzi ulifanyika na kukamilika kwa asilimia 100 na wagombea wote kukabidhiwa vyeti vya matokeo hapakuwa na sababu za kufutwa matokeo ya uchaguzi huo.
Msimamo wa Cuf anasema utakuwa na madhara makubwa katika masuala ya demokrasia visiwani Zanzibar.
“Kama uchaguzi kurudiwa ulitakiwa kurudiwa katika majimbo ambayo kumetokea kasoro na siyo kufuta uchaguzi wote na kutangaza na kurudia tena,”anasema.
Anasema Zec imepoteza imani kwa jamii na sifa kwa wananchi kwa kuwa imeonyesha haitaki CCM iondoke madarakani.
Sukari anasema Cuf wangekubali kushiriki uchaguzi huo dunia ingewashangaa kwa kuwa waangalizi wa uchaguzi wa ndani na nje walieleza kuwa ulikuwa huru na haki.
Anashauri kwamba njia pekee ya kumaliza mgogoro wa Zanzibar ni mwenyekiti wa Zec na wajumbe wake kujiuzuru nafasi zao ili kuunda tume nyingine.
Anasema Wananchi wa Zanzibar hawana imani na Zec kutokana na mwenyekiti wake kufuta matokeo ya uchaguzi baada ya kuona CCM hakiwezi kushinda.
Mzee Rashid Mohamed Said (CUF), anasema Zanzibar hakuna sababu ya kuwa na mfumo wa vyama vingi na kwamba wakati umefika wa kurudi katika chama kimoja.
Anasema CCM hawataki kuondoka madarakani pamoja na wananchi kuonyesha kuikataa tangu uchaguzi wa kwamza wa vyama vingi mwaka 1995.
Anasema Cuf wanastahili kupongezwa kutokana kwa uamuzi wao kwani utasahidia kuepusha kutokea vurugu na kusababisha kutoweka kwa amani.
“Haiwezekani kurudia mechi na mwamuzi aliyevuruga mechi na wasaidizi wake wale wale akiwemo kamisaa wa mchezo yule yule .”anasema .
Mpasuko uliokuwapo kabala ya kuundwa kwa SUK umerudi kama zamani na nchi haiwezi tena kupiga hatua moja mbele ya maendeleo kama wananchi wake wakiwa wamegawanyika kisiasa.
Anasema busara na hekima ya Maalim Seif Sharif Hamad ndiyo iliyosaidia kuwepo kwa amani Zanzibar mpaka leo baada ya kufutwa kwa matokeo ya Uchaguzi Mkuu Oktoba 28 mwaka jana
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment