Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Daktari Mkuu wa Hospitali ya Nanjing Dkt. Zhou Yujie akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Mnazi mmoja vitabu vitakavyotumika kuendesha mafunzo ya madaktari na wauguzi wa Zanzibar.
Dkt. Zhou Yujie ambae ni Mkurugenzi na Daktari Mkuu wa Hospitali ya Nanjing akizungumza na madaktari na wauguzi watakaoshiriki mafunzo ya miaka mitatu nchini China na Zanzibar wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo uliofanyika Hospitali ya Mnazi mmoja.
Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Mnazi mmoja Dkt. Ali Salum Ali akizindua mafunzo ya madaktari na wauguzi yatakayofanyika katika Hospitali ya Nanjing na Hospitali kuu ya Mnazi mmoja Mjini Zanzibar, (kushoto) ni Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Daktari Mkuu wa Hospitali kuu ya Jimbo la Nanjing
Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Mnazi mmoja Dkt. Ali Salum Ali,akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Daktari Mkuu wa Hospitali ya Nanjing Dkt. Zhou Yujie, baada hafla ya kukabidhi vitabu kwa ajili ya mafunzo kwa madaktari wa hospitali ya mnazi mmoja.
Jimbo la Nanjing Nchini China limeongeza ushirikiano mpya na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuanzisha mpango maalumu wa mafunzo ya miaka mitatu kwa madaktari na wauguzi wa Hospitali kuu ya Mnazi mmoja.
Mafunzo hayo yatakayofanyika kwa zamu katika Hospitali ya Mnazi mmoja na Hospitali ya Nanjing yatawashirikisha madaktari sita na wauguzi sita kutoka sehemu ya wazazi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Mnazi mmoja Dkt. Ali Salum Ali ameyazindua rasmi mafunzo hayo na kueleza kuwa wamejiandaa vizuri ili kuhakikisha mafunzo hayo yanafanyika kwa ufanisi.
Amesema mafunzo hayo yanatarajiwa kuwaongezea uwezo madaktari wazalendo na wauguzi katika kukabiliana na vifo vya mama wajawazito wakati wa kujifungua na watoto wachanga.
Dkt. Ali Salum amesema katika mpango huo, madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Nanjing watakaoendesha mafunzo hayo wataambatana na wanafunzi wao kwa awamu katika hospitali ya Jimbo hilo na Hospitali ya Mnazi mmoja.
Ameongeza lengo la kuendesha mafunzo hayo katika vituo viwili tofauti, China na Zanzibar, ni kuwapa fursa madaktari na wauguzi kujifunza kwa kutumia mazingira ya nyumbani na mazingira ya kigeni ambapo yatakuwa na ufanisi zaidi.
“Mara nyingi vijana wetu wanapokwenda nje ya nchi kwa mafunzo hutumia teknolojia ya huko na wanaporudi wanatumia teknolojia ya kwetu hivyo baadhi ya wakati wanajikuta wapo njia panda,” aliongeza Mkurugenzi Mtendaji.
Amesisitiza kwamba mpango huo mpya wa mafunzo utatoa fursa kwa madaktari na wauguzi wengi kutoka Zanzibar kupata mafunzo kwa wakati mmoja na utapunguza gharama za kuwasafirisha watu wachache kwa gharama kubwa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Mnazi mmoja alisema baada ya madaktari na wauguzi hao kumaliza mafunzo yao watasaidia kutoa huduma katika Hospitali na vituo vyengine vya afya vya Zanzibar.
Mkurugenzi wa Idara ya Elimu ambae pia ni daktari mkuu wa Hospitali ya Nanjing Dkt. Zhou Yujie amesema tayari wameandaa mtaala na kufanya uteuzi wa madaktari 20 watakaosimamia mafunzo hayo.
Katika uzinduzi wa mafunzo hayo uliofanyika Hospitali ya Mnazi mmoja, Dkt. Zhou alimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji vitabu vitakavyotumika katika kuendesha mafunzo hayo.
Alisema katika mafunzo hayo wakufunzi kutoka Hospitali ya Nanjing watashirikiana na wanafunzi wao kuwafanyia matibabu ya kawaida na upasua wagonjwa ikiwa ni miongoni mwa mafunzo yao.
Amekumbusha kuwa uhusiano wa sekta ya afya kati ya Jimbo la Nanjing na Zanzibar ulianza tokea mwaka 1964 kwa kuleta madaktari katika Hospitali ya Mnazi mmoja na Hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani na mpango wa sasa wa mafunzo ya miaka mitatu ni muendelezo wa historia hiyo.
No comments :
Post a Comment