- By Joseph Lyimo, Mwananchi
Babati. Wazee wanaolelewa katika Kituo cha Sarame kilichopo Kata ya Magugu wilayani Babati Mkoa wa Manyara, wamelalamikia kutapakaa kwa kunguni kwenye nyumba wanazoishi.
Wakizungumza na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Manyara, Anna Gideria aliyewatembelea na kuwapa msaada wa vyakula na dawa za thamani ya Sh1.5 milioni juzi, wazee hao walisema kunguni wamekuwa kero kituoni hapo.
Ofisa Maendeleo ya Jamii anayewalea wazee hao, Samson Munuo alisema: “Wadudu wengine ambao wamekuwa kero kubwa hapa kituoni ni mende na mbu, tunaomba tusaidiwe dawa za kuua wadudu.”
Hata hivyo, aliishukuru Serikali kwa kujenga uzio wa kituo hicho. Akisema awali walikuwa wanasumbuliwa na tembo, simba na nyoka wakubwa waliokuwa wanatoka kwenye Hifadhi ya Taifa ya Tarangire.
Mbunge huyo ameahidi kuzifanyia kazi changamoto zote zinazowakabili ikiwamo ya ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa. “Nitakaa na wadau wengine ikiwamo Serikali kutafuta njia ya kutatua matatizo haya,” alisema.
Kituo cha Sareme kilianzishwa 1975 kikiwa na wazee watano na sasa kina wazee 13 wanaohudumiwa na Serikali.
No comments :
Post a Comment