dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Sunday, January 6, 2013

Gesi Mtwara: Kikwete apingwa


Na Waandishi Wetu  (email the author

SAKATA la wananchi na baadhi ya wanasiasa kupinga usafirishwaji wa gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam, limechukua sura mpya, baada ya vyama vya siasa nchini kuungana na kutumia jukwaa kumpinga Rais Jakaya Kikwete, vikisisitiza kuwa gesi haitaondoka Mtwara.
Vyama hivyo pia, vimemtaka Rais Kikwete kumwondoa katika wadhifa wake, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kwa madai kuwa ametoa kauli ya kuwakejeli wananchi wa mkoa huo.
Vyama hivyo vinapinga gesi asilia itayotarajiwa kuanza kuvunwa katika Mkoa wa Mtwara, kusafirishwa kwa bomba kwenda jijini Dar es Salaam kwa madai kuwa haitawanufaisha.
Hata hivyo, Rais Kikwete katika hotuba yake ya Mwaka Mpya, alisema  siyo sahihi kwa wakazi wa Mtwara kuizuia gesi isisafirishwe kwenda Dar es Salaam kwa sababu rasilimali hiyo ni ya Watanzania wote.
Wakihutubia kwa nyakati tofauti mkutano wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Soko Kuu, mjini Mtwara jana jioni, viongozi wa vyama hivyo walisema kwamba hawako tayari kuona rasilimali za nchi zikiendelea kusababisha umaskini kwa wananchi, badala ya kuwakomboa.
“Ukicheka na nyani utavuna mabua, wenzetu kwenye madini walicheka nao na wamevuna mabua, sisi hatuko tayari…; Tunatambua kuwa mamlaka ya nchi yapo mikononi mwetu kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kama Kikwete amesema kwa namna yeyote ile gesi itatoka, basi sisi tunamwambia, kwa namna yeyote ile gesi hatoki,” alisema Mohamedi Salim mjumbe wa umoja huo kutoka NCCR- Mageuzi.
Aliongeza: “Kwanza, tunataka Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo aondolewe katika wadhifa huo kwa sababu analeta propaganda za kisiasa kwenye masuala nyeti yanayohusu maisha ya watu.”  
Kwa pande wake, Mwenyekiti wa Chadema wa Wilaya ya Mtwara Mjini, Mustafa Nchia alisema kuwa wataandamana hadi Serikali itakaposikia kilio chao na kwamba kwa kuanzia wanataka Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Joseph Simbakalia, aondolewe mkoani humo akidai aliwatusi wananchi kwa kuwaita wapuuzi.
Katika mkutano huo, makamu mwenyekiti wa umoja huo, Uledi Abdallah alimpongeza Kamanda wa Polisi mkoani humo, Maria Nzuki, kwa kuruhusu maandamano hayo na kuwataka wananchi kuondoa woga katika kusimamia rasilimali zao, mradi wasivunje sheria.
Mikutano hiyo itaendelea kesho katika Viwanja vya Bima na keshokutwa katika Viwanja vya Nkanaledi.
Awali, Makamu Mwenyekiti wa umoja huo unaojumuisha vyama vya siasa, Uledi Abdallah aliliambia gazeti hili kuwa, kwa siku tatu mfululizo wanatarajia kuendesha mikutano mikubwa ya hadhara katika Viwanja vya Soko Kuu, Bima na Mkanaledi.
Uledi ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, Wilaya ya Mtwara Mjini alisema: “Januari 13, tutawapokea viongozi wa NCCR-Mageuzi Taifa, James Mbatia, wabunge wote wanne wa chama hiki.”
Kamati ya Siasa ya CCM mkoa kukutana
Wakati mkutano huo wa vyama vya siasa ukifanyika, Kamati Siasa ya CCM Mkoa wa Mtwara, inatarajiwa kukutana kesho ili kujadili mgogoro wa gesi na kutoa msimamo wao.
Kamati hiyo itakutana huku tayari kukiwa na mgongano baina yao, kutokana na chama hicho Wilaya ya Mtwara Mjini, sambamba na mbunge wa Mtwara Mjini, Hasnain Murji kuunga mkono wananchi wa mkoa huo kupinga kusafirishwa kwa gesi hiyo inayovunwa katika Kijiji cha Msimbati mkoani humo.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mtwara, Mohamedi Sinani amethibitisha kufanyika kwa kikao hicho kesho Jumatatu.
Akizungumza na Mwananchi Jumapili alisema: “Tutakutana Jumatatu kwenye kikao cha Kamati ya Siasa Mkoa, baada ya hapo nitawaambia nini msimamo wa chama mkoa kuhusu gesi.”
Wadadisi wa mambo wanasema kuwa kikao hicho pia kitajadili na kutoa tamko juu ya msimamo wa mbunge Murji na ule wa chama hicho Wilaya ya Mtwara Mjini kupinga mradi huo.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mtwara Mjini, Ali Chinkawene, hivi karibuni alisema kuwa msimamo wa chama chake ni kuungana na wananchi, kupinga gesi kusafirishwa kwenda Dar es Salaam na kwamba Serikali inapaswa kujenga mitambo ya kuzalisha umeme mkoani Mtwara, badala ya Dar es Salaam.
Mwenyekiti huyo alibainisha kuwa msimamo huo siyo wake binafsi, bali ni maazimio ya vikao halali vya chama hicho vinavyowakilisha wanachama na kwamba, historia ya mikoa ya kusini jinsi ilivyonyimwa maendeleo ilitumika na wajumbe kujenga hoja yao hiyo.
Kwa uamuzi huo, CCM Mtwara Mjini, inaungana na vyama tisa vya awali vilivyokuwa vinapinga gesi kupelekwa Dar es Salaam,  ambavyo ni Chama cha Wananchi (CUF), Chadema, NCCR-Mageuzi, SAU, TLP, APPT Maendeleo, ADC, VDP na DP, vikiwa na kaulimbiu ya “Gesi kwanza vyama baadaye, hapa hakitoki kitu.”
Umoja wa vyama hivyo tisa, ndiyo uliratibu maandamano ya Desemba, 27 mwaka uliopita kupinga mradi huo wa gesi.
Mbunge wa Mtwara Mjini, Hasnain Murji, ameweka wazi msimamo wake wa kupinga gesi kupelekwa Dar es Salaam na kuongeza kuwa yupo tayari kuvuliwa ubunge, kama ikibidi kufanya hivyo katika kutetea masilahi ya wananchi.
Tofauti na Murji, Mbunge wa Mtwara Vijijini, Hawa Ghasia ambaye ni Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Mbunge wa Newala, George Mkuchika Waziri wa Ofisi ya Rais, Utawala Bora wao wanaonyesha kuunga mkono mradi huo.
Kwa nyakati tofauti mawaziri hao wamekaririwa wakiwatia moyo wananchi kuwa mradi huo unalenga kuwanufaisha wao na Taifa kwa jumla, licha ya kukabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa wananchi.
Novemba, 20 mwaka jana wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Abdulrahman Kinana, Ghasia alizomewa na wananchi pale alipojaribu kutetea mradi huo.
Licha ya Ghasia na Mkuchika kuwa siyo wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa, wabashiri wanasema kuwa kuna uwezekano wa kikao hicho kuwa kigumu kutokana na baadhi ya wajumbe wake kuonyesha wazi kutounga mkono hoja ya gesi kupelekwa Dar es Salaam.
“Keshokutwa (kesho) kutakuwa na kazi ngumu. Wapo wajumbe waliopania kutetea masilahi ya wananchi…wanaona chama kitakufa iwapo wataunga mkono gesi kuondoka, watu wanajipanga kwa hoja siyo ushabiki,” kilisema chanzo chetu ambacho ni kada wa CCM.
CUF kuandamana Dar
Jumuiya ya Vijana wa CUF imesema kuwa itafanya maandamano makubwa jijini Dar es Salaam, kuunga mkono wananchi wa Mtwara.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Katani Katani alisema kuwa maandamano hayo yatafanyika siku yoyote kuanzia leo kwa lengo la kuonyesha kwamba hata vijana wa CUF na chama chao kwa jumla kinapingana na mpango wa Serikali kuhusu mradi huo.
Mbunge apinga
Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu amesema kuwa haungi mkono maandamano kupinga ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi kwenda jijini Dar es Salaam.
Alitoa kauli hiyo jana kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari, ambapo pamoja na mambo mengine, alisema kuna haja kwa Serikali na wananchi kukaa pamoja na kujadiliana jambo hilo kwa kina, badala ya kulipinga kwa kutumia maandamano.

Abdallah Bakari, Mtwara na Aidan Mhando, Fidelis Butahe, Dar.
Chanzo: Mwananchi



No comments :

Post a Comment