Kwarara Msikitini

Dual Citizenship #2

Dual Citizenship #2

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

Mwanakwerekwe shops ad

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Tuesday, July 1, 2014

Mafuta Bahari ya Hindi, Ziwa Nyasa mtego mpya mipakani - REVISITED!!!

Toleo la 337 Raia Mwema
5 Feb 2014
WAKATI Tanzania na Malawi zinaweza kuwa zinaendelea na mzozo wa mpaka wa Ziwa Nyasa (Ziwa Malawi) Idara ya Mazingira ya Wizara ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi ya Malawi imetangaza kuanza kusikiliza maoni ya umma juu ripoti ya Athari za Jamii na Mazingira (ESIA) ya kampuni ya mafuta ya Surestream Petroleum, inayotaka kutafiti mafuta ndani ya ziwa hilo.
Taarifa iliyosambazwa mwishoni mwa mwezi uliopita (Januari 2014) nchini Malawi kupitia mitandao mbalimbali inawahimiza raia wake kupeleka maoni yao kuhusiana na athari zinazoweza kutokea katika utafiti huo na hatimaye uchimbaji mafuta.
Kampuni ya Surestream Petroleum ya Uingereza imepewa kibali cha utafiti wa mafuta katika maeneo mawili yenye ukubwa wa kilometa za mraba 20,000 ndani ya ziwa hilo tangu mwaka 2011.
Ziwa hilo lina ukubwa wa kilometa za mraba 29,000.
“ Kama ilivyotangazwa, umma unaalikwa kupitia ripoti ya ESIA kama inavyoagizwa na Sheria ya Usimamizi wa Mazingira (1996) na kutoa maoni kwa Idara ya Mazingira ifikapo Februari 12, 2014, kabla ya uamuzi wa serikali wa ama kuzuia au kukubaliana na shughuli za utafiti za Surestream,” inasema taarifa hiyo inayoambatana na mkanda wa video wa Surestream, unaoitwa: Malawi A New Dawn (Kumekucha Malawi) http://www.surestream-petroleum.com/video-3.htm
unaozungumzia jinsi Malawi itakavyonufaika na mafuta.
Mzozo unaorejewa katika utangulizi  unahusu mvutano wa mpaka kati ya Tanzania na Malawi, nchi mbili jirani zinazochangia Ziwa Nyasa (kwa Tanzania) na Ziwa Malawi (kwa Malawi) na ambazo huko nyuma zilipata kuvutana kuhusu ulipo mpaka. Malawi imekuwa ikidai kuwa inamiliki maji yote ya ziwa hilo huku Tanzania ikisema mpaka uko katikati ya ziwa.
Kila nchi ina sababu zake. Malawi inasema inafuata makubaliano ya Mkataba wa Heligoland wa Julai 1, 1890, kati ya Ujerumani na Uingereza unaoonyesha kwamba Malawi inamiliki maji yote ya ziwa mpaka kwenye ufukwe wa upande wa Tanzania.
Kwa upande wake, Tanzania inasema inafuata makubaliano ya baada ya Vita ya Kwanza ya Dunia kuelekea mwaka 1920 baada ya kuwa Ujerumani imeshindwa katika vita hiyo, iliingia makubaliano na Uingereza, mpaka ukawekwa katikati kwa maana ya kila nchi ambazo wakati huo (Tanganyika na Nyasaland) zilikuwa zinatawaliwa na bwana mmoja, Uingereza, kila moja imiliki asilimia 50 ya maji ya ziwa.
Nyaraka kadhaa zinaonyesha kwamba huo ni mzozo wa muda mrefu kati ya Tanzania na Malawi uliodumu kwa zaidi ya miaka 50 na japo sasa umefikishwa mbele ya usuluhishi wa rais wa zamani wa Msumbiji, Joaqium Chissano, na wakubwa wenzake, taarifa kwamba Surestream inaweza kuendelea na utafiti wa mafuta ndani ya ziwa zinaupasha moto zaidi sasa, pamoja na mambo mengine, taarifa za utajiri wa mafuta zikizingatiwa.
Katika hatua nyingine, akihutubia katika kilele cha sherehe za maadhimisho ya miaka 37 ya kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete alisema Watanzania wanaoishi kando ya Ziwa Nyasa wasiwe na hofu kwani suala hilo la mzozo wa mpaka linashughulikiwa na wazee wenye busara.
“Kama kuna mwanasiasa analizungumzia suala hili anatafuta umaarufu tu. Lipo katika hatua nzuri na Kamati ya Chissano itatueleza ukweli,” alisema Kikwete Jumapili, Februari 2, 2014, kwenye sherehe hizo mjini Mbeya alikohutubia kama Mwenyekiti wa CCM.
Ukiacha hayo ya Tanzania na Malawi, umekuwapo mvutano wa waziwazi kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ)  kuhusiana na umiliki wa mafuta yanayoelezwa kuwa huenda yakapatikana Zanzibar, hasa maeneo ya Pemba.
Baadhi ya wanasiasa wa Zanzibar, akiwamo Ismail Jussa Ladhu, kwa nyakati mbalimbali, wamekuwa wakieleza kwamba pindi yakipatikana mafuta, basi utajiri huo utakuwa ni wa watu wa Zanzibar.
Katika mwendelezo wa fikra hizo, Juni 28, 2012, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliliambia Bunge kwamba Serikali ya Muungano haikuwa na pingamizi kwa Zanzibar kuanzisha utafiti na uchimbaji mafuta Visiwani.
Akizungumza katika kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu bungeni, Dodoma, Waziri Mkuu Pinda alisema Serikali ilikuwa inaangalia taratibu za kuiwezesha Zanzibar kuendelea na utafiti wa mafuta huku ikipitia vipengele vya sheria na Katiba kuamua kama suala la mafuta liendelee kubaki kuwa la Muungano au la.
Alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Konde (Pemba), Khatibu Said Haji (CUF), aliyetaka kujua msimamo wa Serikali ya Muungano juu ya taarifa ya Waziri wa Nchi wa SMZ, Mohamed Aboud, kwamba utafiti na uchimbaji mafuta Zanzibar utafanywa na SMZ.
Kwa mujibu wa mbunge Khatibu Said Haji, katika swali lake kwa Waziri Mkuu Pinda, suala la mafuta ya Zanzibar lilikuwa kati ya changamoto nyingi zilizokuwa zikiusukasuka Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kwamba msimamo wa Zanzibar, ambao alisema tayari ulikwisha kuelezwa kwa uwazi, ulikuwa ni mafuta hayo yachimbwe na Zanzibar.
“ Binafsi sioni tatizo hapa… iwapo Zanzibar itagundua mafuta, sisi hatutapoteza chochote, badala yake tutakuwa tukipata mafuta jirani,  bei itakuwa nafuu,” alijibu Waziri Mkuu Pinda na kuongeza kwamba tatizo lilikuwa ni kwenye sheria na Katiba na kwamba jitihada zinafanyika utafiti uendelee huku taratibu za kisheria na Katiba zikiendelea kwa vile “utafiti na uchimbaji mafuta huchukua mpaka miaka minane”.
Mwishoni mwa mwaka jana, SMZ iliingia makubaliano ya awali (MoU) na kampuni ya Uingereza ya mafuta na gesi asilia, Shell, wakati wa ziara ya Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein. Taarifa zinasema Mtendaji Mkuu wa Shell, Peter Voser, alisaini mkataba huo kwa niaba ya kampuni yake huku Waziri wa Nishati,  Ramadhan Abdallah Shaaban, akisaini kwa niaba ya SMZ.
Taarifa zinasema chini ya mkataba huo SMZ imeipatia Shell idhini ya kutafiti na hatimaye kuchimba mafuta katika vitalu vinne Zanzibar: vitalu namba 9,10,11 na 12.
Nyaraka zinasema kwamba katika kauli mbalimbali, magwiji wa sheria na Katiba nchini, Profesa Issa Shivji na Dk. Rugemeleza Nshala, waliuita mkataba huo kati ya SMZ na Shell kuwa ni batili na uliokwenda kinyume cha Katiba ya Tanzania.
Akizungumza mwishoni mwa mwaka jana kutokea Kilwa Masoko katika mafunzo ya wanahabari ya mafuta na gesi, yaliyoandaliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT), Profesa Shivji, alisema mafuta na gesi ni mambo ya Muungano, na kwa hiyo ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano pekee yenye uhalali wa kisheria kusaini mkataba wowote unaohusiana na jambo hilo.
“Masuala ya mafuta na gesi yaliongezwa kwenye mambo ya Muungano na Mzee Karume (Abeid Amani Karume, rais wa kwanza wa SMZ) mwenyewe mwaka 1968. Zitafuteni Hansard (taarifa za mazungumzo bungeni) zipo. Hao wanaopiga propaganda kwamba mambo hayo yaliingizwa kinyemela kwenye mambo ya Muungano ni watu wa kupuuzwa,” alisema Profesa Shivji.
Dk. Nshala alisema kwa kusaini makubaliano hayo, SMZ na Shell walikuwa wamevunja Katiba kwa vile si wahusika sahihi.
“Mwenye mamlaka ya kisheria kusaini mkataba wowote unaohusu nishati na madini, kwa mujibu wa Katiba, kwa niaba ya Serikali (ya Muungano)  ni Waziri wa Nishati na Madini. Suala la mafuta na gesi asilia viko chini ya Muungano.…unajua kuna watu wanataka kutumia kipindi hiki ambacho tuko kwenye mchakato wa kuandika Katiba mpya kuvuruga Muungano,” alisema Dk. Nshala ambaye ni mbobezi katika mikataba ya madini, mafuta na gesi.
Mkanganyiko wanaouzungumzia Profesa Shivji na Dk. Nshala ulipata kutajwa katika muongo uliopita kwenye utafiti uliofanywa mwaka 2009 na Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF) kwa niaba ya The Norwegian People’s Aid chini ya mada: Petroleum Exploration Study.
Inasema sehemu ya utafiti huo kuonyesha changamoto mbalimbali zinazoigonganisha Serikali ya Muungano na SMZ kuhusu milki ya maliasili kama mafuta kwenye masuala ya sera: ” utafiti umeonyesha kwamba si Tanzania (Serikali ya Muungano) wala Zanzibar yenye sera timilifu ya kitaifa ya utafiti na maendeleo ya mafuta.
Serikali ya Muungano ina Sera ya Taifa ya Nishati (1992 na 2003) na sera nyingine zinazowezesha ukuzaji wa sekta ya mafuta Tanzania. Serikali ya Zanzibar haina sera timilifu ya nishati. Ndiyo kwanza iko katika mchakato wa kukamilisha sera yake yenyewe ya nishati ”.
Utafiti huo unataja changamoto nyingine kuwa ni pamoja na Katiba. “Serikali ya Muungano ina sheria mbalimbali zinazoathiri maendeleo ya shughuli za mafuta, kwa kuanzia na  (1) Katiba ya Jamhuri ya Muungano, (2) Sheria ya Petroli ya mwaka 1980; Sheria ya EWURA  ya  2001,   na (3), Sheria ya uhifadhi wa Petroli ya 1987, ambayo sasa imerekebishwa na Sheria ya 2008.
“Kuna changamoto nyingi bado. Ibara ya 4 (3) ya Katiba inasema maliasili kama madini, mafuta na gesi zipo chini ya usimamizi wa Jamhuri ya Muungano. Kwa ajili ya uendeshaji mzuri wa mambo ya Jamhuri ya Muungano na kwa kutoa mamlaka kwa vyombo vinavyotajwa katika Ibara hii. Aya ya 15 ya jedwali la kwanza la Katiba chini ya Ibara ya 4 inasema kwamba madini, mafuta na gesi ni masuala ya Muungano. Na hapo ndipo penye mkanganyiko na panapozua mjadala wa je, mafuta ni suala la Muungano au la.”
Kama itapitishwa ilivyo kuwa Katiba, Rasimu ya Katiba mpya inaweza kutoa suluhisho la mvutano uliopo kati ya Serikali ya Jamhuri na SMZ kuhusu suala la umiliki wa mafuta.
Rasimu inapendekeza katika Ibara ya 63 kwamba: “ Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano, na kwa ajili ya mgawanyo wa madaraka juu ya shughuli hizo baina ya vyombo vilivyotajwa katika Ibara ya 61, Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na mamlaka juu ya mambo ya Muungano kama yalivyoorodheshwa katika Nyongeza ya Katiba hii”.
Ibara ya 61 (1) kwa upande wake inasema: “ Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa ndiyo chombo chenye mamlaka ya utendaji, Bunge litakuwa na mamlaka ya kutunga sheria kwa mambo ya Muungano na kusimamia utekelezaji wa shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Mahakama itakuwa ni chombo cha utoaji haki; (2) Kila chombo kilichotajwa katika ibara hii kitaundwa na kutekeleza majukumu yake kwa kufuata masharti ya Katiba hii ”.
Aidha, Rasimu ya Katiba mpya katika Nyongeza: Mambo ya Muungano inataja mambo saba tu kuwa ndiyo yasimamiwe na Serikali ya Muungano. Hayo ni Katiba na  Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania; Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania; Uraia na Uhamiaji; Sarafu na Benki Kuu; Mambo ya Nje; Usajili wa Vyama vya Siasa; na, Ushuru wa Bidhaa za mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na Mambo ya Muungano.
Mivutano ya maeneo ya mipakani  inayotokana na nchi kutaka kumiliki rasilimali kama madini, mafuta na gesi si mipya katika Afrika ingawaje sasa inaonekana sana ndani ya Afrika Mashariki na eneo zima la Maziwa Makuu.
Kwa nini Afrika Mashariki? Sababu ni kwamba eneo hilo lipo karibu na China na India kulinganisha na maeneo mengine.
Nyaraka kadhaa zinasema kwamba huko nyuma eneo hilo halikufahamika kwa wengi kuwa lingekuwa na utajri mkubwa wa gesi na mafuta. Ndiyo kwanza wengi wamefahamu.
Kwa mujibu wa nyaraka hizo za kwenye mitandao kama wa www.nextoilrush.com, sifa au kivutio kikubwa kitakuwa ni nafasi ya kijiografia ya eneo hilo kuwa karibu na bara la Asia, na hasa, kuwa karibu na China na India, nchi mbili ambazo sasa ziko mbele katika maendeleo ya kiuchumi na uwekezaji. Ukaribu huo unalifanya eneo la Afrika Mashariki kuwa kivutio zaidi kwa China na India katika gesi na mafuta.
“Mahitaji ya mafuta ya China na India bado yako chini kulinganisha na nchi zilizoendelea za Magharibi. Lakini idadi ya watu wa China inakaribia bilioni 1.34. India inaifuatia China kwa karibu ikiwa na watu wapatao bilioni 1.21.
“Ulaya ina idadi ya watu wapatao milioni 500, Marekani inao kiasi cha milioni 300. Unaweza kuona ni kiasi gani cha mafuta kitaweza kutosheleza idadi ya karibu Wachina na Wahindi wapatao bilioni 2.5 ambao karibuni wataanza kutumia mapipa zaidi ya mafuta kwa kila mtu katika matumizi ya kuongeza joto majumbani, umeme, magari, usafiri na huduma nyingine,” zinasema nyaraka hizo.
Zinaongeza nyaraka hizo: “ Yatakapokuwa mahitaji hayo yanaanza kukua, kampuni kubwa za mafuta zitahitaji kuwa na hazina ya mafuta na gesi katika vituo vya karibu na masoko makubwa, yaani China na India, na vituo hivyo ni Afrika Mashariki.
“Kukodisha meli za kusafirishia gesi na mafuta ni gharama kubwa na gharama hizo hulipwa kila siku. Gharama hizo kutoka kwenye chanzo hadi sokoni hurundikiwa mnunuzi kwa hiyo ina maslahi kama mnunuzi atapata shehema karibu na kwake. Hii ndiyo sababu iliyosukuma kujengwa kwa Mfereji wa Panama.”
Nyaraka hizo zinasema ni ukaribu wa aina hiyo kwa masoko ya China na India uliozivuta kampuni kubwa duniani kama Chevron, Exxon Mobil na ConocoPhilips, Total na Shell kuwekeza karibu dola za Marekani bilioni 200 katika miradi ya gesi Australia. Wakati tayari Australia imeanza mchakato wa uzalishaji, itachukua miaka hata 10 kwa Afrika Mashariki kuweza kuanza kuzalisha mafuta.

- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/mafuta-bahari-ya-hindi-ziwa-nyasa-mtego-mpya-mipakani#sthash.fV5e7aBS.dpuf


No comments :

Post a Comment