dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Saturday, August 30, 2014

Uraia Pacha: Rai yangu juu ya mchango wa wana Diaspora kwenye maendeleo ya Tanzania

Mada ya uraia pacha imechukua sura mpya ndani na nje ya Tanzania hasa katika kipindi hiki ambapo wadau mbalimbali wameshirikishwa kuchangia katika uandikwaji wa katiba mpya ambayo itaunda sheria mpya au kurekebisha zile za zamani zitakazowaathiri watanzania wote popote waishipo duniani.  Kuna masuala mengi ambayo yanahitaji utafiti, uelimishwaji wa umma na wabunge wa baraza la katiba kuhakikisha kuwa sheria zinazopitishwa zitalinda maslahi ya nchi pamoja na haki za msingi za kila mwananchi mzawa na kuboresha sheria zinazozungumzia raia wapya ambao si wazawa ya Tanzania. Katika vifungu vifuatavyo, nitajaribu kutoa maelezo kuhusu baadhi ya hoja ambazo zimepelekea suala zima la ujumuishwaji wa uraia pacha kuvuta hisia tofauti.

Watakaopewa uraia pacha wataigeuza Tanzania shamba la bibi
Hii ni moja kati ya hoja nyingi ambazo kundi la watanzania wanaopinga uraia pacha wamekuwa wakiitumia kueleza jinsi gani urai pacha utakavyoathiri uchumi na maliasili za nchi. Hoja hii inaukweli ndani yake iwapo tu nchi haitakuwa na sera na sheria za kulinda uchumi kwa maslahi ya taifa. Si hivyo tu, hata kama nchi itakuwa na sheria lakini kama hazitasimamiwa kwa ufanisi wa makusudi,  kutoka kwa wale waliopewa majukumu ya kuzisimamia, bila shaka nchi yetu itakuwa shamba la bibi.
Pamoja na hoja hii kuwa na nguvu, siamini kama hii ni sababu tosha ya kutopitisha sheria ya uraia pacha kwa mamilioni ya watanzania ambao walichukua uamuzi wa kwenda kutafuta elimu, kazi na maisha bora ambayo yalikuwa ni vigumu kuyapata katika mazingira wajiyoondokea.  Ukweli wa mambo ni kuwa hawa wananchi walioondoka kwenda nje ya nchi na kujifunza, kupata uzoefu wa nadharia na vitendo katika nyanja na fani tofauti ni rasilimali yenye thamani ambayo ni lazima ienziwe na kujengewa mazingira bora pale wao au watoto wao watakapoamua kurudi kulinufaisha taifa. Ni wazi kuwa taifa letu bado linahitaji wasomi katika fani mbalimbali ambao wanaufahamu mpana na uwezo wa kufanya maamuzi yenye maslahi ya taifa. Zaidi ya wasomi, kuna wanadayaspora wengi waliojenga biashara kubwa nje ya Tanzania ambao wana hamu kubwa kurudi kwao kuziendeleza biashara zao na kutoa ajira kwa maelfu ya raia wenzao. Uamuzi huu unakuja kutoka kwa watu waliona uzalendo na mapenzi ya nchi yao na itasikitisha kuona kama bunge la katiba litashindwa kulielewa hili.

Walioondoka Tanzania hawana uzalendo
Hii ni hoja nyingine ambayo hutumiwa na wale wanaopinga urai pacha, na ni kweli kusema kuwa baadhi ya watanzania walioondoka hawakuwa wazalendo na nchi yetu.  Vile vile kuna watanzania wengi waliopo Tanzania ambao hawana imani wala uzalendo na taifa letu. Kuna mifano mingi ambayo inaipa nguvu hoja hii. Kwa mfano nilishangazwa kuona misururu mirefu ya magari yakivuka mpaka kuelekea Kenya wakati wa uchaguzi wa kwanza  wa vyama vingi wa mwaka 1995. La ajabu zaidi, wale waliokuwa wakivuka mpaka walikuwa watanzania wenye asili ya asia na baadhi ya wazungu wakihofia kutokea machafuko kufuatia matokeo ya uchaguzi. Wengi wa hawa jirani zetu wa kiasia wana uraia wa zaidi ya nchi mbili na hawa ndio walioigeuza nchi yetu shamba la bibi kwa kukosa uzalendo na Tanzania na wako tayari kukimbia pale kunapotokea hali ya wasiwasi. Hawa bado wana hisia na mapenzi ya nchi mama walizotoka tukikubali au tukikataa.
Watanzania wengi waliopo ughaibuni bado wana mapenzi na uzalendo wa kutosha na nchi yao na ndio maana japo kuwa kuna baadhi yetu wasiounga mkono uraia pacha idadi yao ni ndogo kuliko wale wanaotaka uraia pacha. Bado watanzania waishio ughaibuini wanaguswa na majanga yanayotokea Tanzania na mara nyingi hufanya harambee kuchangisha pesa kusaidia wahanga, watoto yatima, mahospitali, mashule, kuchimba visima, kujenga barabara na orodha ya hisani hizi ni ndefu. Urai pacha utatupa nguvu, uhuru na moyo zaidi wa kusaidia nchi yetu kwa hali, mali, na fikra. Katika miaka ya karibuni kuna matawi mengi ya vyama vya siasa vya Tanzania ambayo yameanzishwa kwa imani kuwa  hii itakuwa moja ya njia ya kufikisha mawazo yetu katika ujenzi wa taifa. Haya hayatokei bila ya kuwa na mapenzi na uzalendo na nchi mama.

Watanzania wa ughaibuni hawachangii uchumi na ni hatari kwa usalama wa Taifa
Mchango wa wanadayaspora katika uchumi wa nchi za kiafrika na mahususi Tanzania ni mkubwa na unaotambulika na mashirika yote makubwa ya fedha  duniani. Katika utafiti uliofanywa na taasisi ya Brookings wa mwaka 2013, imeyakinishwa kuwa waafrika waliopo dayaspora hupeleka zaidi ya dolla billion arobaini kwa mwaka ambao huingia moja kwa moja katika uchumi tofauti na misaada toka nchi wahisani ambayo sehemu kubwa huishia kwenye urasimu na kukuza deni la taifa. Watanzania pekee hutuma zaidi ya dolla 300 kila mwaka moja kwa moja katika uchumi na kusaidia kwa kiasi kikubwa kuukuza uchumi wa taifa. Hiki kiasi kinachangia asilimia 2.4 ya pato la taifa.
Kiasi hiki cha pesa zinazoletwa nchini itaongezeka iwapo sheria ya uraia pacha itapitishwa na hoja hii inapewa nguvu kwa mifano hai toka nchi kama za Uganda, Nigeria na Kenya ambazo mara baada ya kupitisha sheria ya uraia pacha wanadayaspora wao  wamekuwa wakituma pesa zaidi ya mara dufu walizokuwa wakipeleka wakati hawana uraia pacha.  Kwa maelezo ya takwimu, wakenya wameongeza kutuma pesa kwenye uchumi wa Kenya hadi kufikia dolla milioni 791 kwa mwaka ambayo ni sawa na asilimia 3.8 ya uchumi wa taifa, waganda wanatuma dolla milioni 642 kwa mwaka sawa na asilimia 6.9 wakati wanaigeria hutuma billion 5, 397 sawa na asilimia 4.7 ya pato la taifa. Kwa mtaji huu mchango wa watanzania wa dayaspora ni wa kujivunia na kuenziwa kwa kupitisha sheria ya uraia pacha. Sisi wanadayaspora hatuna nia mbaya na nchi yetu na takwimu zinajieleza wazi.

Vizazi vya watanzania waishio ughaibuni havina haki ya uraia pacha
Hii ni hoja ambayo haina msingi na inapingana na sheria ya uhamiaji iliyopo sasa ambayo inampa uraia mtoto ambae amezaliwa na wazazi au mzazi ambae ni raia wa jamhuri ya Tanzania. Watoto hawa wana uhuru wa kuukubali au kuukataa uraia wa Tanzania pale wafikishapo miaka kumi na nane (18). Kwa vile sheria ya sasa ya uhamiaji inamvua uraia wa Tanzania mtu yoyote anaekubali uraia wa nchi nyingine wanadayaspora wanalishawishi bunge la katiba kuwafikiria mamilioni ya watoto wa watanzania ambao watapenda kuwa na haki ya nchi ya wazazi wao pale watakapoamua kurudi katika ujenzi wa taifa au hata pale watakapoamua kuja kutembelea ndugu na jamaa zao wasitakiwe kuwa na visa kwani kwa kufanya hivyo itakuwa ni kuwawekea vizingiti katika kushiriki kikamilifu katika kuienzi nchi yao.

Imeandikwa kwa niaba ya watoto wetu waliozaliwa au kukulia ughaibuni.

Na Baba Wangenya, Maryland USA

Chanzo: Vijimambo

No comments :

Post a Comment