dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Tuesday, September 16, 2014

Vietnam wamewezaje?

Home
Toleo la 370
10 Sep 2014
“KAMA kuna nchi ambayo ingekuwa na visingizio vya kuwa nyuma kimaendeleo kuliko nchi yeyote ya Afrika ni Vietnam. Iliharibiwa na vita nyingi dhidi ya China, Japan, Ufaransa na Marekani, iligawanywa na ukoloni na kuwekewa mifumo ya utawala ya kigeni na ilifuata siasa ya ujamaa kikweli kweli.
“Hii ingekuwa nchi masikini zaidi duniani. Hata hivyo, ikiwa imeanza bila kitu chochote, imeweza kuzishinda nchi nyingi za Kiafrika kwa kipato cha mtu kwa mwaka. Mabadiliko makubwa yalitokea pale viongozi wake walipoamua kuachana na sera kandamizi na kuanza kukuza uchumi wao kwa kasi.
“Matokeo yake imebakia katika njia ya kukuza uchumi na maendeleo kuliko Afrika” Haya ni maneno wa mwandishi Greg Mills na Mwenzake Jeffrey Herst katika kitabu chao ‘Africa’s Third Liberation: the new search for prosperity and jobs.
Nimechagua kipande hiki kuelezea namna ambavyo nchi iliyokuwa fukara wa kutupwa na yenye sifa kama zetu imeweza kujikwamua, kutokomeza umasikini na kuendelea kwa kasi.
Sikubaliani kiitikadi na Mills kwani yeye anaamini kabisa kuwa ni mfumo wa soko tu ndio suluhisho la matatizo ya Afrika wakati mimi ninaamini kuwa dola inapaswa kuchukua nafasi yake katika kuzuia makosa ya soko (market failures).
Hata hivyo, Vietnam na Tanzania zina mambo mengi yanayofanana na hivyo ni vema kuangalia wenzetu waliwezaje katika kutafuta kujikwamua na uduni wa maendeleo ya watu wetu.
Kama ilivyokuwa Tanzania, Vietnam ilifuata mfumo wa uchumi unaendeshwa na dola kwa kila kitu. Dola ilijenga viwanda na kuviendesha kama ilivyokuwa Tanzania.
Serikali ya Vietnam ilijenga viwanda vya nguo kama nguzo kuu ya kukuza ajira kwa watu wake. Kiwanda maarufu cha nguo nchini humo ni The Number Three Factory of May 10. Kiwanda hiki kiliajiri watu 3000. Tanzania nayo ilikuwa na viwanda maarufu kama Urafiki kilichoajiri watu 1500.
Baba yangu, Mzee Kabwe Zuberi Kabwe, alikuwa ni miongoni mwa vijana wa mwanzo kabisa kuajiriwa katika kiwanda hiki, walichukuliwa kutoka kila kona ya nchi kuendesha mashine na kuzalisha kanga, mashuka na kila aina ya vitambaa vya nguo.
Leo Kiwanda hiki cha Hanoi kinaendelea kufanya kazi, hiki cha Urafiki sina uhakika. Mara ya mwisho nimemsikia Mbunge wa Ubungo akitaka Kamati Teule ya Bunge kuhusu utendaji wa kiwanda hiki. Tanzania ilikuwa na viwanda vya nguo 12 nchi nzima.
Kama nilivyopata kuandika katika siku za nyuma, viwanda hivi vilijengwa kimkakati ili kuhakikisha kwanza pamba inayozalishwa Tanzania inaongezewa thamani nchini na pili kuzalisha ajira kwa wananchi, kuongeza kipato na kutokomeza umasikini.
Kama Tanzania, Vietnam walifuata sera za kurekebisha uchumi wao ikiwemo kubinafsisha baadhi ya viwanda vyao ili kukuza ufanisi. Kiwanda cha The Number Three Factory of May 10 kilibinafsishwa mwaka 2001 kwa kuuza sehemu ya hisa zake kwa watu binafsi.
Kutokana na uwekezaji uliofanyika, hivi sasa kiwanda hicho kimeajiri watu 8000 na kinauza Ulaya mashati, suruali na fulana zenye thamani ya Dola za Marekani milioni 40 kwa mwaka. Ukuaji huu upo pia katika sekta nzima ya nguo.
Hivi sasa Vietnam ina makampuni 3700 ya nguo yenye kuajiri watu milioni mbili na nusu. Mauzo ya nguo kutoka Vietnam hivi sasa yana thamani ya Dola za Marekani 11.2 bilioni kwa takwimu za mwaka 2010.
Tanzania hivi sasa inauza pamba takribani yote inayozalishwa nchini kama ghafi na takribani viwanda vyote vya nguo vilivyobinafsishwa havifanyi kazi na vingine vimegeuzwa maghala.
Maendeleo hayo katika sekta ndogo ya nguo yaliendana kabisa na maendeleo katika sekta ya Kilimo. Mwaka 1990, Vietnam ilikuwa inaagiza mchele kutoka nje (net importer) lakini mwaka 2005 nchi hiyo ilikuwa ya pili duniani kwa kuuza mchele nje ya nchi.
Asilimia 31 ya mchele unaouzwa na Vietnam hununuliwa na nchi za Afrika, zenye ardhi kubwa zaidi na rutuba kuliko Vietnam. Uzalishaji wa kahawa pia uliongezeka na kuifanya nchi hiyo kuwa ya pili duniani baada ya Brazil kwa kuuza kahawa katika soko la dunia ambapo waliuza tani 900,000 za kahawa mwaka 2012.
Mwaka huo, Tanzania iliuza tani 71,000 tu za kahawa. Kwa upande wa korosho, Vietnam sio tu imeweza kuongeza uzalishaji lakini imeachana na kuuza korosho ghafi na pia hivi sasa ina teknolojia yake ya mashine za kubangua korosho na kuiuza nje.
Mwaka 2012 nilipotembelea viwanda vya korosho vilivyobinafsishwa, niliona mashine hizi kutoka Vietnam katika kiwanda cha Mtwara Mjini kinachoendeshwa na kampuni ya Olam kutoka Singapore.
Mifano hii ya nchi ya Vietnam inatuambia jambo moja kubwa kuwa inawezekana kabisa kuleta maendeleo ya watu na nchi kwa haraka. Kinachotakiwa ni sera makini, dhamira na uwezo wa kutekeleza sera bila kutetereka.
Vietnam walifanya ubinafsishaji kama Tanzania, lakini wao walihakikisha kuwa mali za taifa zilizojengwa na watu wote katika Taifa hazipotei. Walihitaji teknolojia mpya na mitaji ilhali wakiendelea kushikilia sehemu kubwa ya viwanda ili kuhakikisha havigeuzwi maghala.
Pia walitofautisha ‘privatisation’ na ‘liberalisation’ ambapo kulegeza masharti ya biashara haikumaanisha kuuza kila kitu. Bali walikaribisha mitaji binafsi kushindana na mitaji ya umma na hivyo kukuza uzalishaji.
Vietnam iligawa mashamba ya umma kwa raia wake mmoja mmoja na kuwawezesha kuzalisha kwa viwango na tija. Miradi mikubwa ya uzalishaji mchele iliyokuwa ya umma haikuuzwa kwa makabaila bali iligawiwa vipande vya ekari kumi kumi na kugawa kwa wananchi ili wazalishe.
Hapa Tanzania mashamba mengi ya Ushirika yaliachwa tu na kutelekezwa na mengine kuuzwa kwa ‘wawekezaji’. Mwaka 2009 nilikwenda wilayani Mbarali nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya POAC kukagua zoezi la ubinafsishaji ambapo nilikuta Serikali imeuza shamba la Kapunga na kijiji kizima cha Kapunga. Mgogoro wa Kapunga bado unaendelea mpaka sasa na uzalishaji wa mwekezaji umesimama.
Vietnam ilijifunza kutokana na makosa ya sera yao ya ukomunisti na kuamua kufanya mabadiliko makubwa ya kiuchumi. Dhamira kubwa ilikuwa ni kuona watu wa Vietnam wanaondokana na Ufukara na sio kuondoa ufukara wa wachache wenye maslahi na mfumo wa dola.
Mabadiliko ya kiuchumi yaliyofanyika Tanzania yameshindwa kwa sababu moja kubwa kwamba waliokuwa wanatekeleza mipango hiyo walijitazama wao badala ya kutazama Taifa. Ndio Maana viwanda vingi vilivyouzwa kwa ‘wazalendo’ havifanyi kazi kwa sababu ‘wazalendo’ hawa walikuwa ni watu wenye maslahi na sio watu wenye dhamira ya kuendeleza.
Hebu tukaeni na kujitafakari upya. Vietnam wamewezaje na sisi tushindwe?
Wasiliana na mwandishi
Zitto Kabwe
  +255-756809535
http://www.zittokabwe.comZitto Kabwe ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Naibu Kiongozi wa kambi ya Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali.
See more at: http://www.raiamwema.co.tz/vietnam-wamewezaje#sthash.lRS9ZYEl.dpuf

No comments :

Post a Comment