
Wakizungumza katika mkutano na wanahabari jana jijini Dar es Salaam Mwenyekiti wa JUVICUF, Hamidu Bobali, alisema Rais Kikwete ana haja ya kuomba radhi umma kwani kitendo hicho kilichotokea ni cha kiudhalilishaji .
Hivi karibuni huko Mtoni Mtongani Dar es Salaam , polisi ilimkamata na kumpiga Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, viongozi wengine pamoja na wananchi, kwa kile kilichodaiwa ni kukaidi amri ya kufanya maandamano yaliyozuiliwa na polisi.Bobali alisema kitendo cha kupigwa kwa viongozi hao ni cha udhalilishaji na kwamba JUVICUF imebaini hizo ni mbinu chafu zilizoandaliwa na serikali ya CCM kumdhalilisha mwenyekiti wao pamoja na viongozi wandamizi wa chama hicho.
“Hali hii ilionekana jinsi ilivyojiandaa kuhakikisha wanatimiza azma yao waliotumwa na watu na baadhi ya watu kuwapiga viongozi wetu kwa kutumia nguvu kupita kiasi na hata kutumia silaha ambazo sio stahiki katika harakati za kioparesheni za polisi,” alisema
Aliongezea kusema: “Chakusikitisha zaidi ni kauli iliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe, imeonyesha jinsi ambayo ilikuwa ni mpango wa serikali ya CCM na kuendeleza agizo la Waziri Mkuu Mizengo Pinda alilolitoa bungeni kuwa watapigwa tu.”
Alisema umoja huo umeazimia mambo mbalimbali ikiwamo kumtaka Waziri Chikawe kujiuzulu kufuatia tukio hilo pamoja na kauli yake ya uongo ambayo ameitoa juzi bungeni.
Pia vijana wa CUF wameitaka serikali izifute kesi zote zilizopo mahakamini zilizotokana na tukio la Januari 27 mwaka huu, siku ambayo chama hicho kinaadhimisha mauaji ya wafuasi kadhaa wa chama hicho yaliyofanyika miaka ya nyuma.
Bobali alisema JIVICUF imeazimia kuandaa maandamano makubwa ya kulaani vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu vinavyofanywa na serikali ya CCM kupitia polisi.
Alisema watatoa taarifa za maandamano wakati wowote na kueleza yatafanyika lini na endapo wakinyimwa kibali yatafanyika bila kuhofu.
Hata hivyo, alisema wanamtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Ernest Mangu , asikubali kutumiwa na wanasiasa kwani wananchi wanaendelea kuliona jeshi hilo kuwa limekosa watu wanaoweza kujenga hoja mbele ya umma.
Alisema jeshi hilo limetoa taarifa ya kudai kuwa wamezuia maandamano hayo kutokana na kuibwa silaha katika kituo cha polisi cha Ikwiriri mkoani Rufiji zikihofiwa kuwa zipo jijini Dar es Salaam.
“Hivi kuibwa kwa silaha hizo kuna husiano gani na maandamano yetu wakati wao CCM wameandaa maandamano makubwa huko Songea kusherehekea miaka 38 ya kuzaliwa CCM huko Songea hivi silaha hizo hazifiki Songea?” alihoji na kuendelea kusema
“Wana CCM wamesafiri kutoka mikoa kwa nini basi polisi wasihofu yawezekana hatari kutokea Songea ambapo wananchi wanaweza wakawa na visasi na mafisadi pamoja na wezi wa rasilimali za taifa?,” alisema
Wakati huo huo wafuasi wa Chama cha Wananchi (CUF), wapatao 30 wameachiwa huru katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana baada ya kutimiza masharti ya dhamana.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment