dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Monday, August 31, 2015

ACT-Wazalendo yavishukia CCM, Ukawa.

Kiongozi mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo Zitto Kabwe.
Chama cha ACT-Wazalendo kimezindua rasmi kampeni zake za uchaguzi mkuu wa urais, wabunge na madiwani huku Kiongozi Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe, akisema mabadiliko ya nchi hayawezi kuletwa kwa kuwatumia watu wale wale aliyodai kuwa ndiyo walioingiza nchi katika shida iliyopo kwa sasa.
Katika uzinduzi wa kampeni hizo uliofanyika jana katika Uwanja wa Zakhem Mbagala, Temeke jijini Dar es Salaam huku ukihudhuriwa na umati mkubwa, Zitto
alisema CCM na Ukawa wanahubiri kuwaletea mabadiliko Watanzania, lakini wanashindwa kueleza ni namna gani ambavyo wataleta mabadiliko hayo.
Alisema viongozi wote waliopita  walishindwa kusimamia nchi iondokane na  na vitendo vya  ufisadi  na kuwaomba wananchi kufanya mabadiliko ya uongozi kwa kumchagua rais mwanamke.
Alisema chama hicho kikiingia madarakani kitarejesha miiko ya uongozi kwa kuhakikisha viongozi wote wanataja mali zao ili zifahamike kwa Watanzania.
Zitto alisema ACT Wazalendo ndicho chama pekee chenye uwezo wa kurudisha uzalendo wa taifa hili katika kukabiliana rushwa na ufisadi.
Alisema bila vyama kuweka misingi ya miiko na maadili ni vigumu kwao kukabiliana na vitendo vya rushwa na kifisadi nchini.
Kiongozi huyo alisema CCM ina mawaziri wakuu wa zamani wanne na Ukawa wanao mawaziri wakuu wa zamani wawili na wote katika kampeni zao wanahubiri mabadiliko wasiyoweza kuyaleta.
Alisema wagombea kutoka vyama vingine  wanatoa ahadi mbalimbali kama vile kuboreshewa huduma za jamii lakini hawaelezi namna watakavyoweza kuzipata fedha za kutekeleza ahadi hizo.
Kwa upande wa mgombea urais kwa tiketi ya chama hicho, Anna Elisha Mgwira, akijinadi kwa kusema endapo wananchi watampa ridhaa ya kuwa rais, ataunda serikali ya umoja wa kitaifa itakayoundwa na vyama vya siasa na asasi za kiraia wenye sifa ya uzalendo na uadilifu.
Anna alisema mfumo wa maisha wa nchi umeshidwa kutoa fursa ya kuthamini wanawake na kwamba mwaka huu ni wa utu, uzalendo na uadilifu mambo ambayo alidai kuwa Hayati Mwl. Julius Nyerere aliyasisitiza.
“Nitaunda serikali itakayotokana na makundi mbalimbali ya umma. Serikali hii itakapoundwa, itarudisha makao makuu ya kuwa Dodoma kwani Dodoma maana yake ni kuwaleta watu kutoka maeneo mbalimbali,” alisema.
Alisema baada ya miaka 50 ya uhuru , Watanzania wanahitaji  mabadiliko yakiwamo ya kisera na kijinsia.
VIPAUMBELE 
Alisema ilani ya uchaguzi ya ACT-Wazalendo imebeba vipaumbele vikubwa vinne huku akivitaja kuwa ni hifadhi ya jamii ambao ni mfumo imara na endelevu kwa wananchi kujiwekea ili kukabiliana na majanga mbalimbali kwani hadi sasa ni asilimia tisa tu ya wananchi wapo katika mfumo wa hifadhi ya jamii.
“Chama hiki kitakapopata ridhaa kitahakikisha asilimia kubwa ya wananchi wanaingia katika mfumo wa hifadhi ya jamii,” alisema.
Alitaja kipaumbeele cha pili kuwa ni kutengeneza uchumi shirikishi ili kuwawezesha Watanzania kuwa na akiba na kuweza kujiajiri. Kwa mujibu wa mgombea huyo, uchumi shirikishi utasaidia  sekta za kilimo, viwanda, elimu na ajira.
Alisema ACT-Wazalendo kitahakikisha kinatoa kipaumbele katika kufufua viwanda ili kuibua ajira zaidi. 
Kuhusu  uchumi wa gesi na mafuta, alisema serikali ya chama hicho itahakikisha wananchi wananufaika na rasilimali hizo kikatiba.
Alitaja kipaumbele cha tatu kuwa ni afya kwa madai ya kwamba Tanzania ina mfumo mbovu wa utoaji wa huduma za afya. Akitolea mfano kwamba wanawake wanapata shida wakati wa kujifungua kutokana na huduma hizo kwa sabahu ya kukosekana kwa uadilifu na uzalendo.
Alisema kila mwananchi atafikiwa na huduma za afya kikatiba hivyo kupunguza vifo kwa watoto.
Kipaumbele cha nne alikitaja kuwa ni elimu, akisema elimu inayotolewa kwa sasa haiwezi kuwasaidia wahitimu. Mgombea huyo, alisema watoto wanahitimu elimu ya msingi na sekondari wakiwa hawajui kusoma wala kuandika.
“Kutokana na mfumo mbovu wa elimu, kumesababisha kuwapo kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu,”alisema.
Katika kukabiliana na hilo alisema, atahakikisha anakuza elimu kwa kina mama na watu wazima.
Kuhusu kodi, alisema akichaguliwa kuwa rais ataondoa utitiri wa kodi zisizo za lazima na kuhakikisha anayabana makampuni makubwa ya kigeni yanayokwepa kodi.
Kadhalika mgombea huyo alisema endapo ACT-Wazalendo kitaingia madarakani, kitamchagua Zitto kuwa Waziri Mkuu wa awamu ya tano.
PROF. MKUMBO: RAIS NI MLINZI
Akizungumza katika uzinduzi huo, Mshauri wa ACT-Wazalendo, Prof. Kitila Mkumbo, alisema rais ndiye mlinzi mkuu wa tunu za taifa, umoja, usalama na mwenye kujali wanyonge na siyo kuwa mateka wa matajiri.
Alisema rais ambaye Watanzania wanamtaka lazima awe ni yule atakayelinda muungano na mwenye uwezo wa kutafuta suluhisho la kero za muungano huo.
Alisema ni vema Watanzania wakaepuka kuchagua kwa kufuata mbwembwe za vyama, ulaghai, na badala yake kuongozwa na sera za chama.
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment