Vitimbwi hivyo vilianza kujitokeza jana jijini Dar es Salaam saa 3:30 baada ya mgombea Urais kwa tiketi ya Chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP), Fahmi Dovutwa, kuwasili Nec saa 3 asubuhi na kupanda moja kwa moja ghorofa ya saba kuchukua fomu.
Baada ya kuchukua fomu hiyo akiwa ameambatana na mgombea mwenza, Hamad Ibrahim Mohamed na watu wengine zaidi ya watano, walipanda lifti za ghorofa hilo ili kushuka.
Katika hali isiyotarajiwa, baada ya kufika ghorofa ya nne, umeme ulikatika na kulazimika kukaa kwenye lifti hiyo zaidi ya dakika kumi huku wakipiga namba ya dharura.
Vijana wa uokoaji walifika na kufanikiwa kuufungua mlango wa lifti kwa chuma na kuwatoa waliokuwamo huku wengine wakibebwa kutoka ndani baada ya eneo walikokwama kutokuwa na sehemu ya kushukia.
Akizungumza na waandishi wa habari nje ya jengo hilo mara baada ya uokoaji huo, Dovutwa alisema tatizo si la Tanesco bali la CCM la kuruhusu viongozi wake kumiliki maduka ya majenereta.
Dovutwa alisema ameamua kuchukua fomu kwa sababu matatizo yaliyopo Tanzania ni sera na utekelezaji wake.
Mgombea Urais kwa tiketi ya Tanzania Labour Party (TLP), Macmillian Lyimo alifuatia kuchukua fomu na wapambe wake ambao wakati wakipandisha ngazi ya kuingia kwenye jengo hilo, mmoja wao alijikwaa na kuanguka.
Lyimo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa, uchaguzi wa mwaka huu utakuwa wa historia kwa miaka 50 iliyopita kwa kuwa utawapatia kiongozi wasiomtarajia.
Mgombea kupitia Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, alisema kuwa, haki ya mgombea binafsi imeporwa.
“Amri ya Mahakama Bara la Afrika ilitaka utaratibu wa kuchukua fomu uwe na mgombea huru lakini haki hii imeporwa hivyo kesi zitakuwepo lakini tutaenda mahakama ipi ikiwa hii ya Afrika imedharaulika,” alisema.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI


No comments :
Post a Comment