- ALIYEKUWA Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anne-Kilango Malecela, aliiacha ofisi saa 5:00 usiku baada ya Rais Rais John Magufuli, kutangaza kutengua uteuzi wake Jumatatu iliyopita.
Aliondoka ofisini hapo akiwa mwenye huzuni na kupanda gari la serikali lililompeleka katika Hoteli ya Karena aliyokuwa akiishi tangu aliporipoti katika kituo chake cha kazi kama Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.
Habari za ndani ambazo Nipashe ilizipata, zilisema baada ya Kilango kupata taarifa ya kutimuliwa kazi, aliitisha ghafla kikao cha wakuu wa idara zote pamoja na wakuu wa wilaya zote na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa.Kilango na Katibu Tawala wa Mkoa huo, Abdul Dachi, walifutwa kazi na Rais Magufuli, baada ya kuwasilisha taarifa za uongo kuhusu mkoa huo kutokuwa na watumishi hewa, hali iliyomtia wasiwasi Rais Magufuli na kuagiza uchunguzi ufanyike.
Baada ya uchunguzi kufanyika, iligundulika kuwapo kwa wafanyakazi hewa 45 waliokuwa tayari wamelipwa mishahara na kazi ya kuhakiki ilikuwa bado inaendelea.
Ilidaiwa baada ya Kilango kupokea taarifa za kutenguliwa nafasi yake, aliwaita viongozi wote wa ofisi yake, wakuu wote wa wilaya, Kamati ya Ulinzi na Usalama na kukaa nao ofisini tangu mchana hadi saa 5:00 usiku wakijadili mambo mbalimbali.
Baada ya majadiliano hayo ya kuwaaga viongozi hao, Kilango alitoka nje na kupanda gari la ofisi lililompeleka Hoteli ya Karena.
Mpaka sasa Kilango bado yupo mkoani hapa akisubiri kumkabidhi ofisi mkuu wa mkoa mpya atakayeteuliwa na Rais Magufuli.
Aidha, habari zilisema mizigo ya Kilango ilitarajiwa kuwasili wiki hii wakati wowote, lakini kutokana na kutenguliwa uongozi wake, mizigo hiyo haitaletwa tena mkoani Shinyanga.
Aidha, habari zinadai kuwa mpaka sasa Mkoa wa Shinyanga umebaini kuwapo kwa watumishi hewa 102, licha ya kwamba taarifa rasmi hazijawekwa hadharani.
Nipashe
No comments :
Post a Comment