dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Wednesday, April 26, 2017

Maalim Seif asema Profesa Lipumba anaihofia ofisi ya Mtendeni!

MGOGORO ndani ya Chama Cha Wananchi (CUF), unaendelea kuchukua sura mpya baada ya Mwenyekiti wa chama hicho anaetambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba, kudai kumvua wadhifa Katibu Mkuu wake, Maalim Seif Sharif Hamad kwa madai ya kushindwa kazi ndani ya chama hicho.

Mgogoro huo ambao umedumu takriban mwaka mmoja sasa na ulianzia pale Profesa Lipumba alipojiuzulu wadhifa wa uenyekiti kabla ya uchaguzi wa Oktoba 25, 2015 na kusema ataendelea kuwa mwanachama wa kawaida. 

Wakati Profesa huyo alipojiuzulu nafasi hiyo chama hicho kilikuwa katika wakati mgumu kutokana kukabiliwa na Uchaguzi Mkuu wa 2015 ambapo CUF ndicho chama kinachotoa ushindani mkubwa wa kisiasa kwa CCM hasa kwa upande wa visiwani Zanzibar.
Licha ya CUF kuwa na wakati huo mgumu lakini chama hicho kilipambana na kuingia katika uchaguzi huo bila ya kuwa na Mwenyekiti lakini hatimaye kiliweka historia kwa kupata majimbo 10 ya uchaguzi Tanzania Bara na majimbo 25 kwa upande wa Zanzibar ingawa uchaguzi huo Zanzibar ulifutwa kwa madai mbalimbali yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Salim Jecha. 

Baada ya kufutwa kwa uchaguzi huo Zanzibar, ZEC ilitisha uchaguzi mwingine wa marudio Machi 20 mwaka 2016 lakini chama cha Wananchi CUF kilisusia uchaguzi huo na hatimaye CCM ikaibuka na ushindi wa kishindo. 

Tangu wakati huo CUF bado haiko sawa kutokana na kukukabiliwa na mgogoro ndani ya chama hicho na wanachama wake kugawanyika katika makundi mawili, lile linalomuunga mkono Profesa Lipumba ambaye baada ya kujiuzulu nafasi ya Mwenyekiti alitengua nafsi hiyo na hivi sasa anatambulika na Msajili wa Vyama vya Siasa kuwa ni Mwenyekiti halali wa chama hicho. 

Kundi la pili ni lile linaloungwa mkono na Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad, ambaye anamvuto mkubwa wa kisiasa visiwani Zanzibar na yeye hatambui wadhifa wa Mwenyekiti wa CUF Profesa Lipumba. 

Mwishoni mwa wiki iliyopita Profesa Lipumba naye alitangaza kumwajibisha Maalim Seif Sharif Hamad kwa kumvua wadhifa wake wa Katibu Mkuu kwa madai kuwa ameshindwa kazi ndani ya chama hicho kwani ameshindwa kuhudhuria vikao katika ofisi kuu za chama hicho zilizopo Buguruni Jijijini Dar es Salaam. 

Kutokana na hatua hiyo Maalim Seif Sharif Hamad, alisema Profesa Lipumba hana mamlaka hayo kwanza siyo mwanachama tena wa CUF, hivyo yeye ndie Katibu Mkuu wa chama hicho na maamuzi yake ni batili hayakubaliki kisheria na kikatiba. 

Mwishoni mwa wiki iliyopita akiwa katika ziara yake ya kichama Kisiwa cha Tumbatu Maalim Seif, alisema mgogoro unaoendelea ndani ya chama hicho umesababishwa na Msajili wa vyama, Jaji Francis Mutungi kwa kitendo cha kumhalalisha Profesa Lipumba kuwa Mwenyekiti wa CUF wakati alijiuzulu mwenyewe nafasi hiyo lakini pia alishafukuzwa uwanachama na Baraza Kuu. 

Maalim Seif alimshauri Rais wa Jamuhuri ya Muungano Dk. John Pombe Magufuli kumchukulia hatua Mrajisi wa Vyama vya Siasa Jaji Mutungi kutokana na kile walichodai kuwa msajili huyo amekuwa akivunja sheria. 

“ Tumameshangazwa na kitendo cha rais wa Dk. John Pombe Magufuli kuwawajibisha watendaji wasio waadilifu huku akimuacha msajili wa vyama vya siasa,”alisema. 

Maalim Seif alisema kuwa msajili huyo ni wakutumbuliwa kama wanavyotumbuliwa watendaji wengine kwa sababu siyo mwadilifu na amesababisha mtafaruku mkubwa kwa wananchi na wanachama wa CUF. 

“Rais Magufuli anatumbua watendaji ambao siyo waadilifu lakini Msajili wa Vyama vya Siasa amemuacha kwasababu huyu mtu ametuvuruga na anaendelea kutuvuruga,” alisema

Alisema msajili huyo amempa uhalali Profesa Ibrahim Lipumba kuwa Mwenyekiti wa CUF wakati alijiuzulu mwenyewe kabla ya uchaguzi mkuu na hivi sasa amekuwa akikihujumu chama. 

Alisema Lipumba wa sasa ni tofauti na yule wa 2010 kwani hivi sasa amekuwa akiihujumu CUF kwa makusudi kwa kushirikiana na wadau wake mbalimbali. 

Aidha, alisema baadhi ya askari wa vyombo vya dola wamekuwa wakitumika kisiasa na wanafanya kazi kwa ubaguzi na kuegemea upande mmoja wa chama tawala. 

Hata hivyo, aliwatoa hofu wafuasi wa chama hicho kuwa yeye ndiye Katibu Mkuu wa CUF wala wasibabaishwe na kitendo cha Profesa Lipumba kutangaza kumvua wadhifa huo. 

“Eti Lipumba anasema kuwa mimi nimeshindwa kazi akidai kuwa siendi ofisi kuu ya CUF Buguruni mbona na yeye haji makao makuu ya CUF Mtendeni……Lipumba hana mamlaka hayo ya kuniondoa nafasi yangu ya ukatibu mkuu”alisema. 

Alihoji kuwa tangu Agosti mwaka 2015 Lipumba hajakanyaga makao makuu ya CUF Mtendeni yaliyopo Unguja na yeye pia ameshindwa kazi. 

Alisema hata kama Lipumba angekuwa Mwenyekiti halali wa chama hicho alipaswa kumuita na kumhoji yeye Katibu Mkuu kwa nini haendi ofisi kuu za chama hicho Buguruni kuliko kuchukua madaraka ya kujaribu kumuondoa kwenye wadhifa wake.

Akizungumza na wananchi wa kisiwa hicho kidogo cha Tumbatu Maalim Seif alielezea kuchukizwa na kitendo cha siasa za chuki na uhasama zilizotawala kisiwani humo kati ya CCM na CUF na kufikia hatua ya kupigana na kuhujumiana kwa kuchomeana nyumba moto kwa itikadi za kisiasa. 

Tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa, wananchi wa kisiwa kidogo cha Tumbatu wamegawanyika kisiasa kati ya Wananchi wa Tumbatu Uvuvini ambako ni ngome ya CCM na Tumbantu Jongowe ambayo ni ngome ya CUF. 

No comments :

Post a Comment