dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Wednesday, July 5, 2017

SMZ Kutenga 1b/= Kwa Ununuzi wa Mashine ya DNA. Lapokelewa Kwa Shangwe na Wanaharakati, Waathirika Mimba za Umri Mdogo!

Image result for dna machine

Na.Haji Nassor - Pemba.
WALISHASEMA waliotutangulia kuwa, nguo ya kuazimwa haiendewi ngomani.

Walijenga hofu kuwa, maana mwenyewe anaweza kukuadhiri, au hata kukuvua na pengine ngoma ndo kwanza ‘inogele’.
Hawa, hawakuwa tofauti na wale waliotuambia kuwa, mtegemea cha ndugu hufa masikini.Yote kwa yote, kumbe kumiliki chako ni jambo la faraja, maana unaweza kukitumia, kukipunzisha wakati wowote uupendao.

Na ndio maana kauli hizo na nyengine, zimekuwa zikirejewa mara kwa mara na wanaharakati wanaopambaana na magwiji wanaowapa watoto mimba za umri mdogo.hapa Zanzibar.

Wanaharakati hawa wamekuwa wakisaka mwarubaini na tatizo hilo kwa mtoto wa kike, miaka nenda miaka rudi, ingawa kikwazo wanachokumbana nacho ni ukosefu wa mashine ya vina saba ‘DNA’ Zanzibar.Changamoto ya mashine hiyo, imeshabisha hodi serikali kuu, baada ya wanaharakati hao na waathirika wa mimba za mapema kuwa na sauti moja kwa muda mrefu sasa.

Mdau mkuu wa kadhia hizi Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania ‘TAMWA’ kimekua kikihaha kila kona ya dunia, kuona kundi hili la watoto wa kike linakuwa huru kama yalivyo makundi mengine.

Afisa Miradi wa TAMWA ofisi ya Zanzibar, Asha Abdi Makame, anaesema wamekuwa wakisaka, kwanza uwezo wa kuwafikia walengwa, ili kuwapa taaluma ya kujikinga na kadhia hiyo.

“Sisi kama TAMWA kwanza tuntoa elimu ya athari za ndoa za mapema na mimba za umri mdogo, lakini hata waandishi wa habari huwa tunawapa elimu ili kuvitumia vyombo vyao kuelimisha hili’’,alisema.

Yeye anasema, TAMWA pamoja na shughuli zake nyengine, lakini suala la kupiga vita mimba na ndoa za mapema, wamelipa kipaumbele cha pekee, maana hata hivi karibuni baada ya kuhangaika wamepata mradi.

“Mfano wenzetu wa EU, wametufadhili ingawa tumeshirikiana na Shiriaka la Kimatafa la Idadi ya Watu ‘UNFPA’ kuwa mradi wa kupiga vita mimba na ndoa za mapema kwa watoto wa wasichana, sasa tunatarajia mafanikio’’,alifafanua.

TAMWA inakiri kuwa ukosefu wa mashine ya DNA, ni moja ya ukuta mkubwa wa kumaliza kesi za mimba za umri mdogo wa watoto wa kike, kutokana na Zanzibar kutokuwa na mashine yake yenyewe.

Analalamika kuwa kuwepo kwa mashine hiyo hospitali ya Muhimbili pekee, ni udhaifu mkubwa, kwa wale watoto wa kike waliopewa ujauzito na kisha kesi zao zikahitaji ‘DNA mahakamani.

‘’Unajua nguo ya kuazimwa haiendewi ngomani, sasa lazima serikali inunue yake yenyewe, inaweza kuwa mwarubaini wa kuzipunguza ama kuzimaliza kesi za mimba za mapema kwa watoto wetu’’,alisema.

Aliekuwa Mdhamini Afisi ya Mkurugenzi wa Mahitaka Pemba wakati huo Al-baghiri Yakout Juma, anasema wanazo kezi zaidi ya 12 ambazo zinaendelea kusota kwenye mahakama za Mkoa, zikisubiri kipimo cha ‘DNA’ kilichopo hospitali ya Muhimbili.

“Unajua zinapopelekwa ‘sampuli’ kwa ajili ya kipimo cha ‘DNA’ Hospitali ya Muhimbili, ni sawa na kusema ndio mtoto wa kike ameshakoseshwa haki yake, maana matokea hadi kurudi ni zaidi ya mwaka mmoja’’,anasema.

Mtoto wa kike (19) ambae anakesi katika mahakama ya Mkoa Chake chake, tokea mwaka 2013, kwa sasa ameshajifungua na mwanawe anasoma skuli ya maandalizi, ambapo kesi yake inasubiri matokeo ya ‘DNA’.

“Sina hakika kwamba kesi itatolewa hukumu, maana hata alienipa ujauzito ameshamaliza kusoma chuo, na sasa yuko Unguja, anakuja kila baada ya miezi miwili kughairishiwa kesi yake’’,anasema.

Nae muathirika wa mimba ambae amejifungua mwaka 2014 na tayari sampuli ya damu imeshachukuliwa na kupelekwa Muhimbili, anasema hana hakika sana kwamba kesi yake itamalizwa.

“Nasikia wapo wenzangu wana miaka zaidi ya minne bila ya matokeo kurudi, sasa lazima Zanzibar iwe na ya kwake ili kupunguza foleni mahakamani, na sisi tupate haki zetu mapema’’,alifafanua.

Yeye anasema kama serikali ya Zanzibar haina uwezo wa kununua mashine ya ‘DNA’ ni vyema iwaombe wafadhili kama EU, UNESCO, DANIDA, WHO ili wanunue, maana vyenginevyo wengine watakosa haki.

Fatma Marouz Kombo ambae ni Makamu Mwenyekiti wa Jumuia Kuelimisha Athari za Madawa wa Kulevya, Ukimwi na Mimba za Utotoni ‘JUKAMKUM’ Pemba, anasema mwarubaini pekee wa kuzimaliza kesi za mimba ni kuwepo kwa mashine ya ‘DNA’ Zanzibar, ambayo ndio chaka la vyombo vya sheria kwa sasa.

“Wakati umefika kwa serikali kununua mashine ya ‘DNA’ ili hawa wanaowapa mimba watoto wetu, wasiwe na pakukimbilia, maana sasa wamekuwa wakidunda mitaani, kwa vile hichi kipimo hakipo kwetu’’,aliweka wazi.

“Inaweza kuwa juhudi zetu za kutomeza hilo zikawa butu, iwapo serikali yetu haitoharakisha kumiliki mashine yake ya ‘DNA’ badala ya kutegemea ilioko Muhimbili’’,alifafanua.

Ali Mbarouk Omar ambae ni Afisa Mawasiliano wa Klabu ya watoto Pemba ‘PCC’ anasema uwepo wa mwashine ya ‘DNA’ wahalifu wa kuwapa mimba watoto watafikia mwisho.

“Lakini hata ukienda Dawati la jinsia la wanawake na watoto na mahakamani, kesi nyingi zimelala sababu ikiwa ni kukosekana kwa kipimo cha DNA, sasa ni kazi kwa serikali, kuinunua na kuondoa adha hiyo’’,alifafanua.

Katibu wa Jumuia ya Kupunguza Umaskini na Kuboresha Hali za Wananchi Pemba (KUKHAWA) Hafidh Abdi Said, anasema pamoja na ushahidi kukamilika, bado tatizo la kukosekana kwa mshine ‘DNA’ ni changamoto nyengine katika vyombo vya kisheria.

Hivyo vyombo vya sheria nchini, wametakiwa kuacha kisingizio cha ukosefu wa kipimo cha vina saba ‘DNA’ na kuwaachia huru wanaowadhalilisha wanawake na watoto, ikiwa ni pamoja na wanaowapa mimba.

Afisa Mipango wilaya ya Chakechake Pemba, Kassim Ali Omar nae akifungua kongamano la siku moja, la kupinga ukatili wa kijinsia, lililoandaliwa na jumuia ya kimataifa ya ‘YUNA’ alipigia chapuo kuweko kwa mashine hiyo hapa Zanzibar.

“Sio busara kwa vyombo hivyo, kupata kichaka cha ukosefu wa kipimo hicho, na hatimae kuwaacha watoto wa wanawake, wakiwa wamedhalilika na wakosaji, kudunga mitaani’’,anafafanua.

Akizungumza kwenye mdahalo huo, Mkuu wa Idara ya wanawake na watoto wa Wizara ya uwezeshaji, ustawi wa Jamii maendeleo ya wanawake na watoto Pemba wakati huo, Sara Khamis Salim, anasema wazazi wamekuwa wakijitahidi katika malezi, ingawa watoto hubuni njia ya kuwatoroka.

Afisa mkuu wa dawati la jinsia na watoto la Polisi mkoa wa kusini Pemba, Asha Talib, anasema wamekuwa wakikabiliwa na changamoto kadhaa, katika kutomeza kesi za udhalilishaji wa kijinsia.

Polisi kwa makusudi limeanzisha madawati zaidi ya 417 Tanzania, ili kuhakikisha wanawake na watoto wanaishi bila ya ukatili, ingawa jamii imekuwa ikiviza nguvu hizo kwa kutokuwa tayari kutoa ushirikiano.

Hivi karibuni Mkuu wa upelelezi na makosa ya jinai Jeshi la Polisi wilaya ya Micheweni Pemba, Suleiman Khamis Juma, wakati akitoa mada juu ya majukumu ya jeshi la Polisi, ukumbi wa Benjamin Mkapa Pemba, anasema kuwa kushughulikia makosa ya udhalilishaji na ulawiti ni moja ya jukumu la jeshi la polisi.

Chakufurahisa afisa huyo anaeleza kwenye kongamano hilo kuwa, jeshi la polisi kwa sasa linamchakato wa kujenga maabara kubwa na ya kisasa katika maeneo ya wilaya ya Kibaha mkoani Pwani, kwa lengo la kupunguza usumbufu na msongamano wa vipimo vya vinasaba DNA.

Mwanasheria wa serikali kutoka ofisi ya DPP Zanzibar ofisi ya Pemba, Ali Haidari Mohamed, yeye anasema vitendo vya ubakaji na udhalilishaji, vimekuwa vikishika kasi kubwa na kuwaathiri watoto kisaikolojia.

Lakini Mratibu wa shirika Action Aid Pemba, Omar Ali Salum, aliitaka jamii kuacha tabia ya kusuluhishana wenyewe kwa wenyewe, pale zinapotokea kesi hizo na badala yake kuzifikisha kwenye vyombo vya sheria.

Naibu Katibu Mkuu wziara inayoshughulikia wanawake na watoto Zanzibar Mauwa Makame Rajab, ansema wazo la wanaharakati la kutiaka serikali inunue mashine hiyo ni jambo jema, na sasa hilo linatarajiwa kufanyika.

‘’Unajua kuwa zipo kesi nyingi mapaka waathirika wanakata tamaa za watoto wetu kupewa ujauzito, sasa ni kweli Serikali ifanya hima kuwepo kwa mashine hiyo’’,alifafanua.

Tokea mwaka 2011 hadi mwezi mwaka 2017 Dawati la Polisi mkoa wa Kusini Pemba lilipokea kesi 10 za mimba, kwa ajili ya kupatiwa kipimo vya ‘DNA’ na hadi mwaka 2014 ni mbili zilizorudi na nyengine zikiwa foleni kusubiria kipimo hicho.

Mambo hayo ni tofauti kwa jamii ya leo, na ndio maana wapo watoto wa kike 196, kati yao 122 wameripotiwa kupewa ujauzito na 74 kuolewa wakiwa chini ya umri wa miaka 18.

Idadi hiyo ni ile kuanzia mwezi Januari mwaka 2012 hadi mwezi Disemba mwaka 2016, tena hali hiyo ni kwa wilaya za Chakechake na Mkoni pekee.

Uchunguzi ukabaini kuwa, kwa mwaka 2012 pekee, kesi za mimba za utotoni zilikuwa 73, wakati kipindi cha mwezi Januari hadi disemba 2014, ziliripotiwa kesi 49 za mimba kwa wanafunzi.

Kesi za ndoa kwa wanafunzi, kulikuwa na idadi ya 54, kwa mwaka 2012 na mwaka 2016 kuliripotiwa kesi 20 katika taasisi mbali mbali.

Wizara ya elimu pekee ilikusanya jumla ya kesi 67 za mimba na ndoa, ambapo kati ya hizo, mwaka 2012 kesi za ndoa zilikuwa 38, wakati kesi za mimba kwa wanafunzi zilikuwa 14, wakati mwaka huu kumesharipotiwa kesi 9 za ndoa na 6 za mimba.

Vyanzo mbali mbali vya habari, vilisema chanzo cha kujitokeza kwa matendo hayo husababishwa na mambo kadhaa, ikiwa ni pamoja na ukosefu wa mashine ya DNA Zanzibar.

Sheha wa shehia ya Madungu wilaya ya Chakechake, Mafunda Hamad Rubea, aliweka wazi kuwa, kwa kama Serikali ikinunua mashine yake, sasa watoto wa kike watapata haki zao kwenye kesi za mimba na ubakaji.

Mrajisi wa Elimu Zanzibar Siajabu Suleiman Pandu, anasema ukosefu wa mashine ya ‘DNA’ kwa Zanzibar ndio kikwazo pekee, maana mtoto wa kike huathirika mara mbili na wa kiume mara moja.

“Mtoto wa kike kwanza kesi yake huchelewa maana hata samapuli ya vina saba ikija, mwenzake ameshasahu machungu yeye bado, sasa lazima tuwe na yetu Zanzibar’’,alisema.

Shirika la Kimataifala Kuchangia Maendeleo ya Mtoto, limeeleza kuwa, wasichana zaidi ya milioni 14 huolewa wakiwa na umri chini ya miaka 18, katika nchi za kusini mwa jangwa la sahara, nchi za Chad, Niger na Mali zinaongoza.

Azimio la Umoja wa Mataifa la kupunguza aina zote za udhalilishaji kwa wanawake (CEDAW) haliruhusu watoto wenye umri wa chini ya miaka 18 kuolewa.

Azimio la Haki za Binaadamu (the 1948 UDHR) linasema kwamba ndoa yoyote nilazima iwe ni ya maridhiano na kwamba mtoto mwenye umri chini ya miaka 18 huwa hana maamuzi huru.

Kila mwaka, watoto milioni 7.3 wa kike chini ya umri wa miaka 18 hushika na kujifungua mimba, imesema ripoti mpya kuhusu hali ya idadi ya watu mwaka 2013, ambayo imetolewa na Shirika la Mfuko wa Idadi ya Watu katika Umoja wa Mataifa, UNFPA.

Ripoti hiyo imesema, milioni 2 kati ya watoto hao wana umri usozidi miaka 14, na kwamba watoto hao hukumbana na matatizo ya muda mrefu ya kiafya na kijamii kutokana na mimba hizo, yakiwemo vifo vinavyohusiana na uzazi.

Katika kukuza kampeni dhidi ya mimba za utotoni, na unyanyasaji kwa watoto, UNFPA nchini Tanzania, limeshiriki katika mashindano ya riadha ya Kilimanjaro Marathon nchini humo.

Hata hivyo aliekuwahi kuwa Naibu Waziri wa Afya, Dk. Sira Ubwa Mamboya mwezi Julai mwaka 2011, alisema Serikali ina mpango wa kununua mashine ya ‘DNA’ kutokana na umuhimu wake.

Alibainisha kuwa Serikali imeshafanya upembuzi yakinifu kwa kushirikiana na ofisi ya maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano Tanzania, pamoja na kutayarisha jengo la Mkemia Mkuu kwa ajili ya kuweka mashine hiyo.

Aidha alisema DNA ni mashine ya kupima uasilia pale panapotokezea utata wa mtoto, kipimo hicho hufanyika baada ya kuzaliwa mtoto na kuthibitisha nani baba halisi.

Sasa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hivi karibuni kupitia waziri wake katika afisi ya Makamu wa pili wa rais Zanzibar Mohamed Aboud Mohamed, amesema tayari serikali imeshatenga shilingi bilioni 1 kwa ajili ya ununuzi wa mashine hiyo.

“Sasa serikali imeshatenga bilioni 1 kutoka kwenye fungu la Mkemia mkuu wa serikali kwenye mwaka huu wa fedha wa 2017/2018 kwa ajili ua kununua mashine ya DNA”,anabainisha.

Jengine linalotarajiwa kufanywa sambamba ni serikali imeshatenga shilingi milioni 175 kwa ajili ya matumizi ya shughuli mbali mbali za mapambano ikiwemo kuwaelimisha wananchi.

1 comment :

  1. World Best Forex Signals service provider is UsaForexSignal. 100 % Profitable forex signals service provider.

    ReplyDelete