dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Monday, June 17, 2013

Nani anafadhili ugaidi nchini?

NA WAANDISHI WETU

17th June 2013


  Mbowe asema walilenga kumuua na Lema
  Nassari ashambuliwa, ajeruhiwa, alazwa
  Polisi waendelea kuunda timu za makachero
Waziri wa mambo ya ndani ya nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi akipewa maelezo na daktari wa hospital ya Selian juu ya mtoto aliyejeruhiwa katika bomu lililorushwa kwenye mkutano wa kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani wa chadema juzi.
Matukio ya ugaidi yanazidi kutikisa nchi, huku hofu kubwa ikitanda miongoni mwa jamii kwa kuwa juhudi za kuwasaka wahusika hazionyeshi kuzaa matunda na wala umma hauelezwi taarifa zozote juu ya uchunguzi wake.

Ugaidi uliofanywa dhidi ya mkutano wa kufunga kampeni za udiwani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), jijini Arusha juzi ni limetokea takribani siku 40 tu baada tukio jingine lilinalofanana nalo kwa kila kitu, kutokea kwenye hafla ya uzinduzi wa Parokia ya Olasiti ya kanisa Katoliki Mei 5, mwaka huu jijini Arusha pia.

Katika shambulizi la kanisani, bomu lilirushwa kwenye mkusanyiko mkubwa wa waumini nia ikiwa ni kuangamiza watu wengi, hata hivyo walikufa watu watatu na kujeruhi wengine zaidi ya 60.

Ingawa hadi sasa polisi hawajatoa taarifa kwa umma juu ya aina ya bomu lililolotumika Olasit, mlipuko wa juzi kwenye mkutano wa Chadema, unafanana kwa kila kitu na ule wa Mei 5, mwaka huu.

Wakati Olsasit walengwa wakuu alikuwa Balozi wa Vatican na Mwakilishi wa Papa nchini Tanzania, Askofu Mkuu Francisco Montecillo Padilla na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Arusha, Josephat Lebulu, juzi walengwa walitaka kuwaua pamoja na watu wengine  Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema.
Mfululizo wa matukio haya ya ugaidi mbali ya kuasababisha kuahirishwa kwa uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata nne jijini Arusha, pia umekifanya Chadema kusitisha mahudhurio ya wabunge wake wote katika vikao vya Bunge kuanzia leo na kwamba wanatakiwa kwenda Arusha kwa ajili ya shughuli za maziko ya watu wawili waliouawa katika mlipuko wa bomu uliotokea juzi jijini Arusha.

Watu hao na wengine 68 walijeruhiwa katika mkutano wa hadhara wa kuhitimisha kampeni za uchaguzi ndogo wa udiwani katika kata nne.

Msimamo wa Chadema ulitangazwa na Mbowe kwa waandishi wa habari jijini Arusha.

Aidha, alisema kuwa tukio la ulipuaji wa bumu na kufyatua risasi kwa kutumia bunduki aina ya SMG na bastola halikuwa tukio la bahati mbaya, bali lilipangwa kwa lengo la kuwaua yeye na Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema.

Mbowe alisema salama yake na Lema ni uamuzi wao wa kushuka jukwaani saa 11.43 tofauti na mikutano yao yote hushuka jukwaani saa 12:00 juoni  au baada ya muda huo.

Alisema kuwa katika eneo la tukio yaliokotwa maganda ya risasi za SMG na ya bastola kuongeza kuwa nyingine zilipasua tenki la mafuta la gari la mtangazo, ambalo walikuwa wakitumia kama jukwaa lao.

“Hawa watu walikuwa wamesimama kati kati ya watu maeneo tofauti, baada ya bomu kurushwa, risasi zikaanza kupigwa kuelekea jukwaani ila kwa kuwa watu walikuwa wengi bahati mbaya hazikuwapata,” alisema.

Alisema kuwa marehemu waliofariki mmoja wao ni kiongozi wao wa chama ni mkazi wa Kilimanjaro na mwingine mkazi wa Tabora na wote watasafirishwa kwenda kuzikwa  kwao na wao kama chama watashiriki hatua zote ikiwa ni pamoja na kuangalia hali za majeruhi.

Aidha, alisema kuanzia leo chama kitaweka turubai kwenye uwanja wa Soweto ambako mlipuko wa bomu ulitokea na miili yote ya marehemu wataiaga katika uwanja huo.

“Lakini kama chama tunachoona ni kuwa hawa wenzetu (CCM) mchezo wa  siasa halali umewashinda. Kuliko kuwa hivi ni bora watangaze kufuta mfumo wa vyama vingi tujue moja kuliko kuumiza watu,” alisema.

Mbowe alisema kuwa kuanzia sasa Watanzania watambuwe kuwa nchi imeingia katika siasa chafu na zisizo halali. “Kwa sababu tukio hilo la
kisiasa na limepangwa kisiasa kwa kushirikiana na vyombo vya dola,” alisema.

NASSARI ASHAMBULIWA, AJERUHIWA
Alisema Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari, ambaye alikuwa Meneja kampeni wa uchaguzi mdogo wa kata ya Makuyuni, alipigwa vibaya na makada wa CCM na kumuumiza vibaya kwamba na hali yake siyo nzuri, hivyo amelazwa katika Hospitali ya Selian.

Habari za uhakika kutoka eneo la ukio Makuyuni, inadaiwa mbunge huyo alipigwa na vijana wa Kimasai.
Hata hivyo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, hakupatikana kutoa ufafanuzi kutokana na siku yake kuita bila majibu.

HUZUNI, VILIO VYATAWALA 
Mfululizo wa matukio ya mabomu yanayotokea katika Mkoa wa Arusha kumezua hofu kwa wakazi wa mji huo ambao sasa wameanza kuogopa kukaa katika makundi.

Tukio la kwanza la bomu kulipuka katika mkusanyiko wa watu lilitokea Mei 5, mwaka huu katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasit mjini Arusha na kuua watu watatu na wengine zaidi ya 60 kujeruhiwa.

Tukio la pili limetokea juzi katika mkutano wa Chadema kufunga kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata nne za jijini Arusha.

Kutokana na tukio hilo, hali ya huzuni na vilio ilitawala miongoni mwa wakazi wake huku baadhi yao wakisema kurushwa kwa bomu hilo, ni hujuma ya kupunguza wapiga kura wa Chadema katika uchaguzi uliotarajiwa kufanyika jana.

Kata zilizotakiwa kufanya uchaguzi ni Themi, Kaloleni, Kimandolu na Elerai.
Jana vilio vilitawala kwenye viwanja vya Soweto, Hospitali za  Manispaa ya Arusha ambazo majeruhi walipelekwa kwa ajili ya matibabu.

Katika Hospitali za Mount Meru, St .Elizabeth na Selian inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) kulikuwa na makundi makubwa ya watu walioonekana kuwa na simanzi.

Juzi juoni baada ya bomu hilo kurushwa, magari ya maji ya kuwasha na magari mengi ya Polisi yalionekana yakiwa yamesimama kituo kikubwa cha Polisi huku baadhi ya askari waliokuwa na mabomu wakitembea katika baadhi
ya maeneo na kuweka ulinzi mkali kwenye hospitali walizolazwa majeruhi.

NCHIMBI: HALIKUBALIKI
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, amesema tukio hilo halikubaliki na siyo la kibinadamu kwa kuwa linaashiria kuvuruga amani.

Alitoa kauli hiyo jana alipotembelea na kujionea eneo la tukio na waathirika waliolazwa katika hospitali kadhaa jijini Arusha.

NYONGEZA KWA NASARI

Akizungumza na NIPASHE akiwa amelala hospitalini, Nassari,  alisema anamshukuru Mungu kutokana na waliomshambulia kushindwa kutimiza lengo lao la kumuua.

Alisema kuwa alishambuliwa na kujeruhiwa katika eneo la kwapa na kwamba waliomshambulia pia walimchania nguo.

WALIOUAWA WATAJWA
Watu wawili waliokufa katika tukio hilo ni Katibu wa Chadema Kata ya Sokoni One ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha) wa kata hiyo,  Judith  Moshi  (25).

Mwingine ni mtoto aliyejulikana jina moja la Jastin anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka (13).

Aidha, watu 56 wamejeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za miili yao yakiwamo macho, miguu  na kiunoni na kulazwa na idadi yao kwenye mabano, katika Hospitali ya Mount Meru (9),  Selian  (40) na Hospitali ya St. Elizabeth (7).

Majeruhi waliolazwa katika Hospitali ya Mkoa Mount Meru na umri wao kwenye mabano ni Bakari Adam (11), Amiri Ally (9), Sharifa Jumanne (9), Masid Msuya, Labah Israel, Joseph Anthony, Fortin Joseph, Asafi  Shakadem na Ben Mganga.

Majeruhi waliopo Hospitali ya St. Elizabeth  inayomilikiwa na Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Arusha ni Emmanuel Lucas, Raphael Mohamed, Bakari Yuda, Sarah John, Abraham Samweli, Naomi  Cosmas na Peter Thadei.

Waliolazwa katika Hospitali ya Selian ni Daud Laizer,Vick Minja,Yusuph Mlonge, Silvester Jacalando, Godwin Lema, Ibrahim Salum, Hazra Kwire, Renatha Kessy na Fahad Jamal (7) ambaye amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).

KAULI YA MKUU WA MKOA
Mkuu wa Mkoa Arusha, Magesa Mulongo, jana alitembelea wagonjwa katika hospitali hizo.
Mulongo akiwa katika Hospitali ya Mkoa Mount Meru alikataa ombi la wazazi wa mgonjwa Sharif Jumanne (9), waliotaka kumhamishia Hospitali ya Selian kwa maelezo kuwa atapatiwa huduma zote.

Aidha aliagiza Amiri Ally (9) aliyelazwa Mount Meru kuhamishiwa Aga Khan, lakini kabla ya kupelekwa huko alihamishiwa Hospitali ya Selian kwa ajili ya uchunguzi maalum wa kichwa kilichopata majeraha makubwa.

Mulongo alisema hadi kufikia jana jioni majeruhi waliobakia wodini ni 56 katika hospitali tatu na wanaendelea na matibabu.

Alisema tukio hilo limemsikitisha sana na wahusika lazima watafutwe kokote waliko kwa kuwa tukio hilo linafedhehesha Tanzania na Arusha.

“Bomu hili linafanana kabisa na lile lililorushwa kanisani , sasa hatuwezi kuvumilia na kuona watu hawa wanaendelea kuwepo, lazima tuwatafute na Mungu atasaidia tu tuwapate, maana hapendi kuona watu wake wanateseka bila sababu,” alisema.

Mulongo alisema kuwa tangu kuanza kwa kampeni za uchaguzi mdogo hali ya usalama ikiwa nzuri na vvama vilikuwa vikinadi sera zao, hivyo imeshangaza kuona kampeni zinahitimishwa katika hali ya majonzi makubwa.

“Wananchi mvumilie serikali yenu wakati huu mgumu inapowatafuta wahalifu hawa, muwape ushirikiano na hata mkiona tumekamata watu  msitaharuki, lengo ni kupata ukweli na sasa tayari kuna watu tumewakamata kwa mahojiano,” alisema.

Mulongo alisema kwa sasa maneno ni mengi, lakini viachiwe vyombo vya dola kwa sababu hakuna sababu ya kusema bomu hilo lilirushwa kwa lengo fulani kwa kuwa waliokuwapo wafuasi wa vyama mbalimbali.

Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Selian, Dk. Paul Kisanga, alisema majeruhi wanne kati ya  40 hali zo ni mbaya na kuwa Fahad Jamal (7) alitarajiwa kuhamishiwa KCMC, lakini ilishindikana kutokana na kupumua kwa msaada wa mashine.

MBOWE, LEMA WATEMBELEA MAJERUHI

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, alitembelea majeruhi hao, huku akiongozana na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema.

Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo, ambao hawakutaka kutaja majina yao, walisema kuwa baada ya bomu kulipuliwa, Mbowe aliangua kilio na kusaidia baadhi ya majeruhi wenye hali mbaya kwa kuwanyanyua na kuwaingiza ndani ya magari kwa ajili ya kuwakimbiza hospitalini.
Walisema hata mtoto Jastin alifia mikononi  mwake, akiwa amemshikilia huku akitokwa na machozi kutokana na tukio hilo baya.

UCHAGUZI WAAHIRISHWA ARUSHA

Tume ya Taifa ya Uchaguzi  (NEC) imesogeza mbele tarehe ya uchaguzi wa udiwani katika kata nne jijini Arusha hadi Juni 30, mwaka huu kutokana na hali ya usalama jijini humo.

Mkurugenzi wa NEC, Julius Mallaba, aliliambia NIPASHE kuwa: “Ni kweli, tuliona kuwa watu wasingeweza kwenda kupiga kura kutokana na kukosekana kwa utulivu uliosababishwa na tukio hilo la kulipuliwa bomu.”

Kwa mujibu wa Malaba uchaguzi huo uliotakiwa kufanyika jana, tume hiyo imeuahirisha hadi Juni 30, mwaka huu.

Baadhi ya kata zitakazoshiriki katika uchaguzi huo ni Kaloleni, Elerai, Kimandolu na Themi.

Mallaba aliwataka wananchi wote katika kata hizo kujitokeza kwa wingi ili kuwachagua watu wanaowataka.

Aliongeza kuwa kama siyo sababu za usalama, uchaguzi huo ungefanyika kama kawaida kwa kwa kuwa kila kitu kilikuwa kimekamilika ikiwa ni pamoja na kufungwa kwa kampeni na kupelekwa kwa vifaa vya uchaguzi.

CUF: NI TUKIO LA KINYAMA 

Chama cha Wananchi (CUF) kimelaani tukio la  kulipuliwa bomu katika mkutano wa hadhara wa kufunga kampeni za Chadema za kuwania udiwani mkoani Arusha, kikiita kuwa ni cha kinyama.

Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, alitoa tamko la chama chake kuhusu kitendo hicho, alipozungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam jana.

“Ni tukio baya, la kinyama, ambalo linapaswa kulaaniwa,” alisema Profesa Lipumba.

Alisema Watanzania wanahitaji kujenga utamaduni wa kuendesha siasa za kistaarabu na za kujenga hoja, hawahitaji siasa za mabomu kwenye mikutano ya hadhara.

Alivitaka vyombo vya dola kufanya uchunguzi wa kina kuhakikisha wahusika wanakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Profesa Lipumba alisema aliyehusika na tukio hilo, ana kosa la kuua, hivyo anapaswa kuchukuliwa hatua kali.

Alisema nia ya watu hao ililenga kuvuruga uchaguzi wa udiwani usifanyike katika kata za eneo hilo.

PENTEKOSTE YANENA

Katibu wa Umoja wa Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT), David Mwasota, alisema tukio hilo ni la kusikitisha na kuitaka serikali iweke wazi kwa kuwa yenyewe ndiyo yenye majibu vinginevyo wananchi wasiokuwa na hatia wataendelea kuuawa.

Alisema mlipuko huo ni wa pili kutokea ndani ya miezi miwili huku serikali ikiwa imekaa kimya bila kuwaeleza wananchi uchunguzi umefikia wapi na kuwafanya kukosa imani na vyombo vya dola.

Aliitaka serikali iwasake wahusika na kuwachukulia hatua.  “Mwenye majibu ni serikali na kama haina majibu basi tutaendelea kuuawa,” alisema Mwasota.

TLS: VYOMBO VYA USALAMA VISEME
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanzania (TLS), Francis Stolla, alisema ni wakati mwafaka vyombo vya dola kuwaeleza wananchi kila kitu kinachoendelea badala ya kuendelea kukaa kimya.

Stolla alisema Jeshi la Polisi linatakiwa kuonyesha jitihada wanazozifanya katika kudhibiti matukio hayo ya kigaidi ili wananchi wawe na amani wanapokuwa katika mikusanyiko.

Alisema serikali kuendelea kukaa kimya badala ya kuwapa wananchi taarifa ni kuwanyima haki ya kupata taarifa.

JK ATUMA SALAMU
Rais Jakaya Kikwete amesema  amepokea kwa mshituko na huzuni kubwa taarifa za shambulio la mlipuko ambalo limesababisha vifo vya watu wawili na majeruhi ya watu kadhaa.

Aidha, ametuma salamu za rambirambi kwa jamaa na ndugu wa wafiwa wote na pia ametuma pole nyingi kwa majeruhi ambao wameumizwa na kujeruhiwa katika tukio hilo aliloliita kuwa ovu na katili.

Vile vile, Rais Kikwete amewatumia salamu za pole viongozi wa Chadema kufuatia tukio hilo la woga mkubwa na pia kuviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuchukua hatua stahiki za kuchunguza kwa haraka, kubaini, kuwakamata na kuwafikisha mbele ya sheria wote waliohusika na tukio hilo, wawe watu wa ndani ya nchi ama nje ya nchi.

Aidha, Rais Kikwete ametoa wito maalum kwa wananchi akisema: “Kwa wananchi wenzangu, Watanzania wenzangu, napenda kutoa wito wa kuviachia vyombo vya ulinzi na usalama kufanya kazi yao vizuri ili tuweze kuwabaini waovu waliofanya kitendo hiki.”

“ Natambua kuwa yatakuwepo maneno mengi na hisia mbali mbali zitakazojaribu kulielezea tukio hilio ovu na katili kwa njia mbali mbali. Nawasihi tujiepushe na kuchukua dhana na hisia zetu au maneno ya watu wengine kuwa ni ukweli wa tukio hili. Tujipe nafasi ya kutafakari vizuri na kufanya uamuzi ulio bora.”

IGP ATUMA MAKAMISHNA

Jeshi la Polisi Makao Makuu kijini Dar es Salaam  limetuma timu ya makamishna wawili kwenda jijini Arusha kuongeza nguvu katika upelelezi.

Mkuu wa Jeshi la Polisi, Said Mwema, alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa Jeshi hilo linalaani tukio hilo ambalo limesababisha watu wawili kupoteza maisha na wengine 68 kujeruhiwa.

Mwema alisema timu hiyo inaongozwa na Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja na Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Kamishna Issaya Mngulu, ambao watashirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama.

“Jeshi la polisi linalaani sana tukio hilo linaloashiria vitendo vya kigaidi ambalo limesababisha vifo na majeruhi kwa watu wasio na hatia pamoja na kujenga hofu miongoni mwa jamii,” alisema Mwema.

Aliongeza kuwa Jeshi hilo linaendelea na operesheni popote nchini kuhakikisha linawasaka na kuwatia mbaroni watu wote waliowezesha, waliofadhili na waliotenda uhalifu huo.

Matukio ya kigaidi yaliyotokea nchini tangu mwaka jana hadi juzi yanazua mashaka kwamba kuna kundi au mtu anayeyafadhili.

Hofu hiyo inatokana na vyombo vya usalama hususani Jeshi la Polisi kila yanapotokea kutangaza haraka kuunda timu za kuchunguza, lakini uchunguzi huo hauleti majibu kuhusu sababu wala kuwabaini waliohusika.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda, Machi 5,  mwaka huu alivamiwa na watu wasiojulikana wakati akirejea nyumbani kwake, Mbezi Juu, jijini Dar es Salaam, ambao walimng’oa meno, kumkata kidole, kumjeruhi kwa kitu kizito kichwani na kumharibu jicho la kushoto.

Baada ya tukio hilo Jeshi la Polisi liliunda timu ya wachunguzi ambayo hadi leo haijatoa taarifa yoyote wala kukamata mtuhumiwa yeyote zaidi ya kila uchao kusema kuwa uchunguzi unaendelea.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka, alitekwa na watu wasiojulikana, ambao walimshambulia, kumjeruhi na kumng'oa kucha katika eneo la Mabwepande, nje ya jiji la Dar es Salaam, Juni 26, mwaka jana.

Jeshi la Polisi lilitangaza kuunda timu ya kuchunguza na kutoa taarifa kwa umma, lakini hadi leo hakuna taarifa iliyotolewa, mbali tu ya kufikishwa mahakamani kwa mtu mmoja ambaye anadaiwa ni raia wa Kenya. Mtuhumiwa huyo alizua utata mkubwa ambao hadi leo umma haujaelezwa kwa kina jinsi alivyohusika kumteka Dk. Ulimboka peke yake.

Padri wa Parokia ya Minara Miwili mjini Zanzibar, marehemu Evarist Mushi, aliuawa kwa kupigwa risasi, Februari 17, mwaka huu.

Tukio hilo pia lililishtua Jeshi la Polisi na kupeleka timu ya makachero kutoka kwenda kusaidiana na wenzao wa Zanzibar. Vile vile, serikali iliwaleta makachero wa FBI kutoka Marekani, lakini hadi leo Jeshi la Polisi halijatoa taarifa kwa umma zaidi ya kumkamata mtu mmoja na kumfungulia mashitaka, baada ya kushinikizwa na kauli za viongozi wa dini akiwamo Askofu mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycap Kardinali Pengo.

Padri wa Kanisa Katoliki la Mpendae, mjini Zanzibar, Ambros Mkenda, alijeruhiwa kwa risasi na watu wasiojulikana, nje ya nyumba yake, wakati akitoka kanisani, Desemba 25, mwaka jana. Hadi leo Keshi la Polisi halijamkamata mtuhumiwa yeyote.

Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhili Soraga, alimwagiwa tindikali wakati akitoka kufanya mazoezi, kwenye uwanja wa mpira, eneo la Mwanakwerekwe, mjini Zanzibar, Novemba 6, mwaka jana. Hadi sasa hakuna mtuhumiwa aliyekamatwa.

Katika ugaidi dhidi ya parokia  ya Olesiti, licha polisi kutangaza kuunda timu ya makachero wakiwamo wa FBI, lakini imeshindikana kuwapata wahusika zaidi ya kuendelea kumshikilia kijana mmoja mwendesha bodaboda wa jijini Arusha na wengine kuachiwa. Kijana huyo amefikishwa mahakamani.

Kutokea kwa matukio hayo bila vyombo vya usalama kuyachunguza, kuficha taarifa za uchunguzi na kutowafikisha wahusika mahakamani kutaendelea kuwafanya watu waamini kuwa kuna watu wazito wanaofadhili vitendo hivyo vya ugaidi.

Imeaandikwa na Cynthia Mwilolezi, Charles Ole Ngereza, Arusha; Jimmy Mfuru, Rehema Kilagwa, Isaya Kisimbilu na Muhimu Said , Dar.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments :

Post a Comment