NA MWANDISHI WETU
18th November 2013
Mkurugenzi Mkuu wa EPZA, Dk. Adelhelm Meru, alikabidhi leseni hizo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na kusema kuwa hatua hiyo ni uthibitisho wa nia ya mamlaka yake kuendeleza sekta ya viwanda hapa nchini.
“Kuendeleza sekta ya viwanda ni moja ya ajenda kuu ya mamlaka yetu,” aliwaambia waandishi wa habari baada ya kukabidhi leseni hizo.
Kampuni zilizokabidhiwa leseni na EPZ ni Kokoa Kamili Ltd, Rift Valley Tea Ltd, Mambo Coffee Ltd, Sheikh Motors Ltd, Afriweld Industries Ltd na Tanzania Macenta Co Ltd.
Kampuni hizo zimejikita katika kuendesha viwanda vya kuongeza thamani mazao na vitu mbalimbali hapa nchini.
Kati ya kampuni hizo sita, mbili ni za wawekezaji toka Uingereza na Marekani wakati mbili nyingine ni za ubia kati ya Watanzania na wawekezaji wenzao toka nchi za Ukraine na India.
Kampuni mbili zilizobaki zinamilikiwa kwa asilimia 100 na wawekezaji wazawa.
Jumla ya uwekezaji uliofanywa na kampuni hizo ni Dola za Marekani milioni 17 na zinatarajiwa kuzalisha ajira mpya zaidi ya 700.
Pia, thamani ya mauzo ya nje ya kampuni hizo kwa mwaka yanatarajiwa kufikia zaidi ya Dola za Marekani milioni 23 kwa mwaka.
Dk. Meru alisisitiza kuwa nchi zote zilizopata maendeleo zilifanya jitihada kuwekeza katika viwanda na kwamba ni muhimu pia Tanzania ifuate mkondo huo.
Alisema kwa sasa Tanzania inapata hasara kwa kiwango cha juu kutokana na kuuza mali ghafi badala ya bidhaa zilizoongezwa thamani na kwamba hali hiyo inatakiwa kurekebishwa haraka.
Mkurugezi wa Mambo Coffee Co. Ltd, Athanasio Massenha, alisema walihamasika kuomba leseni ya EPZ baada ya kugundua vivutio vya uwekezaji vinavyotolewa na mamlaka hiyo kwa wawekezaji.
Kwa upande wake, Meneja wa Utawala na Masoko wa Rift Valley Tea Solutions Ltd, Dilip Rughani, alisema leseni hiyo itawawezesha kuwa washindani wazuri katika eneo la Afrika.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment