Vigogo hao, wamejinadi katika uchaguzi wa kura za maoni ndani ya CCM unaondelea katika mikoa mbalimbali nchini ili wachaguliwe kugombea ubunge katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika nchini Oktoba 25, mwaka huu.
LEONIDAS GAMA
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, amesema mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Pombe Magufuli anastahili kuchaguliwa ili kuwaletea Watanzania maisha mazuri kutokana na uwezo wake.
Gama aliyasema hayo juzi kwenye mikutano ya kampeni ya kuwania ubunge ndani ya chama hicho katika Jimbo la Songea Mjini iliyofanyika kata za Mwengemshindo na Ruhuwiko.
Alisema ni vema wananchi na wanancha CCM wakamchagua Magufuli kuwa Rais wa serikali ya awamu ya tano katika uchaguzi mkuu utakaofanyika nchini Oktoba 25, mwaka huu.
Alisema kada huyo ambaye ni Waziri wa Ujenzi amefanya kazi kubwa nchini ya kuhakikisha kuwa barabara zinajengwa kwa kiwango cha lami na kupitika kwa wakati wote. Gama ambaye ni kati ya makada wanane wa wanaowania ubunge wa jimbo hilo ndani ya CCM, aliwaangukia wakazi wa Songea Mjini kwa kuwaomba wamchague kuwa mbunge wao na madiwani wa CCM ili washirikiane kuleta maendeleo kwenye maeneo yao.
Alisema endapo wakimchagua katika uchaguzi huo, atafanya kazi kama tingatinga linavyotengeneza barabara na madiwani wa CCM watakuwa sawa na mitambo ya kusindilia.
"Siku ya uchaguzi kura ya kwanza wananchi mumpe Magufuli kuwa rais, mimi (Gama) mbunge na madiwani wa CCM," alisema.
ERICK MAPUNDA
Kwa upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Ufundi Mbeya, Erick Mapunda, aliwaomba wakazi wa jimbo hilo wamchague kuwa mbunge kwa sababu amerudi kuwaletea maendeleo, kutatua na migogoro ya ardhi na kuhakisha baadhi ya wakazi wa Mwengemshindo wanalipwa fidia kupisha ujenzi wa viwanda.
DC HANANG'
Naye Mkuu wa Wilaya ya Hanang' mkoani Arusha, Peter Miti, aliwaomba wakazi wa jimbo hilo kuwachagua kuwa mbunge wao na kuahidi wakulima wa mahindi kuwatafutia soko ili kuwadhibiti walanguzi.
THERESA UVIZA
Vilevile; Mbunge wa Viti Maalum kupitia Vyuo Vikuu, Dk. Theresa Uviza ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mazingira), alisema endapo wananchi watampa ridhaa ya kuwa mbunge wao, watapata manufaa zaidi kwa kuwa mianya ya kupata misaada anaijua.
KATIBU CCM
Pia; Katibu wa CCM wa Wilaya ya Namtumbo, Azizi Mohamed Fakil, alisema endapo atachaguliwa kuwa mbunge wa jimbo hilo, atakarabati ofisi zote za chama hicho za matawi na kata ambazo majengo yake yako katika hali mbaya.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment