Akizungumza na NIPASHE mjini hapa jana, Mtaturu alisema ni heri kubaki na wanachama wachache wanaokipenda na wenye kuamini kwa moyo wa dhati itikadi ya chama hicho kuliko kuwa na wengi wasio na msimamo.
“CCM ni chama kinachoongozwa kwa kanuni na maadili na zaidi kina itikadi yake, mwanachama yeyote anayekiuka maadili hafai, hilo ni kosa kubwa kuliko yote ndani ya chama chetu…wanaohama wanajihami kwani wanafahamu hawana sifa ya kupata uongozi kwa kuvunja maadili,” alisema Mtaturu.
Mtaturu alisema CCM mkoani Mwanza haitarudia makosa yaliyofanyika katika uchaguzi mkuu uliopita hadi kupoteza majimbo ya Nyamagana, Ukerewe na Ilemela kwani wapinzani wamekuwa na tabia ya kuvizia makosa ya chama hicho ili washinde badala ya kutegemea nguvu zake yenyewe.“Mkoa wa Mwanza una majimbo tisa ya uchaguzi, kati ya majimbo hayo CCM ilishinda sita lakini tumejipanga kuyarudisha matatu yaliyoenda upinzani 2010,” alisema.
Katibu huyo wa CCM mkoa wa Mwanza alisema hayo kufuatia waliokuwa wabunge wawili wa CCM wa majimbo ya Kahama (James Lembeli) na Esther Bulaya (Viti Maalum- Vijana), kuhamia Chadema na kutambulishwa katika mkutano wa hadhara jijini hapa juzi.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment