dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Monday, September 7, 2015

Kupiga kura dakika moja

Jaji Damian Lubuva

By Mwandishi Wetu, Mwananchi
Dar es Salaam. Ikiwa zimebaki siku 47 kabla ya kufanyika Uchaguzi Mkuu, imebainika kuwa kila mtu atatumia wastani wa dakika moja kupiga kura kuchagua diwani, mbunge na rais.
Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Damian Lubuva amesema kila kituo kitakuwa na watu 450 watakaopiga kura kuanzia saa 2.00 asubuhi mpaka saa 10.00 jioni. Hiyo ina maana kwamba, kuanzia saa 2.00 mpaka saa 10.00 jioni ni sawa na saa tisa, ambazo ni sawa na dakika 540.
Kwa sababu kila kituo kitakuwa na watu 450, ina maana kuwa watu hao watatakiwa kupiga kura ndani ya dakika 540 ambazo ni sawa na dakika 1.2 kwa kila mtu.


Kwa mujibu wa NEC, muda huo wa saa 10.00 jioni ni wa kufunga vituo, lakini watu ambao watakuwa katika mistari mpaka wakati huo wataendelea kupiga kura mpaka watakapomalizika. Watu watakaojitokeza kuanzia muda huo hawataruhusiwa kupiga kura.
Kituo kimoja watu 450
Lubuva amefafanua kuwa wakati wa uandikishaji, vilitumika  vituo 37, 848 lakini wakati wa upigaji kura vitaongezeka ili wote waliojiandikisha wapate fursa ya kupiga kura kwa sababu tofauti na uandikishaji, upigaji kura ni kazi ya siku moja tu tena kwa saa zisizozidi tisa.
Alifafanua kuwa ongezeko la vituo hivyo linalenga kuwahudumia Watanzania wote 23,782,558 waliojiandikisha kushiriki uchaguzi wa mwaka huu, akibainisha kuwa kwa mkakati ulioandaliwa, kila kituo kitatakiwa kuhudumia wapigakura wasiozidi 450 kwa saa tisa za siku hiyo, zitakazotumika kuamua mustakabali wa uongozi wa Tanzania kwa miaka mitano ijayo.
“Baada ya kupiga kura na matokeo kubandikwa, litabaki jukumu la mamlaka husika kutangaza mshindi. NEC itatangaza matokeo ya rais, wakati wakurugenzi wa halmashauri watashughulika na matokeo ya ubunge pamoja na udiwani,” alisema Jaji Lubuva.
Ili kuepusha uwezekano wa kuwapo kwa madai ya matokeo kuchezewa, Jaji Lubuva alisisitiza kwamba tume imejipanga vilivyo kumtangaza mshindi ndani ya muda uliopangwa  kisheria.
“Sheria inataka mshindi wa urais atangazwe ndani ya siku saba, baada ya uchaguzi, lakini sisi tumepanga kutangaza matokeo ndani ya siku tatu hadi nne, ili taratibu nyingine ziendelee na wananchi waachane na habari za uchaguzi na kuelekeza nguvu zao kwenye kulijenga taifa kimaendeleo.”
Alitoa wito kwa wananchi  kujitokeza kwa wingi Oktoba 25 ili kila mmoja afanye uamuzi utakaochangia kupatikana kwa viongozi bora.
Upigaji kura utakavyokuwa
Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano wa NEC, Dk Sisti Cariah alisema: “Kila Mtanzania aliyejiandikisha na atakayejitokeza kupiga kura, atapiga kura na kwamba jitihada za kuingiza taarifa za watu wote wanaostahili kwenye kumbukumbu za tume hiyo zinaendelea kabla mpigakura hajakabidhiwa karatasi tatu za kura.
Alisema  kuwa hakuna taarifa itakayopotea kwani zinahifadhiwa eneo maalumu na kwamba hata janga lolote likitokea zitaendelea kuwa salama ili kutoathiri Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
“Tunavyo vituo vitatu vya kutunzia taarifa (data centers). Vimewekwa maeneo tofauti kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa takwimu zimehifadhika hata kama kimoja kati yao kitapata hitilafu itakayosababisha kukosekana kwa kinachohitajika kwa wakati husika. Janga kama moto au mafuriko yakitokea na kuathiri kituo kimoja, viwili vilivyobaki vitatumika,” alisema Dk Cariah wakati wa ziara ya waandishi wa habari kwenye kituo cha hifadhi kilichoko Bohari Kuu ya Serikali.
Waliojiandikisha mara mbili kupiga kura
Dk Cariah alifafanua hata watu 52,078 waliobainika kujiandikisha zaidi ya mara moja, wataruhusiwa kupigakura kwenye kituo kimoja kati ya walivyoenda kujiandikisha na kusisitiza kwamba kila mwananchi mwenye sifa, atashiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Alisema upigaji kura utafanyika kuanzia saa 2.00 asubuhi mpaka saa 10.00 alasiri na kudokeza kwamba muda huo wa mwisho utakapofika, askari polisi atasimama nyuma ya mtu wa mwisho aliyepo kwenye foleni na kwenda naye mpaka atakapopiga kura yake na kuondoka.

No comments :

Post a Comment