Akizungumza na Nipashe jana, mbunge huyo alisema sababu za kutaka mjadala huo kurejeshwa ni kutaka kujua mmiliki halali wa fedha hizo kama ni Kampuni ya Kufua Umeme Tanzania (IPTL) au Umma.
Sababu nyingine, kwa mujibu wa Kubenea, ni kutaka kuchukuliwa hatua dhidi ya wahusika wa sakata hilo ili iwe fundisho kwa wengine.
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) walitakiwa kuchukua hatua ya kumkamata Mkurugenzi Mtendaji PAP, Harbinder Singh Sethi, na kumfikisha mahakamani kwa makosa ya utakatishaji wa fedha.
Kamati ilielekeza serikali kutumia sheria za nchi, kuhakikisha kuwa Sethi anarejesha fedha zote alizochota kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT).Kwa mujibu wa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kuthibitishwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, fedha hizo pia ziligawiwa kwa watu mbalimbali binafsi.
Kamati ilijidhihirishia kuwa fedha iliyotumika sehemu yake ni ya umma iliyochotwa bila huruma wala aibu kutoka BoT, hivyo kamati kutaka mamlaka za uchunguzi kuhakikisha fedha hizo zinarudi Benki Kuu hata ikibidi kwa kufilisi mali za watu wote 97 waliofaidika kwa thamani ya fedha walizopewa na Mkurugenzi Mtendaji wa VIP Engineering and Marketing Limited, James Rugemalira.
Baadhi ya waliofaidika na fedha hizo ni viongozi wa umma ambao wanapaswa kuzingatia Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Na. 13 ya mwaka 1995 ambayo inawataka kutoa taarifa ya zawadi wanazopokea au malipo wanayolipwa ili vyombo vya uchunguzi vifanye uchunguzi.
Kamati hiyo pia ilijiridhisha kwamba suala la Akaunti ya Escrow ni jambo la utakatishaji wa fedha, kama alivyosema Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU alipohojiwa na na Kamati.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment