dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Sunday, January 24, 2016

Membe: Serikali isicheze na wafanyabiashara

Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa , Benard Membe.
Dar es Salaam. Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Serikali iliyopita, Benard Membe amempongeza Rais John Magufuli kwa kasi aliyoanza nayo katika vita dhidi ya ufisadi na kudhibiti mianya ya wakwepa kodi, lakini akamshauri kuwa mwangalifu katika kushughulikia wafanyabiashara.
Membe alisema hayo katika mahojiano maalumu na Mwananchi yaliyofanyika mapema wiki hii kuhusu, mambo mbalimbali yanayoendelea tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani.
Mwanadiplomasia huyo alisema hatua ambazo Rais Magufuli amekuwa akichukua kuwabana wakwepa kodi ni za msingi, lakini lazima alifanye kwa uangalifu mkubwa ili asiwafukuze wawekezaji ambao kimsingi ndiyo wabia wa maendeleo ya taifa.
“Wafanyabiashara ni watu wa ‘kuwahandle’ vizuri na kwa uangalifu mkubwa kwa sababu wao ndiyo gurudumu la maendeleo ya nchi yoyote duniani,” alisema Membe.
“Tunapozungumzia ajira, tunazungumzia wafanyabiashara ambao ndiyo wawekezaji. Sasa ombi langu ni kwamba Serikali isicheze nao.”
Akitumia ishara ya mkono wake wa kulia, Membe alisema: “(Mfanyabiashara) Ni kama ndege ambaye ili uendelee kuwa naye, ni lazima umshikilie hivi, lakini ukiachia vidole ataruka na kwenda kutaga mahali kwingine.”
Alikuwa akijibu swali kuhusu hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa na Serikali kuwabana wafanyabiashara wakubwa ili walipe kodi. Katika hatua hizo, Serikali ilibaini zaidi ya makontena 11,800 na magari 2,019 yalipitishwa bila ya kulipia ushuru bandarini na kusababisha Serikali ipoteze Sh 48.77 bilioni.
Pia, ilibaini kuwa kampuni zinazomiliki bandari kavu zilisababisha upotevu wa makontena 349 na hivyo kusababisha Serikali kukosa kodi ya Sh80 bilioni. Serikali ilichukua hatua kwa kubadilisha watendaji wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Mamlaka ya Mapato (TRA), kuwasimamisha kazi baadhi na wengine kufunguliwa kesi mahakamani.
Katika kikao na wafanyabiashara Desemba 3, 2016, Rais Magufuli pia aliagiza wafanyabiashara ambao hawakulipa kodi, wafanye hivyo ndani ya siku saba kuanzia siku hiyo.
“Ingekuwa mimi sikupi siku tatu wala siku saba kulipa kodi. Nakupa miezi miwili mpaka mitatu ili uweke sawa mahesabu yako kwa sababu kutunza hesabu siyo jambo rahisi na baada ya hapo nitakwambia tuendelee kuijenga nchi pamoja,” alisema Membe, ambaye pia aliomba ridhaa ya CCM ili agombee urais, lakini akaishia kwenye tano bora.
Membe, ambaye alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje kwa miaka tisa, alisema wafanyabiashara wana masikitiko makubwa dhidi ya Serikali na anaona suala hilo litaibuka bungeni kwa kishindo safari hii kwa kuwa wengi hawaridhiki.
Membe alibainisha kuwa moja ya masikitiko ya wafanyabiashara hao ni kupewa notisi ya muda mfupi kulipa kodi wanazodaiwa kukwepa katika uingizaji wa makontena bandarini.
Agusia kilio cha Lowassa
Membe pia aligusia tuhuma alizotoa aliyekuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa kuwa wafanyabiashara waliounga mkono wagombea wa upinzani wananyanyaswa na kuandikiwa kodi kubwa.
“Si dhambi wafanyabiashara kufadhili vyama vya siasa wakati wa uchaguzi. Lakini akishapatikana Rais, Serikali ina wajibu wa kuwakusanya wafanyabiashara wote na kufanya nao kazi ya ujenzi wa Taifa na siyo kuwaburuza,” alisema Membe.
Fukuzafukuza
Kuhusu mwenendo wa kutimua na kusimamisha watumishi wa Serikali walio kwenye maeneo yenye harufu ya ufisadi, Membe alisema, “Ni rahisi kumshughulikia mtu usiyemfahamu, lakini siyo rahisi kumshughulikia unayemfahamu”.
Alifafanua kuwa haitakuwa shida kwa Rais Magufuli kuwashughulikia watendaji aliowakuta serikalini ambao kimsingi hakuwateua, kwa kuwa hawafahamu.
“Kwake kufanya hivyo ni rahisi kwa kuwa pia ni rahisi kuwashughulikia watu usiowajua kuliko watu unaowajua, lakini hebu tuone kama atafanya hivyo pia kwa hao aliowateua mwenyewe,” alisema Membe.
/Mwananchi.

No comments :

Post a Comment