dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Sunday, January 24, 2016

ZEC yatahadharishwa kasoro uchaguzi Zanzibar

Image result for ELECTIONS ZANZIBAR

Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) imeshauriwa kuondoa kasoro zilizojitokeza katika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka jana kabla ya kufanyika kwa uchaguzi wa marudio Machi 20 mwaka huu.

Ushauri huo umetolewa kwa nyakati tofauti na baadhi ya wagombea wa Urais wa Zanzibar, wanasheria na  wananchi walipokuwa wakizungumza na Nipashe Mjini Zanzibar baada ya tume kutangaza rasimi kufanyika kwa uchaguzi huo Machi 20 juzi.

Mgombea wa urais wa Chama cha AFP, Soud Said Soud alisema kuwa ili uchaguzi uwe huru na wa haki lazima kasoro za kiutendaji zilizojitokeza na kusababisha matokeo ya uchaguzi kufutwa zifanyiwe kazi ili kuepusha kujirudia kwa kasoro ikiwemo kuongezeka kura katika masanduku kinyume na idadi ya watu waliosajiliwa kwenye daftari la wapiga kura katika vituo vya uchaguzi.

Alisema hatua hiyo ndiyo njia pekee itakayosadia kufanyika kwa uchaguzi huru na wa haki na kumaliza tatizo la uchaguzi Mkuu wa Zanzibar.

Soud alisema ni lazima kwanza wananchi wote wenye sifa wapate nafasi ya kuhakikisha wanashiriki kupiga kura bila ya kuwepo vikwazo na mazingira ya vitisho.

“Tume ya uchaguzi lazima wasimamie na kuondoa kasoro zilizojitokeza katika kuchaguzi wa Oktoba 25 mwaka jana, kabla ya kufanyika uchaguzi wa marudio Zanzibar," alisema Soud.

"Vitendo vya udaganyifu na mizengwe havikubaliki katika utaratibu wa kupata viongozi waliochaguliwa kidemokrasia na wananchi.”

Mgombea urais wa Zanzibar kupitia chama cha ADC, Hamad Rashid Mohamed, alisema uchaguzi uliofutwa ulitawaliwa na vitendo vya udaganyifu katika vituo vya wapiga kura jambo ambalo linahitaji kuangaliwa na ZEC kabla ya kufanyika uchaguzi mpya.

Hata hivyo, alisema kuwa mfumo mzima wa muundo wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar kikatiba unahitaji kuangaliwa upya kwa kufanyiwa marekebisho ya kikatiba baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu.

Alieleza kuwa marekebisho ya Katiba yaliyofanyika na kuingiza wajumbe wa tume wanaotokana na vyama vya siasa, kumeongeza matatizo mkubwa na kukwamisha utekelezaji wa majukumu ya tume hiyo.

Alisema tatizo la wajumbe wa ZEC kutawaliwa na utashi wa vyama katika utekelezaji wa majukumu yao kumechagia kwa kiasi kikubwa kujitokeza kwa matatizo na kulazimika uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka jana kurudiwa Visiwani humo.

Aidha alisema sheria ya kuzuia maamuzi ya Tume ya Uchaguzi kuhojiwa Mahakamani imepitwa na wakati kwa sababu inawanyima wapiga kura uhuru wa Kikatiba wa kutumia mahakama, sheria zinapovunjwa na tume hiyo.

Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS) Omar Said Shaban alisema kurudiwa kwa uchaguzi Zanzibar sio ufumbuzi wa kumaliza mgogoro wa mkwamo wa uchaguzi Mkuu wa Zanzibar.

Alisema njia pekee ya kumaliza mgogoro wa uchaguzi ni kurudi katika hoja ya msingi ya kufutwa matokeo ya Uchaguzi Mkuu; kuangalia kama uchaguzi huo ulikidhi matakwa ya kisheria na Katiba kabla ya kufutwa matokeo  na Mwenyekiti Jecha Salim Jecha Oktoba 28 mwaka jana.

Waangalizi wa kimataifa kutoka ndani ya Afrika na Ulaya walitangaza kuwa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 ulikuwa huru na wa haki kabla ya kufutwa siku chache baadaye na mwenyekiti wa ZEC, Jecha Salum Jecha.

“Kabla ya Mwenyekiti kutangaza tarehe ya uchaguzi alitakiwa kusema kifungu gani cha Katiba na sheria kimempa uwezo wa kufuta matokeo na kuitisha uchaguzi wa marudio,”alisema Shaban ambaye pia Wakili wa Mahakama kuu ya Zanzibar.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments :

Post a Comment