dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Saturday, January 12, 2013

THE ZANZIBAR REVOLUTION DAY: HUTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR DR ALI MOHD SHEIN KATIKA SHEREHE ZA MAPINDUZI

"Rais
Revolutionaries celebrating the Zanzibar Revolution at Amaan Stadium in Zanzibar on January 12th, 2013.


HUTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR DR ALI MOHD SHEIN KATIKA SHEREHE ZA MAPINDUZI

Written by   //  12/01/2013 
HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA
MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI,
MHESHIMIWA DK. ALI MOHAMED SHEIN,
KATIKA MAADHIMISHO YA SHEREHE ZA
MIAKA 49 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR,
TAREHE 12 JANUARI, 2013
Mheshimiwa Dk. Jakaya Mrisho Kikwete,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dk. Mohamed Gharib Bilal,
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda,
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad,
Makamu wa Kwanza wa Rais, Zanzibar;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi,
Makamu wa Pili wa Rais, Zanzibar;
Mheshimiwa Mzee Ali Hassan Mwinyi,
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dk. Salmin Amour Juma,
Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Dk. Amani Abeid Karume, Rais Mstaafu wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Viongozi Wakuu Wastaafu Mliohudhuria;
Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;
Mheshimiwa Mama Anne Makinda, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar;

Mheshimiwa Othman Chande Mohamed, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

Mheshimiwa Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa;

Mheshimiwa Abdalla Mwinyi, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi;

Waheshimiwa Viongozi wa Serikali na Vyama vya Siasa;
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Assalaam Alaykum,
Naanza kwa kumshukuru Mola wetu Mwenye kustahiki kushukuriwa na viumbe vyote; Aliyetuumba na akatupa uhai. Namshukuru kwa kutupa fadhila ya uwezo wa kukusanyika hapa leo kuadhimisha kilele cha sherehe za Miaka 49 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.
Namuomba Mola wetu awarehemu na kuwapa malazi mema Viongozi wetu wa Mapinduzi waliotutangulia mbele ya haki; awaghufirie makosa yao wazee, ndugu na jamaa zetu wote waliokwishapita. Atujaaliye rehema sisi tulio hai na atupe mafanikio katika mambo yetu yote mema tunayojipangia. Yeye Ndiye Muweza wa kila kitu.
Ndugu Wananchi,
Kwa niaba ya wananchi wa Zanzibar natoa shukurani za dhati kwako Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa kuja kuungana nasi katika sherehe zetu hizi adhimu na muhimu. Vile vile, natoa shukurani kwa viongozi wote, mabalozi, wawakilishi wa mashirika ya Kimataifa na wananchi wote kwa kuhudhuria kwenu kwa wingi katika sherehe hizi.
Ndugu Wananchi,
Leo tunaadhimisha sherehe za miaka 49 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964. Kuweko pamoja nasi, mabalozi na wawakilishi wa Taasisi mbali mbali za Kimataifa kunatupa faraja kubwa. Kuja kwenu, kunatudhihirishia kuwa Mapinduzi yetu yanaheshimika na yanapewa taadhima kubwa ndani na nje ya nchi yetu.
Tunapoisherehekea siku hii hivi leo, ni vyema tukajikumbusha jukumu letu la kuendelea kuyalinda, kuyadumisha na kuyaendeleza kwa vitendo Mapinduzi yetu Matukufu, kwa sababu ndio yaliyowakomboa wanyonge kutokana na dhulma na kutawaliwa na kuwaletea uhuru wa kweli. Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964 yaliyoongozwa na Jemedari, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume yalirudisha utu na heshima na kuondoa aina zote za ubaguzi na yaliweka misingi ya haki na usawa kwa watu wote. Tufahamu kwamba mafanikio yote tuliyoyapata katika kipindi cha miaka 49 na ya miaka ijayo kwenye nyanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa, msingi wake mkubwa ni Mapinduzi ya Januari, 1964.

Leo tunaona fahari kwamba katika kipindi hiki cha maadhimisho ya sherehe za miaka 49, tumezidi kujenga mshikamano na maelewano miongoni mwetu. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba yenye Muundo wa Umoja wa Kitaifa, ambayo hivi sasa imeingia kwenye mwaka wa tatu, imepata mafanikio ya kuridhisha na kutia moyo. Mshikamano wetu umetuwezesha kufanya mambo mengi na kupongezwa na marafiki zetu. Ni muhimu tuendelee kushikamana na kufanya kazi kwa bidii.

Ndugu Wananchi,
Ushirikiano wa Serikali na wananchi umetupa mafanikio mazuri katika kuimarisha uchumi wetu ambao mwenendo wake umeliwezesha Pato la Taifa kufikia T.Shs. 1,198 bilioni mwaka 2011 kutoka T.Shs. 946.8 bilioni mwaka 2010. Vile vile, ukuaji wa uchumi ulitegemewa kufikia asilimia 7.0 mwaka 2012 kutoka asilimia 6.8 mwaka 2011. Kiwango hiki ni kikubwa ikilinganishwa na miaka mitano iliyopita. Mafanikio haya yametokana na kukua kwa sekta ya uvuvi, biashara na ujenzi wa mahoteli na mikahawa.
Ndugu Wananchi,
Kutokana na jitihada mbali mbali ilizozichukua Serikali, katika mwaka 2012, tumeshuhudia kushuka kwa mfumko wa bei kutoka asilimia 20.8 mwezi Disemba 2011 hadi asilimia 4.2 mwezi Novemba 2012. Hili ni jambo la faraja kwani limesaidia kuwapunguzia makali ya maisha wananchi.
Aidha, ukusanyaji wa mapato ya ndani umeongezeka kutoka T.Shs. 181.4 bilioni mwaka wa fedha 2010/2011 na kufikia T.Shs. 212 billioni mwaka 2011/2012. Hili ni ongezeko la asilimia 17. Kuongezeka huko kumetokana na hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kuimarisha usimamizi na udhibiti wa mapato na misamaha ya kodi, juhudi za watendaji wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), mwamko mkubwa wa walipa kodi wetu wa sekta binafsi na kuimarika kwa michango ya taasisi za Serikali.
Wakati huo huo, huduma za benki zimezidi kuimarika katika mwaka 2012, ambapo amana za benki ziliongezeka kutoka T.Shs. 336.4 bilioni, Septemba 2011 na kufikia T.Shs. 365.5 bilioni, Septemba 2012. Hili ni ongezeko la asilimia 8.5. Mikopo ya benki kwa sekta binafsi iliongezeka kutoka T.Shs. 147.5 bilioni mwezi Septemba 2011 na kufikia T.Shs. 150.9 bilioni katika mwezi wa Septemba 2012. Ongezeko hili ni sawa na asilimia 6.4. Hali hii inaashiria kuongezeka kwa shughuli za kijamii, kibiashara na uzalishaji mali wa wananchi na hivyo inasaidia kuinua uchumi wa nchi.
Ndugu Wananchi,
Zao la karafuu linaendelea kuwa muhimu kwa biashara na uchumi wetu. Kwa msimu tunaoendelea nao wa mwaka 2012/2013 hadi kufikia tarehe 8 Januari,2013, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshanunua Tani 775.3 za karafuu kwa Tsh. 9,565.3 milioni ambazo zimelipwa taslimu kwa wakulima. Ununuzi unaendelea vizuri. Hii ni hatua nzuri ya mafanikio. Serikali inaendelea kutekeleza azma yake ya kulinda hadhi ya karafuu zetu na imefikia hatua kubwa ya kutekeleza mkakati wa kuzifanyia utambulisho maalum (branding).
Tunawahimiza wakulima kupanda mikarafuu kwa wingi, kuyatunza mashamba yao na kuachana na tabia ya kuuza karafuu kwa njia ya magendo. Lengo letu ni kuzalisha miche 500,000 kila mwaka na kuendelea kuwapa wakulima bila ya malipo. Kwa msimu wa mwaka 2011/2012, jumla ya miche 522,000 ilioteshwa na kutolewa kwa wakulima.
Ndugu Wananchi,
Serikali inafahamu kuwa mchango wa viwanda katika Pato la Taifa bado ni mdogo ambapo kwa mwaka 2011/2012 ulifikia asilimia 3.9. Hivyo, Serikali inaendelea kujenga mazingira mazuri yatayopelekea kuvifufua na kuvikuza viwanda, hasa vidogo vidogo, ili viweze kutoa mchango katika soko la ajira na kuchangia zaidi katika Pato la Taifa. Miongoni mwa hatua hizo ni kukamilisha mradi wa umeme wa uhakika na kuiimarisha miundombinu ya bandari, uwanja wa ndege na barabara ambayo ni muhimu kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, ili kuchangia katika kuimarisha sekta ya mifugo, uvuvi na kilimo.
Vile vile, Serikali imekua ikichukua hatua mbali mbali za kuwashajihisha wajasiriamali, ili nao watoe mchango wao katika kuendeleza uchumi wetu. Miongoni mwa hatua hizo ni kuwapa mikopo, ili waweze kuanzisha biashara ndogo ndogo. Katika jitihada hizi, masoko ya Jumapili yameanzishwa Unguja na Pemba na yanaimarishwa hatua kwa hatua.
Ndugu Wananchi,
Jitihada zetu za kuwavutia wawekezaji nchini zimekuwa zikizaa matunda. Hata hivyo, kutokana na hali ya uchumi ilivyo ulimwenguni, kasi ya wawekezaji wa nje ilipungua katika mwaka uliopita. Jumla ya miradi 29 ya uwekezaji iliidhinishwa katika mwaka wa fedha 2011/2012. Idadi hii ni sawa na asilimia 58 ya makadirio ya miradi 50 iliyopangwa. Katika kipindi cha miezi sita iliyopita, Julai hadi Disemba, 2012, jumla ya miradi 17 yenye thamani ya US$ 38.86 milioni iliidhinishwa. Miradi hii inakisiwa kutoa ajira zisizopungua 834 kwa wananchi. Pamoja na hali hii, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendeleza juhudi za kuwavutia wawekezaji wa nje zaidi. Vile vile, tunawashajihisha wawekezaji wa ndani wazidishe kasi yao ya uwekezaji kwa kuzitumia fursa na rasilimali zilizopo nchini.
Ndugu Wananchi,

Serikali yetu imeendelea kuimarisha huduma za jamii na kiuchumi kwa kuzingatia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2010/2015 kwa ufanisi, kwenda sambamba na DIRA 2020 na MKUZA II pamoja na Malengo ya Kimataifa ya Milenia. Tathmini ya mapitio ya mipango yetu iliyosimamiwa na Tume yetu ya Mipango na Taarifa ya Utelekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa CCM 2010/2015, zinatoa matumaini ya mafanikio, licha ya kuwepo kwa baadhi ya changamoto ambazo tunaendelea kuzifanyia kazi hatua kwa hatua.


Ndugu Wananchi,
Katika uimarishaji wa sekta za kiuchumi, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukuwa juhudi ili kuona kuwa sekta hizo zinakua na kuchangia katika ustawi wa jamii. Sote tunaelewa kuwa sekta ya Kilimo inaongoza na inategemewa na zaidi ya asilimia 80 ya wananchi. Kwa wastani, inachangia asilimia 23 katika Pato la Taifa na kiasi kikubwa katika mapato ya fedha za kigeni. Kutokana na umuhimu huo, Serikali inaendeleza jitihada mbalimbali za kuimarisha sekta hii ili iwe na tija zaidi kwa wakulima na kuongeza mchango wake katika Pato la Taifa.
Mafunzo mbali mbali yanatolewa kwa wakulima na katika jitihada za kuimarisha huduma zao, Serikali ilinunua matrekta mapya 10 mwaka 2012 na mengine 20 yameagizwa mwaka huu. Vile vile, iliyafanyia matengenezo matrekta 27 ya zamani na mashine 14 za kuvunia mpunga (combine harvesters), zilinunuliwa.
Kadhalika, wakulima wanaendelea kufaidika na ruzuku za pembejeo ambapo Serikali inawafidia kwa kiwango cha asilimia 75 ya bei ya mbolea na huduma za ukulima wa matrekta. Vile vile, inawafidia kwa asilimia 83 ya bei ya mbegu ya mpunga na asilimia 55 kwa bei ya dawa ya kuulia magugu.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na juhudi za kuimarisha miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji maji kwa kufuata Mpango Mkuu wa Kilimo cha Umwagiliaji Maji. Juhudi zinaendelea kuchukuliwa kwa kuhakikisha kuwa jumla ya hekta 8,521 ambazo zinaweza kutumika kwa kilimo cha umwagiliaji maji zinatumika kwa matumizi hayo ipasavyo. Kati ya hizo, hekta 750 zimeshatayarishwa. Vile vile, Serikali ya Jamhuri ya Korea tayari imekubali kushirikiana nasi kuendeleza miundombinu ya umwagiliaji maji katika eneo la hekta zipatazo 2,200 katika mabonde ya Cheju, Kibokwa, Kilombero kwa Unguja na Makwararani na Mlemele kwa upande wa Pemba. Nachukua fursa hii kuishukuru kwa dhati kabisa Serikali ya Jamhuri ya Korea.

Aidha, Serikali yetu inaendeleza juhudi za kuimarisha utafiti wa kilimo kwa mazao ya chakula na mboga mboga katika Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Kizimbani. Kadhalika, Serikali inaendelea kukiimarisha Chuo cha Kilimo kiliopo Kizimbani ili kiendelee kusaidia katika kukiendeleza kilimo nchini.

Ndugu Wananchi,
Kwa kutambua umuhimu wa ardhi, Serikali inaandaa sera mpya ya ardhi pamoja na kuzipitia upya sheria za ardhi ili ziende sambamba na malengo ya MKUZA II ya usajili wa ardhi kwa asilimia 50, ifikapo 2015. Katika mwaka 2012 migogoro ya ardhi ya muda mrefu, pamoja na ule wa Mchangamle-Kizimkazi na Muyuni-Matemwe, imepatiwa ufumbuzi. Vile vile, Serikali imekamilisha utayarishaji wa ramani za kisiwa cha Unguja na Pemba, pamoja na ramani za mipaka ya Mikoa na Wilaya. Hivi sasa Mipango Mikuu ya Miji inatayarishwa.
Katika kipindi hiki, mafanikio makubwa yamepatikana katika suala la uhifadhi wa mazingira kwa kudhibiti uingizwaji wa mifuko ya plastiki nchini na kuhamasisha upandaji wa miti katika sehemu zilizochimbwa mchanga na mawe. Aidha, katika kuhakikisha kuwa suala la mazingira linazingatiwa katika miradi ya kiuchumi na maendeleo, miradi 182 inayohusisha utalii, barabara, mikahawa na mahoteli imekaguliwa na kutolewa taarifa. Kadhalika, Serikali imeendeleza jitihada za uhifadhi wa misitu ya asili na mikoko katika maeneo mbali mbali, ambapo hivi karibuni ilizinduliwa Sensa ya Miti ili kuelewa idadi halisi ya mikarafuu pamoja na miti mingine tuliyonayo.
Natoa wito kwa wananchi kuzingatia sheria na taratibu za matumizi bora ya ardhi na rasilimali nyengine pamoja na uhifadhi wa mazingira.
Ndugu Wananchi,
Kuhusu sekta ya ufugaji, Serikali inafanya juhudi kubwa ya kuwaendeleza wafugaji kupitia programu mbali mbali, ikiwemo Programu ya Kuimarisha Huduma za Mifugo (ASDP-L), yenye kutoa taaluma ya ufugaji bora. Katika mwaka mmoja uliopita, vikundi vipya vya skuli za wafugaji 155 na vikundi vya zamani 180 kwa Unguja na Pemba vilipewa mafunzo. Aidha, wafugaji 3,200 walitembelewa na kupewa ushauri wa kitaalamu. Vile vile, katika kuimarisha huduma za utafiti na utibabu wa wanyama matengenezo makubwa yamefanywa kwenye maabara ya Maruhubi Unguja na ya Chake Chake, Pemba pamoja na kuviimarisha vituo vya mifugo viliopo katika sehemu mbali mbali.
Ndugu Wananchi,
Katika mwaka uliopita, juhudi kadhaa zilichukuliwa katika kuiendeleza sekta ya uvuvi, ambazo zimezaa matunda na kufanya mchango wa Sekta hiyo katika Pato la Taifa kupanda kutoka asilimia 6.1 mwaka 2011 hadi asilimia 6.7 mwaka 2012. Kiwango cha samaki kilichovuliwa kimeongezeka kutoka wastani wa tani 28,759 mwaka 2011 hadi wastani wa tani 30,500 mwaka 2012. Uzalishaji wa zao la mwani pia umeongezeka, kutoka tani 12,529 mwaka 2011 hadi tani 13,844 mwaka 2012.
Tunaendelea kutilia mkazo katika kuwawezesha wavuvi kwa kuwapa mafunzo ya uvuvi bora unaozingatia uhifadhi wa mazingira pamoja na matumizi bora ya vifaa vya kisasa. Mafunzo kwa wavuvi juu ya udhibiti wa mazingira ya baharini yamefanywa kupitia mradi wa MACEMP, pamoja na kuendeleza maeneo ya ukanda wa pwani. Kwa mwaka wa fedha 2011/2012 jumla ya T.Shs. 163.6 millioni zilitolewa kwa ajili ya kuwaendeleza wavuvi Unguja na Pemba. Vile vile, Serikali inaendeleza jitihada za kutafuta wawekezaji katika uvuvi wa bahari kuu pamoja na viwanda vya usarifu wa samaki na mazao ya baharini. Kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, wananchi 56 walipelekwa nchini China kwa mafunzo ya ufugaji samaki, kilimo cha mwani na viumbe wengine wa baharini.
Natoa wito kwa vijana na wavuvi wote nchini kushirikana na Serikali katika kuiendeleza sekta ya uvuvi yenye fursa kubwa ya kukuza soko la ajira. Nawasihi wananchi waendelee kupiga vita vitendo vya uvuvi haramu, ili kazi ya uvuvi iwe endelevu na yenye tija.
Ndugu Wananchi,
Miundombinu ya kiuchumi ni chachu ya maendeleo na inajumuisha barabara, bandari, viwanja vya ndege na umeme. Kutokana na umuhimu huo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na ujenzi wa barabara mbali mbali Unguja na Pemba, zenye jumla ya kilomita 158.2, zikiwemo zile zinazofadhiliwa na MCC, BADEA na OPEC. Tumeshazifanyia uchambuzi yakinifu, usanifu na utayarishaji wa zabuni barabara saba kuu (7) zinazoingia katika mji wa Zanzibar zenye urefu wa kilomita 78.5.
Katika kuimarisha usalama wa usafiri wa barabarani, Serikali ilizindua Kamati ya Wiki ya Usalama Barabarani pamoja na Muongo (decade) wa usalama barabarani na kuwashirikisha wahusika mbali mbali kwa lengo la kuimarisha usalama na kupunguza ajali.
Vile vile, Serikali imeendelea kuimarisha kazi za usimamizi wa usalama wa usafiri wa baharini kwa kuimarisha na kuiendeleza Mamlaka ya Usafiri wa Baharini. Aidha, tumetengeneza Kanuni mbali mbali za kusimamia usalama wa vyombo na udhibiti wa mashirika na taasisi zinazotoa huduma.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, imeendelea na hatua za kuliimarisha Shirika la Meli kwa madhumuni ya kuwapa wananchi wa Zanzibar huduma zilizo bora na salama za usafiri huo na kuwaondolea tatizo la muda mrefu la usafiri wa baharini kati ya visiwa vyetu. Serikali imeamua kununua meli mpya ya abiria na mizigo itakayosafiri baina ya Unguja na Pemba na mwambao wa Afrika Mashariki. Meli hiyo itakuwa na uwezo wa kuchukua abiria 1,200 na tani 200 za mizigo. Mipango ya ununuzi wa meli hio inaendelea vizuri.
Ndugu Wananchi,
Juhudi zetu za kuimarisha bandari ya Malindi zinaendelea kuzaa matunda. Idadi ya mizigo imeongezeka kutoka makontena 39,293 yaliyopokelewa mwaka 2011 hadi kufikia 49,821 mwaka 2012, sawa na ongezeko la asilimia 27. Serikali imeshanunua mashine mbali mbali za kunyanyulia makontena zikiwemo “fork lifts” na krini maalum yenye uwezo wa kunyanyua tani 45 ambazo zinategemewa kuwasili mwezi wa Februari, 2013, kwa lengo la kuongeza ufanisi bandarini. Vile vile, Serikali inaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kuimarisha mazingira ya bandari ya Malindi kwa kujenga majengo ya kupumzikia abiria na kutoa huduma mbali mbali. Ujenzi wa eneo la mraba la mita 1,500 unaendelea na linategemewa kukamilika mwishoni mwa mwezi huu.
Katika hatua ya kuimarisha usafiri wa anga, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na kazi ya kukiimarisha Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume Unguja. Majadiliano yanaendelea kuhusu ujenzi wa jengo jipya la abiria uliokuwa umesitishwa kwa muda kutokana na matatizo ya kiufundi. Tunatarajia kwamba kazi hio itaanza tena hivi karibuni. Kwa upande wa Uwanja wa ndege wa Pemba, kazi za uimarishaji huduma katika kiwanja hicho zinaendelea vizuri.
Ndugu Wananchi,
Katika sekta za miundombinu ya huduma za jamii na kiuchumi, umeme wa uhakika ni jambo la lazima. Jitihada za Serikali za kuimarisha umeme zimefikia hatua nzuri. Tunatarajia kuuzindua rasmi mradi wa Uwekaji wa Laini ya pili ya Umeme wa “Millenium Challenge”, hivi karibuni. Mradi huu wa kuleta umeme kutoka Ras Kiromoni, Tanzania Bara hadi Ras Fumba, Zanzibar una nguvu ya Megawati 100, ambapo mahitaji yetu halisi ni kiasi cha Megawati 50. Hizi ni jitihada za washirika wetu wa maendeleo wa Marekani ambao wameamua kutuunga mkono katika kuitekeleza mipango yetu ya maendeleo. Tunatoa shukurani kwa ushirikiano wao huo.
Ndugu Wananchi,
Tuna furaha kuona kuwa huduma za mawasiliano zikiwemo huduma za simu na mtandao zinaimarika. Mradi wa “e-government” uliogharimu US$ 19.8 milioni umekamilka kwa ufanisi na kuzinduliwa tarehe 5 Januari, 2013. Mradi huu unatuwezesha kuunganisha Ofisi na taasisi za Serikali kwa mitandao yenye nguvu zaidi. Hatua hiyo itaifanya Serikali kuwa na uwezo mkubwa zaidi wa kuendesha shughuli zake na kuwahudumia wananchi pamoja na kuimarisha huduma za mawasiliano ya ndani na nje ya nchi.
Ndugu Wananchi,
Vijana ni nguvu kazi muhimu kwa maendeleo yetu. Upungufu wa ajira kwa vijana ni mongoni mwa changamoto inayoikabili Serikali hivi sasa. Uimarishaji wa uchumi wetu unazingatia mbinu mbali mbali za kuitatua changamoto hii. Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali inaendelea na hatua ya kuwajengea uwezo wajasiriamali kwa kuwapatia mafunzo na mikopo yenye riba nafuu kupitia mifuko mbali mbali ukiwemo Mfuko wa AK/JK. Serikali imetoa mikopo ya jumla ya shilingi bilioni 1.5 kwa wananchi mbali mbali. Wajasiriamali 500 wa Unguja na Pemba wamepatiwa mafunzo ya usimamizi wa fedha, masoko na uongozi. Kadhalika, Vikundi 11 vyenye wanachama 1,526 vimeanzishwa, Unguja na Pemba.
Kwa kushirikiana na taasisi ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia masuala ya wanawake “UN WOMEN”, Serikali ya Mapinduzi inatekeleza Mradi wa Kukuza Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake wenye thamani ya T.Shs. 156 milioni. Kupitia mradi huu, vikundi mbali mbali vya kinamama na wakufunzi vimepatiwa mafunzo.
Serikali imeshafanya utambuzi wa vikundi vya vijana katika wilaya zote kwa ajili ya kuyafahamu mahitaji yao ambapo vikundi 789 vimeorodheshwa na baadhi yao kupatiwa mafunzo ya kitaalamu kwa kupitia programu ya ASSP. Aidha. vikundi vya vijana 58, vinavyojishughulisha na shughuli mbali mbali vimepewa T.Shs. 192.4 milioni kupitia Mfuko wa Vijana wenye thamani ya T.Shs. 300 milioni.
Ndugu Wananchi,
Jitihada zinaendelezwa katika kushughulikia masuala ya watoto ikiwa ni pamoja na kuzilinda na kuziimarisha haki zao za elimu, afya na kuwaepusha na vitendo vya udhalilishaji kijinsia. Sheria ya hifadhi ya mtoto Nambari 6 ya mwaka 2011 imeanzishwa ili kuzipa nguvu sheria zinazolinda haki zao zilizokuwepo kabla. Nawasihi wananchi kuzitumia huduma zinazotolewa katika vituo vya mkono kwa mkono vilivyoendelea kufunguliwa Unguja na Pemba.
Vile vile, Serikali inaendelea na jitihada za kuziimarisha huduma za watu wenye ulemavu. Zoezi la usajili kwa ajili ya kuimarisha huduma na haki zao ikiwemo suala la elimu kwa watoto wenye ulemavu liko katika hatua za mwisho. Vile vile, Serikali imeanzisha mfuko wa kuwasaidia watu wenye ulemavu, uliozinduliwa tarehe 28 Septemba, 2012 na hadi mwezi wa Disemba, 2012 jumla ya T.Shs. 211 milioni zimepatikana.
Kadhalika, Serikali imetekeleza ahadi yake ya kuziimarisha huduma za wazee ikiwa ni pamoja na kuwapatia mahitaji ya chakula kwa ukamilifu, posho, ulinzi na matibabu katika makaazi yao huko Sebleni; ikiwa ni njia bora ya kutathmini michango waliotoa wakati walipokuwa wakiitumikia nchi yetu.
Ndugu Wananchi,
Kuhusu huduma za afya, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika kutekeleza mkakati wa miaka 10 wa kuifanya Hospitali ya Mnazi Mmoja kuwa ya rufaa. Kitengo maalum cha utafiti pamoja na elimu kwa wafanyakazi juu ya njia mbali mbali za kukabiliana na maradhi kimeanzishwa. Huduma za tiba zimeimarika zikiwemo Idara ya meno, upasuaji na kitengo cha ICU. Serikali kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Haukeland cha Norway, imeweka vifaa vya kisasa kwenye wodi ya watoto wachanga wenye umri wa mwezi mmoja.
Ndugu Wananchi,
Upandishaji hadhi wa Hospitali ya Wete na ile ya Abdalla Mzee ya Mkoani kuwa Hospitali za Mkoa, umefikia hatua nzuri. Serikali imeshajenga Maabara mpya kwenye Hospitali ya Wete. Vile vile, jengo jipya kwa ajili ya wagonjwa wa akili limejengwa kwa msaada wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB).
Katika kuzipandisha daraja Hospitali za vijiji (Cottage Hospitals) ili ziwe za Wilaya, Serikali kwa kushirikiana na Shirika lisilokuwa la Kiserikali la Uingereza HIPZ (Health Improvement Project Zanzibar) imefanya kazi kubwa ya kuimarisha huduma katika Hospitali ya Makunduchi. Nyumba za wafanyakazi katika hospitali ya Kivunge nazo zinafanyiwa matengenezo makubwa.

Aidha, Serikali imejenga maabara ya kisasa ya uchunguzi wa maradhi mbali mbali katika hospitali ya cottage ya Micheweni. Maabara hii ilifunguliwa rasmi katika shamra shamra za miaka 49 ya Mapinduzi.

Ndugu Wananchi,
Kadhalika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekamilisha ujenzi wa Bohari Kuu la Dawa eneo la Maruhubi, uliogharamiwa kwa pamoja na Serikali yetu, Shirika la Misaada la Marekani (USAID) na Shirika la Misaada la Denmark (DANIDA) ili kurahisisha uhifadhi na upatikanaji wa uhakika wa dawa nchini. Uzinduzi rasmi wa ghala hii ulifanyika katika maadhimisho ya sherehe za Mapinduzi, tarehe 6 Januari, 2013.
Mapambano dhidi ya Malaria yanaendelezwa kwa kushirikiana na Shirika la “Research Triangle Institute” la Marekani katika baadhi ya maeneo yanayoonekana kutoa idadi kubwa ya wagonjwa. Jumla ya nyumba 121,471 zilipangwa kupigwa dawa katika awamu ya saba, kati ya hizo, nyumba 114,858 (asilimia 95) zilipigwa dawa. Kadhalika, Jumla ya vyandarua 717,000 vyenye dawa viligaiwa kwa wananchi wa Unguja na Pemba ili kukabiliana na malaria.
Kwa upande wa VVU/UKIMWI, hadi mwezi wa Septemba 2012, idadi ya vituo vya upimaji vimeongezeka kutoka vituo 56 mwaka 2011 hadi kufikia vituo 76 mwaka 2012. Idadi ya wagonjwa 6,793 wamesajiliwa na kupatiwa huduma katika mwaka 2012 ikilinganishwa na wagonjwa 5,935, mwaka 2011. Aidha, wagonjwa 3,868 wameanzishiwa dawa za ARVS hadi Septemba 2012, kutoka wagonjwa 3,185 mwaka 2011. Kati ya wagonjwa hao 376 ni watoto.
Ndugu Wananchi,
Hali za afya za baadhi ya wananchi wetu na hasa vijana zinaendelea kuathiriwa kwa matumizi ya dawa za kulevya. Serikali kwa kushirikiana na jumuiya mbali mbali zisizokuwa za Kiserikali inaendelea kuchukuwa hatua za kukabiliana na biashara na matumizi ya dawa hizo kwa kushirikiana na vikundi vya ulinzi shirikishi. Aidha, Serikali kupitia Tume ya Uratibu wa Dawa za Kulevya inaendelea kutoa taaluma kwa umma juu ya athari ya dawa hizo. Napenda kuzipongeza taasisi zote zinazotoa huduma katika nyumba zote wanazoishi vijana walioamua kuacha matumizi ya dawa za kulevya. Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi hizo, ili kwa pamoja tuweze kulipunguza tatizo hilo.
Ndugu Wananchi,
Katika hotuba yangu ya maadhimisho ya sherehe za miaka 48 ya Mapinduzi, nilielezea jitihada za Serikali za kuwapatia wananchi huduma za maji safi na salama kwa mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika. Mkopo huo ni kwa ajili ya mradi wa maji ya vijijini Unguja na Pemba pamoja na Miji ya Pemba. Ni jambo la faraja kwamba wakandarasi watatu tayari wamepatikana kwa miradi hiyo na baadhi ya kazi zilianza tangu mwezi wa Julai, 2012. Kadhalika, katika kukabiliana na tatizo la uhaba wa maji kwenye Mkoa wa Mjini Magharibi. Serikali inaendelea kushirikiana na Serikali ya Japan katika kuendeleza Awamu ya Pili ya Mradi wa Maji wa Mkoa huu.
Katika maadhimisho ya miaka 49 ya Mapinduzi, miradi kadhaa ya maji safi na salama ilifunguliwa katika maeneo ya Fumba, Dunga Bweni na Chaani kwa Unguja; Kojani na mradi wa maji safi na salama wa Chokocho na Michenzani huko Pemba. Ufunguzi wa miradi hio utasaidia sana katika kupunguza tatizo la upatikanaji wa huduma hii kwa wananchi wa Chokocho, Kisiwapanza, Michenzani na Makoongwe.
Ndugu Wananchi,
Kuhusu elimu, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, awamu ya saba, inaendelea kuimarisha ubora wa elimu katika ngazi zote na kuhakikisha kuwa watoto wote waliofikia umri wa kuanza skuli, wanapata fursa hiyo.
Katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, idadi ya skuli za maandalizi zimeongezeka kutoka 244 mwaka 2011 hadi 253 mwaka 2012. Uandikishaji wa watoto wanaoanza darasa la kwanza umeongezeka kutoka watoto 31,146 mwaka 2011 hadi kufikia 34,155 kwa mwaka 2012. Ongezeko hili ni asilimia 9.7. Skuli 13 za msingi za Unguja na Pemba zilifanyiwa matengenezo makubwa na kujengwa madarasa mapya 116.
Ndugu Wananchi,
Katika kuimarisha elimu ya sekondari, skuli nane mpya za sekondari kati ya 21 zilizoanishwa kwenye Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010/2015, zimefunguliwa katika kusherekea miaka 49 ya Mapinduzi. Aidha, ujenzi wa skuli mpya za ghorofa 5 unaendelea vyema katika maeneo ya Kiembesamaki, Mpendae, Kwamtipura na Kibuteni kwa Unguja na Mkanyageni kwa Pemba, ili kutoa nafasi zaidi kwa wanafunzi wanaojiunga na elimu ya sekondari.
Serikali inaendelea na juhudi zake za kuimarisha elimu ya amali ili iweze kusaidia katika kutoa ajira kwa vijana. Jumla ya wanafunzi 336 wanaendelea na mafunzo ya Diploma ya Ufundi katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Karume na vijana 720 wanaendelea kupata mafunzo ya amali katika Vituo vya Mafunzo ya Amali vya Mkokotoni na Mwanakwerekwe viliopo Unguja na Vitongoji, kiliopo Pemba.
Ndugu Wananchi,
Idadi ya wanafunzi wanaojiunga na vyuo vyetu vikuu viliopo hapa Zanzibar imeongezeka kutoka 3,914 mwaka 2011 hadi 4,812 mwaka 2012 kwa vyuo vyote vitatu. Ongezeko hili ni sawa na asilimia 23. Kwa upande wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) idadi ya wanafunzi imeongezeka kutoka 916 mwaka 2011 hadi 1,440 mwaka 2012. Ongezeko hili ni sawa na asilimia 57. Aidha, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeongeza bajeti ya Bodi ya Mikopo kutoka T.Shs. bilioni 4 mwaka 2011 hadi T.Shs. bilioni 8 mwaka 2012, ili kuweza kuwahudumia wanafunzi wengi zaidi.
Ndugu Wananchi,
Kwa upande wa Sekta ya habari, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukua hatua mbali mbali za kuimarisha vyombo vyake vya habari vikiwemo redio, televisheni na magazeti. Ujenzi wa studio za masafa ya kati katika eneo la Bungi umekamilika na tayari umezinduliwa. Aidha, Serikali inakamilisha hatua za kiufundi ili kuweza kuhama kutoka kwenye mfumo wa utangazaji wa analojia na kuingia katika mfumo mpya wa dijitali, mwishoni mwa mwezi Februari mwaka huu. Vile vile, kupitia mfumo mpya matangazo ya televisheni ya ZBC yatatolewa kupitia chanali 38.
Matangazo ya redio na televisheni kupitia Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC) yameimarika kwa ubora wa vipindi na muda wa matangazo umeongezwa hadi kufikia saa 24 kwa siku. Aidha, gazeti la Zanzibar Leo limeimarishwa zaidi na hivi sasa linawafikia wasomaji wengi zaidi wa vijijini na hata Tanzania Bara.
Ndugu Wananchi,
Katika kutekeleza ahadi ya Serikali ya kuwajengea wasanii wetu studio ya kisasa ya kurikodia muziki na michezo ya kuigiza, Serikali imelifanyia matengenezo makubwa jengo la zamani la Sauti ya Unguja liliopo Rahaleo kwa ajili ya kutumiwa na wasanii wetu ili waweze kurikodia kazi zao. Jengo hilo lilizinduliwa tarehe 8 Januari, 2013. Matumaini yangu ni kwamba, kuwepo kwa studio hio kutachangia sana kukuza utamaduni na ajira kwa vijana wetu wenye vipaji mbali mbali.
Vile vile, Serikali imeimarisha shughuli za michezo na utamaduni kupitia matamasha mbali mbali ya sanaa za maonesho na maigizo ambayo yanaendelea kufana kila mwaka. Michezo mbali mbali ikiwemo mpira wa miguu, mpira wa vikapu, riadha pamoja na vikundi vya mazoezi nayo imeimarishwa. Jitihada zinafanywa ili kuirudishia Zanzibar hadhi yake ya michezo na kulirudisha vugu vugu la michezo hasa maskulini. Napenda kuchukua fursa hii kuipongeza timu yetu ya Taifa ya mpira wa miguu “Zanzibar Heroes” kwa kupata ushindi wa tatu katika mashindano ya CECAFA yaliyofanyika Uganda mwezi wa Disemba mwaka jana na katika mashindano ya nchi zisizokuwa wanachama wa FIFA yaliyofanyika nchini Kurdistan. Kadhalika, nazipongeza timu zetu nyengine zilizotuletea ushindi na medali ikiwemo timu ya judo, karati, wanyanyua vitu vizito na timu ya mpira wa mikono ya vijana.
Ndugu Wananchi,
Katika jitihada za kukuza utalii nchini, Serikali imeifanyia mapitio Sheria ya Utalii Namba 6 ya mwaka 2009 na sasa Sheria mpya Namba 7 ya mwaka 2012 inatumika ambayo inakwenda sambamba na dhana ya “Utalii kwa Wote”. Juhudi za kuitangaza Zanzibar zinachukuliwa kwa kuiwezesha Kamisheni ya Utalii kwa kuipa nyenzo na vifaa ili iweze kutekeleza jukumu lake, ili lengo la “Utalii kwa Wote” liweze kufikiwa. Vile vile, Serikali kwa kushirikiana na Jumuiya ya Wawekezaji katika Sekta ya Utalii (ZATI), Jumuiya ya Makampuni ya Watembezaji Watalii (ZATO) pamoja na jumuiya nyengine itaendelea kujenga mazingira bora ya kuuendeleza utalii.

Wananchi wanahamasishwa kutumia vivutio vyetu vya utalii ili kukuza utalii wa ndani. Kwa pamoja tutaendeleza juhudi za kukuza sekta ya utalii kwa kauli mbiu ya “Utalii kwa wote” ili iendelee kuwa na mchango mkubwa zaidi katika soko la ajira, kuingiza fedha za kigeni na katika kukuza Pato la Taifa kwa jumla.

Ndugu Wananchi,
Katika kuimarisha utawala bora, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanzisha Sheria ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi Namba 1 ya mwaka 2012, ambayo itasimamia mapambano dhidi ya rushwa na matumizi mabaya ya mitaji ya umma. Kwa mujibu wa Sheria hiyo, Serikali imeanzisha Mamlaka ya Kupambana na Rushwa Zanzibar na tayari Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo ameshateuliwa. Ni imani ya Serikali kwamba wananchi sote tutashirikiana na Mamlaka hii ili kuhakikisha kuwa suala la rushwa na uhujumu uchumi linapigwa vita na kila mmoja wetu.
Aidha, Serikali inatambua umuhimu wa kuimarisha maslahi bora kwa watumishi wote. Kwa lengo la kutekeleza azma hiyo, Serikali tayari imeandaa Miundo ya Utumishi ya Wizara na Taasisi zake mbali mbali na utekelezaji wake utaanza hivi karibuni. Hatua hii itasaidia kuleta uwiano wa kimaslahi kwa kuzingatia viwango vya elimu na uzoefu wa utumishi kwa wafanyakazi. Serikali itaendelea kuimarisha mishahara na stahili nyengine za wafanyakazi kadri hali ya uchumi itakavyoruhusu, ili iwasaidie katika kuendesha maisha yao. Kadhalika, suala la mafunzo ya watumishi limeendelea kuzingatiwa kwa kukiimarisha Chuo cha Utawala wa Umma kwa kukipatia jengo jipya huko Tunguu, ambalo lilizinduliwa tarehe 5 Januari, 2013.
Ndugu Wananchi,
Katika kuleta mageuzi kwenye mfumo wetu wa kiutawala na kuzipa uwezo zaidi Serikali za Mitaa kufanya shughuli za maendeleo na kufanya uamuzi kulingana na mahitaji yao, Serikali tayari imeandaa Sera ya Serikali za Mitaa. Pamoja na Sera hiyo, mpango wa utekelezaji nao tayari umeshaandaliwa.
Katika kuipa nguvu za kisheria Sera hiyo na utekelezaji wake, Sheria Namba 3 na 4 ya mwaka 1995 na sheria Namba 1 ya mwaka 1998 zimeanza kufanyiwa marekebisho. Kukamilika kwa marekebisho hayo ya sheria kutaongeza kasi ya mageuzi ya Serikali za Mitaa.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya Mapinduzi ya Awamu ya Saba inaendelea na juhudi zake za kuimarisha umoja, mshikamano na maelewano miongoni mwa wananchi; ambayo ndio siri kubwa ya kuendelea kuwepo amani na utulivu yenye kuimarisha maendeleo yetu. Hata hivyo, katika kipindi cha mwaka 2012 kwa nyakati tafauti tulishuhudia vitendo vya vurugu na fujo ambavyo vilidhibitiwa na vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama. Serikali haitovumilia kufanyika kwa vitendo hivyo na itaendelea kuchukua hatua madhubuti kwa mujibu wa sheria kwa watakaofanya vitendo hivyo. Zanzibar iko salama na Inshaallah itaendelea kuwa salama.
Wito wangu kwenu ni kuzidi kuuimarisha umoja na mshikamano wetu ambao umeleta amani na utulivu na mafanikio tuliyoyapata.
Ndugu Wananchi,
Muungano wetu upo imara na katika kipindi chote tangu ulipoasisiwa, nchi yetu imepata heshima kubwa katika Jumuiya ya Kimataifa. Kadhalika, tumepata mafanikio makubwa ya kisiasa, kiuchumi na ustawi wa jamii, ingawa zimekuwepo baadhi ya changamoto ambazo zinaendelea kushughulikiwa hatua kwa hatua. Kamati ya pamoja ya SMT na SMZ inayoongozwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itazipatia ufumbuzi changamoto zilizosalia.
Napenda kukuhakikishieni wananchi wote kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuuendeleza muungano wetu na kuwatumikia wananchi wote.
Ndugu Wananchi,
Kwa niaba yenu nataka nitoe shukurani kwa nchi zote marafiki, washirika wetu wa maendeleo, taasisi na mashirika ya Kimataifa zinazoshirikiana nasi kwenye mipango yetu ya maendeleo. Kadhalika, natoa shukurani zangu tena kwa viongozi wote waliohudhuria hapa wakiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete. Natoa shukurani maalum kwa Makamu wa Kwanza wa Rais, Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad na Makamu wa Pili wa Rais, Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, kwa ushauri wao na kunisaidia katika kuiongoza Zanzibar. Kadhalika, nawashukuru Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Wafanyakazi wote kwa jitihada zao za kuwatumikia wananchi.
Navishukuru tena vikosi vyote vilivyozipamba sherehe zetu na jinsi gwaride lilivyochangamsha uwanja mzima. Aidha, nawashukuru wale wote walioshiriki kwenye maandamano na wale waliotupa burudani ya aina yake ambayo sote tumezifurahia. Kadhalika, natoa shukrani zangu kwa waandishi wa vyombo vya habari kwa kuzitangaza shughuli zetu hizi kwa ufanisi.
Ndugu Wananchi,
Nakamilisha shukurani zangu kwa kukushukuruni sana wananchi nyote wa Zanzibar kwa mambo yafuatayo:-
Kwanza, kwa kushiriki kwa wingi katika kutoa maoni yenu ya kupatikana Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ninakusihini muendelee kushiriki kikamilifu katika hatua zilizobakia, kwa mujibu wa utaratibu utakaopangwa na Tume inayoratibu maoni hayo. Zingatieni amani na utulivu viwepo wakati wote.
Pili, ninakushukuruni kwa kushiriki vizuri na kwa idadi kubwa katika Sensa ya Watu na Makaazi ya tarehe 26 Agosti, 2012. Matokeo ya sensa hii yalitangazwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. Jakaya Mrisho Kikwete hapo tarehe 31 Disemba, 2012. Kutokana na sensa hiyo, idadi ya Watanzania sasa imefikia 44,929,012 na idadi ya watu wa Zanzibar ni 1,303,560. Changamoto iliyo mbele yetu ni kuhakikisha kuwa tunafanya kazi kwa bidii ili uchumi wetu uendelee kukua kwa kasi zaidi ili pasiwe na athari katika upatikanaji wa huduma muhimu.
Tatu, ninakushukuruni kwa kuendelea kushiriki katika kujiandikisha kwa ajili ya vitambulisho vya Taifa. Ninakuhimizeni muendelee kujiandikisha kwa haraka bila ya kuchelewa. Hii ni haki yenu msidanganyike wala msibabaishwe.
Nne, nakushukuruni kwa kuwa pamoja na Serikali zetu mbili pale nchi yetu ilipokumbwa na maafa ya kuzama kwa meli ya M.V. Skagit. Tunamuomba Mwenyezi Mungu aendelee kutupa subira na awape malazi mema ndugu zetu waliofariki katika ajali hiyo.
Tano, ninakushukuruni nyote mliohudhuria hapa na wale ambao kwa sababu mbali mbali hawakuweza kuhudhuria, lakini walikuwa wakifuatilia sherehe hizi kwenye vyombo vya habari.
Napenda niishukuru na niipongeze sana Kamati ya Halmashauri ya Sherehe na Maadhimisho kwa mwaka huu wa 49 wa Mapinduzi inayoongozwa na Makamu wa Pili wa Rais. Mmefanya kazi nzuri na ndio iliyofanikisha sherehe zetu. Hongereni sana. Ninakutakieni wananchi nyote kheri ya Mwaka Mpya wa 2013.
MAPINDUZI DAIMA
MUNGU IBARIKI ZANZIBAR
MUNGU IBARIKI TANZANIA
MUNGU IBARIKI AFRIKA
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
Chanzo: Mzalendo

No comments :

Post a Comment