
Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro, akihojiwa jana na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) alisema jeshi hilo liliwasihi tangu awali viongozi wa CUF kwamba wasifanye maandamano kutokana na kuwapo kwa taarifa kuwa silaha zilizoibwa Ikwiriri zingetumika pengine katika maandamano hayo.
“Tuliwaeleza kuna silaha ambazo zimeibwa Ikwiriri na hatuwezi kujua zitatumika maeneo gani, lakini kuna uwezekano zikawa zimeingia Dar es Salaam, hivyo tukawaambia hizi silaha hatuwezi kujua zitapiga wapi na zitakuwa na madhara gani,” alisema Sirro.Kamanda Sirro alisema sababu nyingine ambayo CUF walielezwa ni kwamba katika mauaji ambayo yalifanyika Pemba pia wapo askari polisi waliouawa, hivyo taarifa ambazo jeshi hilo lilikuwa limezipata ni kwamba maandamano hayo yasingeweza kwisha salama.
Juzi Jeshi la polisi lilitumia nguvu kwa kupiga mabomu na silaha za moto wakati wa kuwakamata wanachama wa CUF waliokuwa wamekusanyika baada ya jeshi hilo kuwazuia wasiandamane kufanya kumbukumbu ya wanachama wa chama hicho waliouawa na Jeshi hilo mwaka 2001.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment