Kikwete ambaye alikuwa nchini humo na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu, Tony Abbot, alirejea nchini jumamosi iliyopita usiku.
Katika mazungumzo yao, Abbot alimpongeza Kikwete kwa kukabidhi madaraka kwa kiongozi mwingine kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania. Kwa mujibu wa Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana, Rais Kikwete pia alikutana na kufanya mazungumzo na mwenyeji wake, Gavana Mkuu wa Australia, Peter Cosgrove.
Kisha alikutana na wawekezaji wakubwa wa Australia ambao walionyesha nia ya kuja kuwekeza nchini.
Katika mazungumzo yao, walijadili namna ya kuendeleza sekta mpya ya gesi nchini na jinsi Tanzania inavyoweza kunufaika kutokana na kupata gesi.
Tayari Serikali ya Australia na kampuni binafsi ya gesi na mafuta, zinaisaidia Tanzania katika vyuo vya ufundi stadi (Veta) na kufanya tafiti za kilimo.
Kikwete alihitimisha ziara yake nchini kwa kutunukiwa digrii ya udaktari wa heshima ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Newcastle, kwa mchango wake katika uongozi kwa kipindi cha miaka 10 ya madaraka yake kwa Tanzania na Dunia.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment