dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Sunday, February 14, 2016

Waafrika wanaosoma India waitwa nyani, sokwe

Balozi wa Tanzania nchini India, John Kijazi akiwa na baadhi ya wanafunzi wa Tanzania wanaosoma nchini humo baada ya kukutana nao huko Bangalore wiki iliyopita. Picha ya maktaba.
By Florence Majani, Mwananchi fmajani@mwananchi.co.tz
Dar es Salaam. Wanafunzi wa Tanzania wanaosoma India wamefunguka na kueleza unyanyasaji na ubaguzi wanaoupata wanapokuwa masomoni nchini humo.
Ikiwa ni siku chache baada ya mwenzao kupigwa na mwingine kuvuliwa nguo huku akilazimishwa kutembea uchi, wanafunzi hao wamesema unyanyasaji wanaofanyiwa hauelezeki.
Inaelezwa kuwa karibu wanafunzi 400 hadi 500 Afrika wanasoma nchini humo, wengi wanatoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Nigeria, Tanzania, Sudan na Rwanda.
New Delhi
Mhariri wa Habari wa Kampuni ya Sahara, Jennifer Sumi ambaye alisoma Shahada ya Uzamili katika Chuo Kikuu cha ICFAI, New Delhi, alisema Waafrika wanaoishi nchini humo huitwa majina ya kashfa kama mbwa weusi na wakati mwingine wahindi huhama eneo ambalo Mwafrika anaishi.
“Unyanyasaji wao upo wazi, wanadharau sababu upo nchini kwao. Wakati mwingine unashindwa kuvumilia na kujikuta unajibu mashambulizi,” alisema.
Aliutaja udhalilishaji mwingine kwa Waafrika ni pamoja na baadhi ya raia wa nchi hiyo kugusa ngozi kisha kuangalia vidole kama vimebakia na rangi nyeusi.
“Wanaweza kukuuliza wewe ni mweusi kwa sababu ya jua? Au ukachekwa tu bila sababu na kwa kuwa huelewi lugha yao,” alisema.
Sumi ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa Wanafunzi wa Kitanzania wanaosoma India, alisema ni vigumu kuishi nchini humo, lakini walivumilia mengi kwa ajili ya kufuata elimu.
Sumi anasimulia zaidi kuwa wanafunzi wanawake wanaonekana ni watu waliokwenda India kufanya biashara ya ukahaba.
“Sijui kwa nini wana mtazamo huo, Wahindi wanaamini kuwa wasichana wa Kiafrika wanaoishi India wanafanya biashara ya ukahaba, ndiyo maana kuna ubakaji mkubwa,” alisema.
Sumi alisema wakati anasoma India wanafunzi wengi walikuwa wanaogopa kupanda daladala za bei nafuu kuepuka ubaguzi, kuchekwa na matusi.
Alitoa mfano wa wakati wa kuadhimisha mila za kurushiana rangi, (Walid), baadhi ya raia wa nchi hiyo waliwarushia pia Waafrika na kuanza kuwacheka.
Mbunge wa Viti Maalum CUF, Riziki Lulida ambaye pia amesoma India, alisema alikumbana na ubaguzi na udhalilishaji akiwa masomoni.
Acharya, Bangalore
Mwanafunzi mwingine anayesoma Chuo Kikuu cha Acharya, Bangalore, Dawson Kimenya anasema ubaguzi huo huwezi kuuona kama utaishi kwenye miji mikubwa au hoteli za kitalii au hospitali bali mitaani.
Alisema Waafrika wanalazimika kupanga vyumba uswahilini kwa sababu ya gharama za malazi na chakula vyuoni kuwa juu.
Anasema ni kawaida kwa Waafrika kuitwa ‘kalu’ (nyani) au absiii (sokwe) mitaani na wakati wakipanda daladala.
“Wakati mwingine mtoto ambaye yupo na wazazi wake anakuita hivyo na huwezi kumfanya kitu,” anasema.
Changamoto nyingine aliyoitaja Kimenya ni kukosa siku maalum ya Watanzania kukutana ubalozi wa Tanzania nchini humo.
“Kufika ubalozini hadi unapopatwa na tatizo tu, hakuna siku maalum ya Watanzania kukutana kueleza changamoto,” alisema.
Kifo cha Yannik huko Punjab
Mtanzania, anayesoma Chuo Kikuu cha TGC, New Delhi, Pius Mmasy alishuhudia Aprili 22, 2012 mwanafunzi raia wa Burundi, Yannik Nihangaza akishambuliwa na vijana wa Kihindi na kusababisha kifo chake.
Tukio hilo lilitokea Kaskazini mwa India, eneo la Punjab. Yannik alikuwa akisoma Shahada ya Sayansi ya Kompyuta katika Chuo Kikuu cha Lovely Professional.
Mmasy alisema vijana hao walikuwa nje ya nyumba ambayo Watanzania walikuwa wakifanya sherehe siku hiyo.
Vijana hao walikuwa wakilazimisha kuingia kwenye sherehe bila ya kualikwa. “Yannik alichukua pikipiki ili arudi bwenini kwake kwa kuwa alisahau kitu, alipotoka nje alivamia na kuanza kupigwa, ” alisema.
Baada ya kupigwa na kujeruhiwa vibaya, Yannik alilazwa katika hospitali ya Patlala kitengo cha wagonjwa mahututi kwa miaka miwili akipumulia mashine na kufariki dunia Julai 1 , 2014.
Hakuna mtuhumiwa aliyekamatwa kuhusiana na mauaji hayo na kwa mujibu wa vyombo vya habari vya nchini humo, wengi wa watuhumiwa walitoroshwa kupelekwa nje ya nchi. “Katika kipindi hicho, Waafrika tuliishi kwa hofu, wasichana walibakwa na kupigwa hovyo, kibaya ni kuwa hatuna pa kuripoti,” alisema Mmasy.
Agra
Mtanzania aliyesoma Chuo Kikuu cha Agra, India, Jane Balama, alisema maisha nchini humo ni magumu kutokana na kukithiri kwa ubaguzi.
Mkenya kuvuliwa nguo
Balama anaeleza mwaka 2013 wakati na Waafrika wenzake wanatoka kufanya manunuzi, walikutana na kundi la Wahindi wakiadhimisha moja ya sikukuu zao za kimila eneo la Agra (ilipo Taj Mahal)
Wahindi hao walianza kumrushia chakula msichana wa Kenya aliyekuwa ameongozana na Balama kisha wakamvua nguo zote.
“Ilibidi wanaume tuliokuwa tumeongozana nao wavue mashati wamsitiri,” alisema.
Balama alieleza alivyoporwa pochi yake yenye fedha na mali zake, lakini polisi aliyekuwa karibu akikataa kumsaidia. “Niliripoti polisi lakini sikusaidiwa,” alisema.
Mwanafunzi anayesoma Chuo Kikuu cha Ambedkar, New Delhi, Richard Msuya alisema ameshuhudia kuitwa majina yanayoashiria ubaguzi kama nyani au nigga. “Kiwango cha unyanyasaji kinatofautiana na mazingira, nipo mji mkuu, New Delhi ni Diplomatic City” alisema.
Balozi mdogo wa ubalozi wa India nchini, Robert Shetkntong anasema hajawahi kupokea malalamiko kuhusu ubaguzi huo.
Hata hivyo, anasema haoni kama kuna ubaguzi wa rangi katika mashambulizi hayo zaidi ya ugomvi wa kawaida wa mitaani.
Kuhusu Waafrika kuitwa nyani na kuvuliwa nguo, alikataa kuzungumzia.
Balozi Kijazi
Balozi wa Tanzania, India, John Kijazi alisema ubalozi upo kwenye mchakato wa kuunda kamati zitakazohusisha wanafunzi, polisi, uongozi wa wenyeji, uongozi wa chuo na Serikali ya jimbo kushughulikia tatizo hilo .
Alisema baada ya kudhalilishwa kwa Mtanzania huyo Januari 31, polisi watano na raia wengine 11 waliofanya tukio hilo wamekamatwa.
Alisema ubalozi ulikwenda kuzungumza na wanafunzi wanaoishi Bangalore na kukubaliana kuunda kamati hizo.
“Nia yetu kurudisha amani wanafunzi wasome kwa amani na utulivu na zisiwepo fujo nyingine,” alisema.

No comments :

Post a Comment