NA MWANDISHI WETU
4th December 2013.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Juliet Kairuki, aliwaambia waandishi wa habari kuwa tayari kuna kampuni toka nchi hizo zilizokwisha nunua hisa kwenye vitalu vya mafuta na gesi asilia.
Alikuwa akizungumza baada ya hafla fupi ya kutiliana saini ya makubaliano kati ya TIC na IE Singapore Cooperation Enterprises toka nchi hiyo jijini Dar es Salaam jana.
“Tayari wengine wameshanunua hisa kwenye uwekezaji wa mafuta na gesi asilia,” alisema.
Makubaliano hayo yanahusisha kubadilishana taarifa za uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore kwa faida ya nchi zote mbili.
Makubaliano hayo kati ya TIC na kituo hicho toka nchini Singapore, yalishuhudiwa pia kampuni nne toka nchi hiyo ambazo zimekuja nchini kuangalia mazingira ya uwekezaji nchini ili waanze kufuata taratibu za kuwekeza katika maeneo mbalimbali.
“Wamekuja kuangalia vivutio ambavyo Tanzania inatoa ikiwamo vya uhamiaji, kodi, vibali vya wageni kufanya kazi nchini na ardhi kwa ajili ya uwekezaji,” alifafanua.
Aliongeza kuwa mahusiano hayo yatasaidia kuendelea kuboresha masuala ya uwekezaji na kufanya biashara pamoja na hiyo itawavutia wawekezaji wengi kutoka nchi hiyo kuja nchini.
“Kituo kipo tayari kusaidia kupitia taratibu zake kuhamasisha na kuvutia uwekezaji zaidi nchini,” alisema. Naibu Mwenyekiti, IE Singapore Cooperation Enterprises, Seah Moon Ming, alisema ujio wao nchini Tanzania unalenga kuimarisha ushirikiano kati ya nchi yao na Tanzania katika nyanja za uwekezaji na biashara.
“Tunataka kubadilishana taarifa za kibiashara na uwekezaji kati ya nchi zetu ili kuleta maendeleo yetu sote,” aliongeza Moon Ming.
Alisema maeneo mengine ambayo wanapenda kuwekeza ni pamoja na sekta ya kilimo, mawasiliano, habari na teknolojia (Tehema) na masuala ya mipango miji.
Kampuni zilizokuja ni pamoja na Pavilion Energy, Temasek Holdings na Singapore Cooperation Enterprise (SCE).
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment