dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Wednesday, September 10, 2014

Sitta katikati ya Maalim Seif, Hamad Rashid

  Hamad Rashid Mohamed

Kwa ufupi
Hata hivyo, Hamad Rashid ambaye alifukuzwa uanachama wa CUF na kupinga hatua hiyo mahakamani hakusema atawania kiti hicho kupitia chama kipi.

Dodoma/Dar/Mwanza. Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta jana alitoa dakika tano kwa Mjumbe wa Bunge hilo, Hamad Rashid Mohamed ‘kujibu mapigo’ dhidi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Maalim Seif Sharif Hamad.
Sitta alitoa fursa hiyo baada ya wenyeviti wa kamati kadhaa kumaliza kuwasilisha ripoti za vikao vyake.
“Tumefikia mwisho wa uwasilishaji wa ripoti za kamati lakini Hamad Rashid ana kitu cha kusema, karibu,” alisema Spika Sitta akimkaribisha na kuongeza kwamba
anatumia Kanuni ya 27(1) (e) ya Bunge hilo ambayo inampa mamlaka kuingiza shughuli yoyote anayoiona inafaa kushughulikiwa kwa wakati huo.
“Nimepata malalamiko kutoka kwa Hamad Rashid Mohamed kwamba hakutendewa haki katika moja ya vipindi vya TV.
Nampa dakika zisizozidi 10,” alisema Sitta kabla ya kuahirisha Bunge hadi leo.
Hata hivyo, kitendo hicho kimekosolewa na mwanazuoni wa sheria na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, James Jesse, akisema: “Hatua hiyo si sahihi lazima ikemewe kwa kuwa hapa nchini hatuna sheria inayotoa haki ya kujibu mapigo bungeni kama ilivyo kwa nchi za wenzetu ambao mtu akishambuliwa bungeni anapata nafasi ya kujibu na majibu yake yanaingia kwenye hansard (kumbukumbu rasmi za Bunge).”
Alisema pamoja na kwamba kanuni inasema inatoa mamlaka hayo kwa mwenyekiti, kitu chochote lazima kiwe na mipaka.
“Kwa kuwa kitu kinachojadiliwa pale ni Katiba na si kitu kingine, hiyo nafasi ya kuzungumzia mambo mengine haikuwapo. Siungi mkono na suala kama hilo lazima likemewe.
Alichosema Hamad Rashid
Mbunge huyo wa Wawi (CUF), alisema katika mahojiano yaliyorushwa na Kituo cha Televisheni cha Star TV juzi kuwa Maalim Seif alimshambulia yeye binafsi, kamati yake na Bunge la Katiba.
“Amesema mimi ni dalali wa CCM na kwamba nimepewa fedha ili kuwahonga watu ili waje kwenye kikao hiki (Bunge). Hili nimemwachia mwanasheria wangu,” Mohamed alimnukuu Maalim Seif na kuongeza:
“Nimemkabidhi (mwanasheria) CD. Nimemwambia naomba uipitie ili twende mahakamani. Nimemwambia wakili wangu kwa hili alilosema akathibitishe mahakamani kama mimi ni dalali.”
Katika mazungumzo hayo Hamad Rashid alitumia dakika tano kuzungumzia masuala ya kamati yake na nyingine tano kumzungumzia Maalim Seif, alisema Makamu huyo wa Rais wa SMZ anamshambulia kwa vile amesikia kuwa anataka kugombea urais... “Sasa natangaza rasmi kuwania urais wa Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.”
Hata hivyo, Hamad Rashid ambaye alifukuzwa uanachama wa CUF na kupinga hatua hiyo mahakamani hakusema atawania kiti hicho kupitia chama kipi.
Alisema si mara ya kwanza kwa Maalim Seif kutoa tuhuma nzito zisizo na ushahidi kama ilivyotokea mwaka 1995 alipodai kuwa Rais wa Zanzibar, Dk Salmin Amour anapanga kumuua (maalim).
Alisema yeye ni mtu mwaminifu na hajawahi kupata kashfa yoyote hapa nchini hata alipokuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Naibu Waziri wa Fedha wa SMZ.
“Mtu mzima unaposema maneno ambayo huwezi kuyapanga vizuri kwa sababu tu Hamad katangaza kugombea urais hilo ni tatizo,” alisema na kuongeza:
“Nilitaka kugombea ukatibu mkuu ukanitimua, sasa huna nafasi ya kunitimua kwenye urais. Nakwenda kugombea urais. Nilikuwa sijasema nakwenda kugombea wapi, nakwenda kugombea Zanzibar,” alisema.
Mjumbe huyo ambaye hakuungana na wapinzani wenzake wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kususia Bunge hilo, alimtaka Maalim Seif asiingiwe na kiwewe kwa yeye kutangaza kugombea urais wa Zanzibar mwaka 2015.
Pia alikanusha madai kwamba yuko bungeni kwa sababu ana uchu wa madaraka na kuwa Maalim Seif ndiye mwenye uchu huo kwa kugombea urais mara nne.
“Mimi sijagombea mara nne urais wala sijawahi kutoka makamu mwenyekiti (wa CUF) nikarudi kuwa katibu mkuu wa chama, halafu nikarudi tena umakamu na nikarudi tena kwenye ukatibu mkuu,” alisema na kuongeza: “Sijawahi kuwa kama Putin (Vladmir - Rais wa Urusi) hata siku moja. Ningeomba sana wananchi wa Tanzania wajue kuwa viongozi ni kama popo. Hajulikani ni mnyama au ni ndege. Putin aliachia madaraka ya urais na kuwa waziri mkuu kabla ya kurejea tena kwenye nafasi hiyo.
“Huku mtu anakwambia nautaka muungano huku anataka Serikali ya Mkataba. Serikali ya mkataba ni lazima uvunje muungano. Huwezi kuwa kiongozi unayejifanya unapenda watu wakati wewe ndiye unayeleta chuki na fitina. Haiwezekani kiongozi anayejua mahitaji ya nchi na vipaumbele vyake apinge mchakato wa kuipata Katiba Mpya kama anavyofanya Seif. Kama lengo lake ni kuvunja Muungano ni vyema akaweka wazi.”
Mjumbe huyo pia alikanusha madai ya Maalim Seif kuwa kuwapo kwake ndani ya Bunge hilo ni kunatokana na kubebwa na Spika wa Bunge (la Muungano), Anne Makinda kwa vile kesi aliyoifungua ilishakwisha.
“Naomba nitoe taarifa rasmi kwako kwamba shauri nililolifungua mahakamani bado linaendelea na kesi ipo tarehe 26/9/2014 na siyo kwa kuhukumiwa, bali kwa kuendelea kusikilizwa,” alisema.
Alisema mara zote Spika amekuwa makini katika jambo hilo akisema hana mamlaka ya kuingilia Mahakama ambayo ndiyo iliyoizuia CUF kumfukuza uanachama ambao pia ungemvua ubunge.
“Kwa hiyo kumpandikizia Spika kwa lawama kama hii haistahiki hata kidogo na ni vizuri akamuomba radhi,” alisema.
Maalim Seif amshukia Sitta
Akizungumza katika mkutano wa hadhara katika Viwanja vya Furahisha, Mwanza jana jioni, Maalim Seif alimlaumu Sitta kuwa anachangia kuvuruga Bunge la Katiba kwa kupindisha kanuni za Bunge hilo.
Bila kugusia mambo yaliyozungumzwa juu yake bungeni, Maalim Seif alisema Katiba Mpya haiwezi kupatikana na kuwa hata kama CCM italazimisha kuipitisha bungeni, hatalala usiku na mchana kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanaikataa.

No comments :

Post a Comment