dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Thursday, September 11, 2014

Tunamuunga mkono JK kwa hatua hii

 http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/1596658/medRes/597847/-/maxh/100/-/nq25wx/-/logo.png

  Rais Kikwete
Hatua ya Rais Jakaya Kikwete kukutana na viongozi wa vyama vya siasa vilivyo wanachama wa Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) na kukubaliana kuhusu mambo matano ya msingi yanayohusu mustakabali wa nchi yetu, ni ya kijasiri na ya kupongezwa.
Moja ya mambo waliyokubaliana ni kuahirishwa kwa Bunge la Katiba ifikapo Oktoba 4, mwaka huu kama Tangazo la Serikali Namba 254 linavyotaka.
Itakumbukwa kwamba Agosti 5, mwaka huu Bunge hilo lilitoa azimio ambalo lilirekebisha Kanuni ya 14(4) na kuzifanya Jumamosi, Jumapili na siku za sikukuu kuwa siku zake za mapumziko.
Hatua hiyo ya Bunge hilo ilipingwa na wananchi kila kona ya nchi, kwani ilimaanisha kwamba lingeendelea na shughuli zake hadi Oktoba 31. Wengi walishangazwa na hatua ya wajumbe wa Bunge hilo kujiongezea muda, huku wakijua kuwapo kwa tangazo hilo la Serikali.Hasira za wananchi zilitokana na Bunge hilo kuonekana halina uhalali wa kisiasa na pia kutumia fedha nyingi za walipakodi kulipana posho pasipo kuzingatia ukweli kuwa, Katiba mpya isingepatikana kutokana na wajumbe hao waliokuwa wameunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kususia shughuli za Bunge hilo.
Tambo za uongozi wa Bunge hilo na wajumbe kutoka chama tawala ambao hasa ndiyo waliosababisha Bunge hilo kupasuka vipandevipande, zilikuwa kwamba Bunge lingeendelea na hatimaye Katiba mpya ipatikane pasipo wajumbe wa Ukawa kushiriki.
Pia walisema wajumbe wa Ukawa wasijidanganye kwamba Rais Kikwete atakutana nao tena kusikiliza malalamiko yao kama alivyofanya huko nyuma wakati mchakato wa Katiba mpya ulipoanza.
Ndiyo maana tunasema hatua ya Rais Kikwete kukutana na viongozi wa TCD na kushirikiana nao kufanya uamuzi mgumu ni wa kijasiri na wa kupongeza.
Tangu wajumbe wa Ukawa wasusie shughuli za Bunge hilo Aprili 16, wamekuwa wakimsihi Rais Kikwete kukutana nao ili kupata suluhu ya malalamiko yao.
Wananchi wengi, wakiwamo viongozi wa kidini wamekuwa wakisisitiza kwamba Katiba itakayopatikana pasipo maridhiano na mwafaka wa kitaifa, haitakubalika.
Kwa maoni yao, Bunge hilo limepoteza muda mrefu pasipo kufanya jambo lolote la maana, kwani kususiwa na wajumbe wa Ukawa kulitokana na kutawaliwa na mijadala ya kupandikiza chuki na mifarakano yenye kuwagawa wajumbe katika makundi yanayokinzana kisiasa na kiitikadi.
Kama tulivyosema hapo juu, mazungumzo kati ya Rais Kikwete na viongozi hao wa TCD yamezaa uamuzi mgumu.
Pamoja na kuamua kuahirisha Bunge hilo ifikapo Oktoba 4, uamuzi mwingine ni: Uchaguzi Mkuu ufanyike mwakani kwa kutumia Katiba ya sasa ya mwaka 1977; kuahirishwa kwa kura ya maoni hadi baada ya Uchaguzi Mkuu, Oktoba 2015; na kuahirishwa kwa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa hadi mapema mwakani.
Uamuzi mwingine ni kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi, mshindi wa Uchaguzi Mkuu awe na zaidi ya asilimia 50 ya kura, kuwapo mgombea binafsi na matokeo ya urais pia kupingwa mahakamani.
Tunampongeza Rais Kikwete kwa hatua hiyo itakayoleta maridhiano na kuepusha nchi yetu na vurugu. Hatua hiyo bila shaka itakuwa imewaudhi wengi ndani ya chama chake, lakini ni kwa masilahi mapana ya Taifa letu.
Matarajio yetu ni kwamba wananchi wote watamuunga mkono, kwani hatua yake hiyo siyo uthibitisho wa udhaifu, bali ujasiri wake.

No comments :

Post a Comment