dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Sunday, October 18, 2015

Nec yataja sababu kuzuia Ukawa kukaa mita 200!


Wakati vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vikidai Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kutaka kukiuka sheria  inayoruhusu wananchi kukaa umbali wa mita 200 kutoka kituo cha kupigia kura wakisubiri matokeo baada ya kupiga kura, hatimaye Nec imelitolea tena ufafanuzi, huku ikiendelea kushikilia msimamo wake.

Ukawa wamekuwa na wasiwasi wa kuibiwa kura, jambo ambalo wamewataka wafuasi wao kukaa umbali wa mita 200 baada ya kupiga kura ili kuzilinda, lakini Nec imekuwa ikilipinga na kuungwa mkono na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, ambaye siku ya Maadhimisho ya Kumbukumbu ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, aliwataka watu wote baada ya kupiga kura kurudi majumbani mwao vinginevyo watashughulikiwa.

Mwenyekiti wa Nec, Jaji mstaafu Damian Lubuva, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, kufuatia baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa kuweka msimamo  wa kuwataka wafuasi wao kubaki vituoni baada ya kupiga kura, alisema sheria ya uchaguzi hairuhusu mtu kukaa ndani ya mita hizo baada ya kupiga kura, kuendesha shughuli yoyote, wala kuvaa sare za chama chochote.

Kadhalika, aliongeza kuwa, sheria hiyo pia hailazimishi mtu kukaa ndani ya mita hizo baada ya kupiga kura.

Alisema idadi ya Watanzania waliojiandikisha kupiga kura mwaka huu ni kubwa zaidi ukilinganisha na vipindi vingine vilivyopita, hivyo wanaamini idadi ya wapigakura itakuwa kubwa pia, ndiyo maana wanawataka watu kutobaki vituoni ili kuepusha viashiria vya uvunjifu wa amani ambavyo vinaweza kujitokeza kutokana na msongamano huo wa watu.

Jaji Lubuva alisema, Nec kama chombo chenye mamlaka ya kusimamia uchaguzi, lengo lake ni kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika katika hali ya usalama, huru na haki.

“Sheria ya uchaguzi hairuhusu mtu kukaa, kuendesha shughuli yoyote ndani ya mita 200 katika kituo cha uchaguzi, kuvaa sare ya chama chochote, pia hailazimishi mtu kukaa baada ya mita hizo,” alisema Jaji Lubuva na kuongeza:

“Kutokana na idadi kubwa ya wapigakura mwaka huu, Nec tunaamini idadi hiyo itajitokeza kupiga kura na ndiyo maana tunawaambia wananchi wasikae vituoni baada ya kupiga kura.

Tunaomba Watanzania watuelewe katika hili na hatutaki kuendeleza malumbano na vyama vya siasa. Hakuna kura itakayoibiwa kwa sababu wawakilishi wa vyama vyote watakuwapo na matokeo yatabandikwa katika kila kituo.”

Jaji Lubuva alisema hata kabla ya kuteua wagombea wa nafasi ya urais kwa vyama hivyo nane, walikubaliana kutekeleza makubaliano hayo, lakini cha kushangaza wameyakiuka.

Pia alisema hata katika mkutano ulioitishwa na baraza la vyama hivyo Oktoba 13 na 14, mwaka huu, walikubaliana kila chama kuwaeleza wafuasi wake kuwa mara baada ya kupiga kura siku ya uchaguzi, warudi majumbani kuendelea na shughuli zao na siyo kukaa vituoni.

Alisema kinyume cha makubaliano hayo, wameendelea kuwasisitiza wafuasi wao kubaki vituoni kwa madai ya kulinda kura na kwamba kauli hizo ni ukiukwaji wa makubaliano ambayo vyama vyote viliafiki.

Aidha, alisema elimu ya mpigakura inayotolewa na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, katika karatasi ya mfano ya kupigia kura kwamba siyo sahihi na inapotosha.

Alisema karatasi ya kupigia kura inatakiwa kukunjwa katikati kwa urefu, ndani  ya picha za wagombea na siyo picha hizo kuonekana  nje, na kwamba endapo wananchi watafanya kama Mbowe anavyoelekeza baada ya kupiga kura, upo uwezekano mkubwa wa kura hizo kuharibika.
Waangalizi 60 EU kuwasili leo.

Waangalizi wa muda mfupi 60 kutoka ujumbe wa Waangalizi wa Uchaguzi wa Umoja wa Ulaya (EU EOM), wanatarajiwa kuwasili jijini Dar es Salaam leo kuangalia Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25.

Taarifa iliyotolewa na Umoja wa Ulaya (EU), kwa vyombo vya habari jana, ilisema, waangalizi hao  watasambazwa nchini kote kuanzia Oktoba 20, na wataungana na Waangalizi wa Muda Mrefu wa EU, ambao wamekuwa wakifuatilia maandalizi ya uchaguzi pamoja na kampeni tangu mwisho wa Septemba.

“Kwa kuwapeleka Waangalizi wetu wa Muda Mfupi, Ujumbe wa Waangalizi wa EU utaongeza upeo wa uangalizi wake na utafuatilia shughuli siku ya uchaguzi,” alisema katika taarifa hiyo, Muangalizi Mkuu wa EU, Judith Sargentini.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments :

Post a Comment