dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Wednesday, December 16, 2015

Sakata la makontena 2,431 laibua mazito


By Fidelis Butahe, Mwananchi
Dar es Salaam. Chama cha Mawakala wa Forodha Tanzania (Taffa), kimedai kuwa ‘mchezo’ wa kutoa makontena 2,431 bandarini bila kulipiwa tozo ya utumiaji wa bandari umefanywa na baadhi ya watendaji wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na baadhi ya wafanyakazi wa benki za CRDB na NMB zenye mikataba na mamlaka hiyo.
Rais wa Taffa, Stephen Ngatunga aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuwa, TPA imekuwa ikiwatuhumu mawakala wa forodha wanaolipa kodi kwa niaba ya wateja wao, kuwa ndiyo wahusika, wakati ikijulikana wazi kuwa mzigo hauwezi kutoka bandarini bila kulipiwa tozo hiyo katika benki na kupewa risiti.
Ngatunga alisema hayo jana baada Desemba 3, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kufanya ziara ya pili ya kushtukiza bandarini na kuibua sakata la kutolewa kwa makontena 2,431 bila kulipwa kodi.
Katika ziara hiyo, Majaliwa alisema kwa mujibu wa taarifa ya ukaguzi wa bandari ya kuanzia Machi hadi Septemba 2014, makontena hayo yalipita bila kulipiwa kodi kupitia bandari kavu nne za JEFAG, DICD, PMM na Azam.
Ngatunga alisema kuwa kuna mchezo unafanywa kati ya TPA na wafanyakazi wa benki hizo wa kufuta taarifa za malipo ya tozo hiyo yanayofanywa na baadhi ya wanachama wa Taffa kwa niaba ya wateja wao.
“Huu ni wizi wa siku nyingi ambao tumeulalamikia sana. Mwanachama wetu akilipia benki na kupewa risiti akienda TPA anatoa mzigo kama kawaida. Baada ya muda taarifa za malipo ya benki hufutwa na aliyelipa anaonekana kakwepa kulipa tozo,” alidai.
Hata hivyo, Kaimu Meneja Uhusiano wa TPA, Janeth Luzangi alikanusha suala hilo na kusisitiza kuwa, haiwezekani kampuni kulipa tozo hizo mara mbili, “Nimeuliza wataalamu wetu wanasema hilo haliwezekani, kama Taffa wana taarifa za benki wazilete tuthibitishe.”
Mkurugenzi wa masoko, utafiti na huduma kwa wateja wa benki ya CRDB, Tulli Mwambapa alisema, “Kama wana ushahidi wauwasilishe katika mamlaka husika ili zichunguzwe na kubaini ukweli. Sisi pia tuna kamera na vifaa vingine tunaweza kufuatilia. Hapa lengo ni kuchunguza na kama si kweli basi wafanyakazi wetu wasafishwe.”
Meneja Uhusiano wa benki ya NMB, Vicent Mnyanyika alipoulizwa kuhusu suala hilo alisema hakuna malipo yoyote yaliyofanyika katika benki hiyo na baadaye ionekane hayakufanyika, kusisitiza kuwa malipo hayo hufanyika katika mfumo ambao hauwezi kughushiwa.

No comments :

Post a Comment