dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Tuesday, December 15, 2015

Shehena ya karafuu yakamatwa Pemba

Karafuu
By Masanja Mabula, Mwananchi
Pemba. Kikosi Maalumu cha Kuzuia Magendo (KMKM), kimekamata shehena ya makonyo na karafuu kavu iliyodaiwa kusafirishwa kwenda nje ya nchi kwa njia ya magendo katika Bandari ya Milango Mikavu kisiwani hapa.
Kamanda wa KMKM Pemba, Silima Haji Haji alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi saa 2:30 usiku.
Alisema watu waliokuwa wakivusha shehena hiyo walikimbia na kutelekeza magunia 31 za makonyo na manne ya karafuu kavu baada ya kuwaona askari wa kikosi hicho wakienda kuwakamata.
Alisema kabla ya tukio hilo, askari waliokuwa doria waliwatilia wasiwasi na walipowafuatilia watuhumiwa hao walikimbia.
Kamanda Silima alisema katika kipindi hiki ambacho karafuu zinaendelea kuchumwa, askari wake wameongeza ulinzi baharini na nchi kavu ili kuwadhibiti watu wanaotaka kuhujumu uchumi wa nchi kwa masilahi yao binafsi.
Mdhamini wa Shirika la Biashara la Taifa (ZSTC) Pemba, Abdalla Ali Ussi amepongeza juhudi zinazochukuliwa na kikosi cha KMKM kupambana na biashara ya magendo ya karafuu.
Aliwataka wananchi kujiepusha na biashara hiyo haramu inayowanufaisha kwa kuwa inadhoofisha uchumi wa nchi.
Alisema wananchi wameitikia wito wa Serikali wa kuuza karafuu katika vituo vya ZSTC na kwamba fedha zinazopatikana hutumika katika kukuza maendeleo.
Baadhi ya wananchi wanaouza karafuu katika Kituo cha Shirika Bandarini Wete, wameviomba vyombo husika kufanya uchunguzi ili watuhumiwa wakamatwe.
Mmoja wa wakazi hao, Yussuf Said Rashid alisema ni vema Serikali kupitia ZSTC kuandaa utaratibu maalumu wa kuwakagua wananchi wenye mikarafuu ili kujiridhisha kama wanaziuza kwenye vituo vya shirika hilo.
Alisema vitendo vya magendo vinatakiwa kukomeshwa kwa kuweka mikakati kabambe ya kuvidhibiti ikiwamo wananchi kutoa taarifa wanapoona matukio kama hayo.

No comments :

Post a Comment