dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Sunday, January 6, 2019

TUNDU LISSU ATOA WARAKA MZITO KUTOKA BELGIUM!

ABOVE: TUNDU LISSU BEFORE HE WAS GUNNED DOWN 
BY THE EVIL FORCES IN DODOMA IN 2017.

MWAKA MPYA 2019: MWAKA WA KURUDISHA DEMOKRASIA, HAKI ZA BINADAMU NA UTU WETU TANZANIA

SEHEMU YA KWANZA

Tundu AM Lissu, MB
University Hospitals Leuven, Campus Gasthuisberg, Leuven, Ubelgiji
Januari 6, 2019

Wapendwa Watanzania wenzangu,

Leo tarehe 6 Januari, 2019, ni mwaka mmoja kamili tangu niletwe nchini Ubelgiji kutoka Nairobi, Kenya, ili kuendelea na matibabu, kufuatia jaribio la mauaji dhidi yangu la tarehe 7 Septemba, 2017. 

Na kwa vile tumeuanza Mwaka Mpya 2019, nawaomba mniruhusu kuwapa salamu zangu za Mwaka Mpya kwa njia hii ya Waraka wa Wazi.

Kama ilivyokuwa mwezi Aprili iliyopita nilipowaaga mawakili wa Tanzania Bara kama Rais wao, ninalazimika kuzungumza nanyi nikiwa nimelazwa hospitalini.
Tuliuanza mwaka jana 2018 nikiwa Hospitali ya Nairobi nchini Kenya. Kwa wakati huo, tayari nilikuwa nimeshafanyiwa operesheni 17 katika sehemu mbali mbali za mwili wangu. 

Tumeuanza Mwaka Mpya 2019 nikiwa hospitalini tena, mara hii katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven, Campus ya Gasthuisberg, mjini Leuven, nchini Ubelgiji. 

Hii ni kwa sababu, siku ya mwisho ya mwaka jana, yaani tarehe 31 Disemba, 2018, nimefanyiwa operesheni ya 22 mwilini mwangu, kutokana na majeraha ya risasi nilizopigwa siku hiyo ya Septemba 7. 

Hata hivyo, tofauti na mwanzoni mwa mwaka jana, nimerudi hospitali mara hii ili kumalizia safari ndefu ya tiba, iliyoanzia Hospitali ya  Mkoa wa Dodoma siku ya kushambuliwa kwangu. 

Katika operesheni hii ya majuzi, timu ya madaktari bingwa ambao wamenitibu tangu nilipofika hapa Ubelgiji mapema mwaka jana, imeondoa kifaa kikubwa cha chuma kilichowekwa ili kuunganisha mfupa wa mguu wangu wa kulia, ambao uliumizwa vibaya katika shambulio la Septemba 7.
Baada ya kuondolewa kwa kifaa hicho, maarufu kwa wengi wetu kama 'antenna', kilichobaki sasa ni marekebisho madogo madogo ya mguu huo, na sehemu nyingine za mwili zilizoumizwa wakati wa shambulio la Septemba 7. 

Tayari nimeshaongezewa kasi ya mazoezi ya kutembea, na muda si mrefu nitaanza mazoezi ya kutembea kwa miguu yangu mwenyewe bila kutumia magongo. 

Ni sahihi, kwa hiyo, kusema kwamba, pamoja na ukweli kwamba matibabu yangu bado yanaendelea, nimeanza Mwaka Mpya nikiwa na Mguu Mpya!!!

'WATU WASIOJULIKANA' NA MAAJABU YAO 

Watanzania wenzangu,

Kama ambavyo imekuwa tangu tarehe 7 Septemba, 2017, wale wote walioamuru, kulipia, kupanga na kutekeleza shambulio la risasi dhidi yangu, katika makazi ya viongozi wa umma Dodoma yenye ulinzi mkali, katikati ya kipindi cha Bunge, bado wanaitwa 'watu wasiojulikana.' 

Katika shambulio hili, hakuna anayeshukiwa na Jeshi letu la Polisi hadi sasa. Hakuna aliyehojiwa na wapelelezi mahiri wa Jeshi letu la Polisi. Hakuna aliyekamatwa na, kwa hiyo, hakuna aliyeshtakiwa. 

Hata wale walioandika maneno ya kuchochea vyombo vya ulinzi na usalama vya Serikali ya Rais Magufuli viniue kwa risasi, na kusambaza maneno hayo kwenye mitandao ya kijamii, hawajaguswa pamoja na kwamba wanafahamika wazi. 

Katika shambulio la kipekee katika historia ya kisiasa ya Tanzania, vyombo vya ulinzi na usalama vya Serikali yetu, na Serikali yenyewe, vimekuwa na ukimya wa ajabu na wa kipekee. 

Huu sio ukimya wa kawaida. Ni ukimya wa wanaojua kila kitu kilichotokea: Nani aliyeamuru na kulipia; nani aliyepanga, na nani aliyetekeleza amri na mpango huo. 

Ndio maana ya kauli ya Spika wa Bunge letu, Job Ndugai, alipohojiwa na Azam TV mapema mwaka jana, kwamba shambulio hili lilikuwa "la kipekee na halitarudiwa tena." Wanajua, ndio maana wanadiriki kusema halitarudiwa tena.

Na ndio maana Serikali ya Rais Magufuli, na Bunge la Spika Ndugai, wameendelea kunisusa kuhusu gharama za matibabu yangu na gharama za kujikimu wakati nikiwa matibabuni. 

Kabla sijahamishiwa nchini Ubelgiji kutoka Kenya, Spika Ndugai aliahidi hadharani, kwenye mahojiano na Azam TV, kwamba atafika kunitembelea, mahali popote nitakapokuwa nimelazwa hospitalini. 

Hadi ninapoandika maneno haya, bado Spika Ndugai hajatimiza ahadi yake hiyo. Na hadi sasa, hakuna mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Bunge, au afisa yeyote wa Bunge, aliyefika hospitalini kuniona na kunijulia hali.

Inawezekanaje, kama hawakutaka nife, Serikali  ya Rais Magufuli na Bunge la Spika Ndugai, ambao walimlipia marehemu Spika Sitta fedha za matibabu yake wakati alishastaafu ubunge na uspika, na akiwa tayari hospitalini nchini Uingereza, imekataa kata kata kulipia matibabu ya Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, aliyejeruhiwa kwa risasi nyingi na 'watu wasiojulikana', wakati akihudhuria vikao rasmi vya Bunge Dodoma???

Inawezekanaje hadi sasa sio Bunge la Spika Ndugai, au Serikali ya Rais Magufuli, ambao wamefanya mawasiliano ya aina yoyote ile, juu ya hali ya afya ya Mbunge  ambaye hajaonekana Bungeni wala nchini kwa mwaka mmoja na miezi  minne, lakini ambaye wameendelea kumlipa mshahara wake wa kila mwezi??? 

Kama hawakuwatuma hao wanaowaita 'watu wasiojulikana' kuja kuniua; kama hawakutaka nife, huu ususiaji wao, huu ukimya wao wa kipekee una maana gani hasa???

Kwa hiyo, kama ilivyokuwa tangu mwanzoni kabisa, na kama ilivyokuwa mwaka jana wote, naanza Mwaka Mpya 2019 nikiendelea kutibiwa na kutunzwa kwa michango na fadhila ya Wasamaria Wema, wa Kitanzania na wasiokuwa Watanzania, waishio sehemu mbali mbali duniani. 

Kwangu mimi, hili ni jambo la heshima kubwa na la kujivunia sana. Ninaamini Wasamaria Wema hawa wamejitolea kunitibu na kunitunza muda wote huu, kwa sababu wanafahamu na kuunga mkono msimamo wangu wa kisiasa wa miaka yote: kujenga nchi na jamii isiyotegemea matakwa na fadhila za mtu mmoja mwenye mamlaka; bali jamii na nchi inayoongozwa na misingi na kanuni za demokrasia, haki, ubinadamu na ukweli. 

Mwenyezi Mungu awabariki na kuwakirimu wale wote ambao wameendelea kuthibitisha ukweli wa msimamo wangu huu, kwa kuendelea kunitibu na kunitunza. 

'WATU WASIOJULIKANA' WAMEENDELEA KUTESA WATANZANIA

Watanzania wenzangu,

Tulimaliza mwaka 2017 na tumemaliza Mwaka jana taifa letu likiwa kwenye hofu kubwa. Hofu ya Serikali yetu na vyombo vyake vya ulinzi na usalama. Hofu ya kutekwa nyara na kupotezwa kabisa, ama kuteswa na baadae kuachiliwa bila uchunguzi wala sababu zozote kutolewa na Serikali yetu.

Tulimaliza mwaka jana bila Ben Saanane, msaidizi wa Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, kujulikana aliko, miaka miwili baada ya kutekwa nyara na 'watu wasiojulikana' mwezi Novemba, 2016. 

Tulimaliza mwaka jana bila Azory Gwanda, mwandishi wa gazeti la Mwananchi, aliyepotea mwanzoni mwa 2017, baada ya kuchukuliwa nyumbani kwake Dar es Salaam na watu waliojitambulisha kuwa ni askari polisi. 

Tulimaliza mwaka jana bila Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma, Simon Kanguye, aliyepotea baada ya kukamatwa nyumbani kwake na watu waliojitambulisha kama maafisa wa Idara ya Usalama wa Taifa na Ujasusi. 

Tulimaliza mwaka jana bila hatua zozote kuchukuliwa na Serikali yetu dhidi ya watu waliomuua marehemu Alfons Mawazo, Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Geita, mwezi Novemba 2015. 

Sasa ni miaka mitatu na bado Rais Magufuli anatutaka Watanzania tuamini kwamba yeye na Serikali yake hawawafahamu, au hawawezi kuwachukulia hatua za kisheria, watu waliomkata mapanga na kumuua Mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani katika Mkoa wake wa Geita, mauaji yaliyofanyika mchana kweupe na kushuhudiwa na watu waliopiga picha za tukio na kuzisambaza mitandaoni.

Tulimaliza mwaka jana bila hatua zozote kuchukuliwa dhidi ya wauaji wa Mh. Luena, diwani katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro; na dhidi ya wauaji wa Daniel John, Katibu wa CHADEMA Kata ya Hananasif, Dar es Salaam. 

Tulimaliza mwaka jana huku Serikali ya Rais Magufuli na Jeshi la Polisi likiwa na ukimya wa kaburi kuhusu waliko watu zaidi ya 380 waliopotea katika wilaya za Kibiti, Kilwa, Mkuranga na Rufiji, baada ya kuchukuliwa na askari polisi kutoka majumbani, mashambani na hata misikitini kwao. 

Hata maiti zilizookotwa zikielea kwenye mito Ruvu na Rufiji, au katika fukwe za Bahari ya Hindi, hazijatolewa maelezo yoyote ya maana na Serikali yetu na vyombo vyake vya usalama, zaidi ya mwaka mmoja baadae. 

Matukio yote haya bado hayana majibu yoyote ya maana kutoka kwa Serikali ya Rais Magufuli na vyombo vyake vya usalama. 

Matokeo yake ni kwamba Tanzania yetu imegeuka kuwa nchi ya vilio visivyoisha; ya machozi ya yatima na wajane yasiyofutika; ya maswali ya wananchi yasiyokuwa na majibu kutoka kwa wale wanaolipwa na umma, ili kutoa majibu ya maswali hayo.

UKANDAMIZAJI KWA KUTUMIA MAHAKAMA

Watanzania wenzangu,

Tarehe 5 Februari, 2016, yapata miezi mitatu baada ya kuapishwa, Rais Magufuli aliahidi, kwenye sherehe za miaka 39 ya kuzaliwa kwa CCM mjini Singida, kwamba atahakikisha vyama vya siasa vya upinzani vimefutika nchini kwetu kabla ya mwaka 2020. 

Baadae mwezi Mei wa mwaka huo wa 2016, ndani ya Ukumbi wa Bunge letu, nilimnukuu Harry S. Truman, Rais wa 33 wa Marekani, katika hotuba yangu Bungeni kama Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria: 

"Pale serikali inapojiwekea kwenye kanuni ya kunyamazisha sauti ya upinzani, inakuwa na njia moja tu ya kufuata, nayo ni njia ya kuongezeka kwa vitendo vya ukandamizaji, mpaka Serikali hiyo inakuwa ndio chanzo cha hofu kwa raia wake wote na inatengeneza nchi ambayo kila mmoja anaishi kwa hofu." 

Kwa kuchukua njia hii, kama alivyosema Rais Truman, sasa Rais Magufuli na Serikali yake wamekuwa ndio chanzo cha hofu kubwa kwa raia wa Tanzania; na wameigeuza nchi yetu kuwa ni nchi ambayo kila mmoja wetu anaishi kwa hofu.

Tulimaliza mwaka jana huku Rais Magufuli akitumia jitihada na nguvu kubwa kutekeleza azma aliyoitangaza hadharani ya kufuta siasa za upinzani katika nchi yetu. 

Jitihada hizo hazikuishia kwenye kupiga marufuku mikutano ya hadhara na shughuli nyingine halali za vyama halali vya siasa vya upinzani. Na wala hazikuishia katika mauaji, utekaji na kupotezwa kwa viongozi na wanaharakati wa kisiasa tuliyoyatolea mifano hapa.

Jitihada za Rais Magufuli zilijumuisha pia matumizi makubwa ya sheria za jinai dhidi ya wabunge, viongozi na wanachama wa vyama hivyo. 

Ni ukweli usioipingika kwamba miaka mitatu ya utawala wa Magufuli, imeshuhudia matumizi makubwa ya vifungu vya uchochezi katika sheria zetu za jinai, kuliko kipindi kingine chochote cha zaidi ya miaka sitini ya vifungu hivyo. 

Kama ilivyokuwa dhamira ya wakoloni wa Kiingereza walioitunga sheria hiyo mwaka 1953, Rais Magufuli ametumia vifungu hivyo kujaribu kuwanyamazisha wapinzani wa Serikali yake na chama chake. 

Mimi mwenyewe ni mfano tosha wa jitihada hizi za Rais Magufuli. Kwani, katika mwaka mmoja uliopelekea kushambuliwa kwangu kwa risasi, nilikamatwa na polisi na kushtakiwa mahakamani mara sita, kwa tuhuma mbali mbali za makosa ya uhuru wa fikra na uhuru wa kujieleza. Sijawahi kupatikana na hatia yoyote katika kesi zote hizo. 

Lakini sio mimi tu ambaye nimekuwa mlengwa mkubwa wa Rais Magufuli na Serikali yake. Orodha ya wabunge wa upinzani ambao wamefungwa, au wana kesi za aina hii katika mahakama zetu mbali mbali ni ndefu. 

Hivi ninavyoandika, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa CHADEMA, Mh. Freeman Mbowe, na Mbunge wa Tarime Mjini, Mh. Esther Matiko, wako gerezani yapata mwezi mzima baada ya kufutiwa dhamana na mahakama. 

Aidha, karibu viongozi wote wa juu wa CHADEMA nao wako mahakamani kwa tuhuma mbali mbali zinazohusiana na kauli walizotoa kwenye mikutano ya kampeni za uchaguzi. 

Vile vile, Kiongozi Mkuu wa chama cha ACT-Wazalendo, Mh. Zitto Kabwe, naye yuko mahakamani kwa kutoa kauli kuhusu tuhuma za mauaji ya wanakijiji katika Wilaya ya Uvinza, mkoani Kigoma, tuhuma zilizotolewa kwa mara ya kwanza na Mbunge wa CCM wa eneo hilo, na baadae kuthibitishwa na Waziri wa Mambo ya Ndani Kangi Lugola. 

HAKUNA ALIYE SALAMA!!!

Watanzania wenzangu, 

Kila kundi la kijamii katika nchi yetu limekumbwa na hofu ya utawala wa Rais Magufuli na 'watu wasiojulikana.' Taasisi za kidini kama makanisa ya Kikristo na madhehebu ya Kiislam yameonja adha ya vitendo vya ukandamizaji vya Serikali ya Magufuli: 

* Baada ya Rais wa zamani wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Askofu Severine Niwemugizi kumkosoa Rais Magufuli kuhusu suala la Katiba Mpya, Serikali ya Rais Magufuli ilihoji uraia wake na kumnyang'anya hati yake ya kusafiria. 

* Katibu Mkuu wa zamani wa TEC, Padre Raymond Saba, naye alinyang'anywa hati yake ya kusafiria  baada ya TEC kuandika Waraka wa Kwaresma mwezi Aprili ya mwaka huu ulioikosoa Serikali ya Rais Magufuli kutokana na sera zake za ukandamizaji wa haki za binadamu. 

* Askofu Zakaria Kakobe wa kanisa la Full Gospel Bible Fellowship Church la Dar es Salaam naye alihojiwa uraia wake, na kupelekewa maafisa wa TRA kumchunguza, baada ya kumtaka Rais Magufuli kutubu kwa Mungu kwa sababu ya kukiuka Katiba na Sheria za nchi kuhusu mfumo wa vyama vingi vya siasa na haki za binadamu.

* Mara baada ya Mabaraza ya Maaskofu wa Kikatoliki na Kiluteri Tanzania kutoa Waraka wa Kwaresma mwezi Aprili ya mwaka huu ulioikosoa Serikali, Serikali ya Rais Magufuli ilitishia, kwa maandishi Rasmi, kufuta usajili wa Kanisa Katoliki Tanzania na Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania kwa 'kujihusisha na mambo ya kisiasa yasiyowahusu.'

* Masheikh, Maimam na viongozi wengine wengi wa madhehebu ya Kiislam wameendelea kuwekwa mahabusu kwenye magereza mbali mbali nchini kwa kutuhumiwa kwa makosa ya ugaidi ambayo hayajawahi kuthibitishwa mahakamani wala upelelezi wake kukamilika. 

Mkakati wa wazi wa Serikali ya  Magufuli dhidi ya viongozi hawa wa Kiislam, ni kuendelea kuwatesa magerezani kwa kutumia sheria ya ugaidi, ambayo inazuia watuhumiwa wasipatiwe dhamana mahakamani.

Serikali ya Rais Magufuli imegeuka kuwa chanzo kikubwa cha hofu kwa wafanya biashara pia:

* Wafanya biashara wengi wamevamiwa na maafisa wa TRA, usalama wa taifa na TAKUKURU na kubambikwa madeni makubwa ya kodi na baadae mali na akaunti zao kwenye mabenki kukamatwa na kutwaliwa na Serikali bila kufuata taratibu za kisheria. 

* Wafanya biashara wengine wengi wamekamatwa na kushtakiwa mahakamani kwa tuhuma za makosa makubwa ya uhujumu uchumi, utakatishaji fedha na ukwepaji kodi. 

Lengo la mashtaka haya, ambayo hayajapelelezwa wala kuthibitishwa mahakamani lakini hayana dhamana, ni la wazi: kuwakamua fedha wale wanaoweza kulipia uhuru wao, na kuwaadhibu wale wasioweza au wasiokuwa tayari kukamuliwa namna hiyo. 

* Wafanya biashara wakubwa, kama vile Mohammed Gullam Dewji na Peter Zakaria wa Tarime, mkoani Mara, wametekwa nyara na kutishiwa maisha kwa kile kinachoonekana wazi kuwa ni kazi ya maafisa usalama wa taifa. 

Kama ilivyokuwa kwa tukio la kushambuliwa kwangu, vitendo hivi vya utekaji nyara havijachunguzwa wala kutolewa majibu ya kuridhisha na vyombo vya usalama vya Serikali ya Rais Magufuli.

Hata wasanii nao hawajapona kwenye hii njia ya ongezeko la ukandamizaji wa Tanzania ya Magufuli:

* Mwanamuziki wa kizazi kipya Roma Mkatoliki na wenzake wawili walitekwa nyara na 'watu wasiojulikana' na kushikiliwa kwa siku kadhaa ndani ya nyumba ya kutesea watu, ambapo waliteswa kwa vipigo kwa muda wote walioshikiliwa na watu hao. 

Roma Mkatoliki ameeleza kwamba kwa muda wote wa kushikiliwa na kuteswa kwao, walikuwa wakihojiwa kuhusu kujihusisha na masuala ya kisiasa au wanasiasa. 

Hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya uchunguzi; hakuna mtuhumiwa aliyetajwa kuhusika na utekaji, na hakuna aliyekamatwa. 

* Mwanamuziki Ney wa Mitego naye alitekwa nyara na 'watu wasiojulikana' lakini baada ya kelele kubwa ya umma, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, aliahidi kwamba ataachiliwa na kweli aliachiliwa baada ya kushikiliwa kwa siku kadhaa. 

Hakuna aliyetuhumiwa, kukamatwa au kushtakiwa kwa kumteka Ney wa Mitego na hakuna taarifa yoyote ya uchunguzi iliyotolewa kwa umma. 

Kuachiliwa kwa Ney wa Mitego ni uthibitisho tosha kwamba watu wanaohusika na vitendo hivi ama wametumwa na Serikali, ama inawajua na kuwalinda. 

* Mwanamuziki Fulgence Mapunda aka Mwanacotide na mwenzake Mussa Sikabwe walikamatwa na kushikiliwa katika Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam kwa siku 42 bila kufikishwa mahakamani, kwa tuhuma za kutunga na kurekodi wimbo uliodaiwa kumkashifu Rais Magufuli. 

Baadae kesi ya uchochezi ilifunguliwa dhidi yao, lakini baada ya kupita zaidi ya mwaka mmoja, kesi hiyo ilifutwa na mahakama kwa sababu ya Serikali kushindwa kupeleka ushahidi wowote mahakamani. 

* Nyimbo za wanamuziki maarufu kama vile Diamond Platinumz, Mr. Sugu na wengineo zimepigwa marufuku, ama wanamuziki wenyewe kufungiwa kufanya kazi zao za sanaa, ndani na hata nje ya Tanzania, kwa tuhuma za 'kukiuka maadili ya Kitanzania', au kuwa na mwelekeo wa kisiasa. 

Kwa mujibu wa sheria yake, Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA) halijapewa mamlaka ya kusajili wasanii, kusimamia maadili yao au kuwaadhibu kwa sababu yoyote ile. 

Hata hivyo, kama ambavyo imekuwa kawaida ya Rais Magufuli mwenyewe na watendaji wake, kutokuwa na mamlaka ya kisheria sio kizuizi cha wao kufanya wanavyotaka.

LESENI YA KUUA RAIA???

Watanzania wenzangu, 

Inawezekana, baada ya miaka mitatu ya kumsikiliza Rais Magufuli akitoa kauli hadharani ambazo haziendani na uzito na hadhi ya Ofisi ya Rais, wengi wetu hatuoni ajabu wala kuchukizwa tena na baadhi ya kauli za Rais wetu hadharani. 

'Maneno huumba', na maneno ya Rais Magufuli, au ya kiongozi yeyote mwenye hadhi na nafasi kama yake, yana maana na uzito wa kipekee. 

Kwa mujibu wa Katiba na Sheria zetu, Rais ndiye Amiri Jeshi Mkuu. Kwa mujibu wa sheria zetu na mila na desturi zetu za kisheria, hata adhabu ya kifo iliyotolewa na mahakama zetu, haiwezi kutekelezwa bila ridhaa ya maandishi ya Rais. 

Kwa sababu hizi, Rais wetu hana haki ya kuzungumza atakavyo anapokuwa hadharani, hasa anapozungumzia masuala ya umma yanayotuhusu sisi wote na yanayoihusu nchi yetu. 

Kila neno na kauli inayotoka kinywani mwake lazima ipimwe kwa kwa uzito unaostahili, kabla haijatoka kinywani mwa Rais wetu. Maneno huumba. Na maneno ya Rais huumba zaidi.

Siku ya tarehe 20 Disemba ya mwaka jana, yaani takriban wiki mbili zilizopita, Rais Magufuli ametoa maelekezo kwa Jeshi la Polisi kwamba, askari polisi wanaoua majambazi na au wahalifu wengine wasikamatwe na kuchukuliwa hatua zozote za kisheria, bali wapandishwe vyeo na kuongezewa mishahara!!!

Rais Magufuli ametamka hadharani kwamba hataki kusikia askari polisi wanaoua raia wakikamatwa kwa sababu Jeshi la Polisi halijaonea mtu yeyote hadi sasa. 

Hii ni kauli ya hatari sana kutolewa na Amiri Jeshi Mkuu kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama. Kwanza, sio ya kweli kwani Jeshi letu la Polisi lina historia ndefu na mbaya ya kunyanyasa, kudhulumu na kuua wananchi wasiokuwa na hatia. 

Pili, askari polisi wetu ni binadamu pia: wana uwezo wa kufanya makosa, hata ya mauaji, kwa makusudi, kwa bahati mbaya au kwa uzembe au kwa kutokujali. 

Kwa sababu inaelekea Rais Magufuli hajui, au amesahau, rekodi mbaya na ya muda mrefu ya Jeshi letu la Polisi, naomba kurejea matukio yafuatayo ya mauaji ya raia yaliyofanywa na Jeshi la Polisi katika vipindi mbali mbali vya miaka ya baada ya uhuru:

* Mwaka 1976, Jeshi la Polisi lilifanya operesheni ya kukabiliana na mauaji ya wachawi na vikongwe katika mikoa ya Mwanza na Shinyanga. Katika operesheni hiyo, watu wengi walikamatwa, kuteswa na hata kuuawa na askari polisi na maafisa wa Idara ya Usalama wa Taifa.

Baada ya mauaji hayo kujulikana, Rais Nyerere aliunda Tume ya Rais ya Uchunguzi iliyothibitisha ukatili mkubwa uliofanywa na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama dhidi ya raia. 

Matokeo ya Uchunguzi huo ni kwamba aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, na baadae mrithi wa Mwalimu kama Rais wa Jamhuri ya Muungano, Ali Hassan Mwinyi; Naibu wake Peter Kisumo; Inspekta Jenerali wa Polisi, Solomon Liani, na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Peter Siyovelwa, walilazimika kuwajibika kwa kujiuzulu nyadhifa zao. 

Aidha, maafisa kadhaa wa ngazi za juu na za kati katika Jeshi la Polisi walifukuzwa kazi. Vile vile, askari polisi wengine wengi walikamatwa na kushtakiwa mahakamani kwa mauaji, na baadhi yao walipatikana na hatia na kuhukumiwa adhabu ya kifo, katika kesi maarufu ya Elias Kigadye na wenzake dhidi ya Jamhuri. 

Katika barua yake ya kuomba kujiuzulu, Mzee Mwinyi alimweleza Baba wa Taifa mambo yafuatayo, ambayo ni muhimu kuyarudia hapa:

"Katika kutekeleza nia nzuri ya Serikali (ya kumaliza mauaji kwa visingizio vya uchawi na kuwafikisha wahusika mahakamani), vyombo vinavyohusika na utekelezaji, Polisi ikiwemo, vilivuka mipaka ya wajibu wao, na vikajipa madaraka ya kuogelea kwenye vitendo viovu vya Kishenzi, Kinyama na Kikatili, hata baadhi ya watu waliokamatwa kwa kushukiwa tu kwamba wanahusika wakafa na wengine wakapata vilema vya kudumu."

Mzee Mwinyi aliendelea kusema: "Polisi ni chombo cha kulinda amani, mali na maisha ya watu wake; si chombo cha kuwaua. Pia Polisi ni chombo cha kuhifadhi na kudumisha usalama na haki; si chombo cha kudhulumu, kuonea na kuwatesa makusudi wananchi wale wale wanaokigharamia kukiweka. Kwa bahati mbaya, maovu kama haya ndiyo hasa yaliyotendwa na vyombo vya Serikali huko Mwanza na Shinyanga."

Kwa zaidi ya miaka arobaini iliyofuatia, Jeshi la Polisi halikujifunza kutokana na kile alichokiita Mzee Mwinyi 'fedheha' ya mauaji ya raia. Matukio yafuatayo yanathibitisha ukweli huu:

* Mwaka 1985, Kikosi cha Kutuliza Ghasia cha Jeshi la Polisi (FFU), kilifanya mauaji ya wafanyakazi kadhaa wa mashamba ya miwa ya Kilombero mkoani Morogoro, waliokuwa wamegoma ili kudai maslahi bora kazini.

Baadae Tume ya Rais ya Uchunguzi wa mauaji hayo, iliyoongozwa na Jaji John Mrosso, ilithibitisha kwamba Jeshi la Polisi lilitumia nguvu kubwa kupita kiasi katika kukabiliana na wafanyakazi hao. 

* Mwaka 1996, Jeshi la Polisi lilifanya mauaji ya zaidi ya wachimbaji wadogo wadogo 50 katika eneo la machimbo ya dhahabu ya Bulyanhulu mkoani Shinyanga, wakati wa operesheni ya kuwaondoa wachimbaji hao kwenye machimbo hayo na kuwakabidhi wawekezaji kutoka Canada. 

Mauaji ya Bulyanhulu yalifanyika licha ya Mahakama Kuu ya Tanzania, masjala ya Tabora, chini ya Jaji Lawrence Mchome, kutoa amri ya kuizuia Serikali isiwaondoe wachimbaji hao mpaka kesi ya msingi dhidi yao itakapoamuliwa na Mahakama Kuu hiyo. 

* Mwaka 2001 Jeshi la Polisi lilifanya mauaji ya wananchi zaidi ya 20 wa Kisiwa cha Pemba, waliokuwa wanapinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Rais wa Zanzibar wa mwaka 2000. 

Mwaka 2006, Mkuu wa Upelelezi wa Jinai Mkoa wa Dar es Salaam, Abdallah Zombe na askari polisi kadhaa waliwateka nyara, kuwaibia fedha zao na baadae kuwaua kwa kuwapiga risasi wafanya biashara wanne wa madini kutoka Wilaya ya Mahenge mkoani Morogoro. 

Baadae baadhi ya wauaji hao walihukumiwa kifo na Mahakama Kuu ya Tanzania, kabla ya uamuzi huo kutenguliwa na Mahakama ya Rufani ya Tanzania. 

* Mwaka 2011 Jeshi la Polisi lilifanya mauaji ya wananchi 4 mjini Arusha, kwenye maandamano ya kumbu kumbu ya miaka 10 ya mauaji ya Zanzibar. 

* Mwaka huo huo wa 2011, Jeshi la Polisi mkoani Morogoro lilimuua muuza magazeti Ali Zona, wakati wa jaribio la kuzuia mkutano halali wa hadhara ulioitishwa na CHADEMA mjini Morogoro. 

* Siku chache baada ya mauaji ya Ali Zona, Jeshi la Polisi mkoani Iringa lilimuua mwandishi habari na mpiga picha wa Channel Ten, marehemu Daudi Mwangosi, kwa kumlipua na bomu la kishindo, wakati wa kuwatawanya viongozi na wafuasi wa CHADEMA waliokuwa wanafanya kikao cha ndani katika eneo la Nyololo wilayani Mufindi. 

Licha ya Serikali na Jeshi la Polisi kujaribu kufunika ukweli kwa kuwatuhumu wanachama na wafuasi wa CHADEMA kuhusika na mauaji ya marehemu Mwangosi, Uchunguzi uliofanywa na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ulithibitisha kuhusika kwa Jeshi la Polisi na mauaji hayo. 

* Kati ya mwaka 2012 na 2013, katika kile kikichoitwa Operesheni  Kimbunga na Operesheni Tokomeza Ujangili, Jeshi la Polisi lilifanya mauaji ya wananchi wengi katika mikoa ya mipaka ya magharibi ya Tanzania, na maeneo yanayopakana na Hifadhi za Taifa na maeneo tengefu ya wanyamapori na Hifadhi za Misitu. 

Mauaji haya yalithibitishwa na Kamati Teule ya Bunge na yalipelekea kujiuzulu kwa mawaziri kadhaa wa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete. 

* Mwaka 2014, Jeshi la Polisi lilituhumiwa kuhusika na vitendo vya utesaji na mauaji ya wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara waliokuwa wanaandamana kupinga uamuzi wa Serikali kujenga Bomba la Gesi Asilia kutoka mikoa hiyo kwenda Dar es Salaam.

* Kati ya mwaka 2016 na 2017, Jeshi la Polisi limetuhumiwa kwa mauaji au kutoweka kwa zaidi ya watu 380 kutoka Wilaya za Kibiti, Kilwa, Mkuranga na Rufiji katika operesheni ya kukabiliana na mauaji ya viongozi wa vijiji na askari polisi katika maeneo hayo. 

* Mwaka jana, Jeshi la Polisi limemuua mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Aquilina Aquiline, wakati wa kuwatawanya viongozi na wafuasi wa CHADEMA waliokuwa wanafanya mkutano halali wa kampeni za Uchaguzi wa marudio Kinondoni mkoani Dar es Salaam.

* Na miezi miwili iliyopita, Jeshi la Polisi mkoani Kigoma limetuhumiwa kufanya mauaji ya raia wengi katika Kata ya Nguruka wilayani Uvinza. 

Hili ndio Jeshi la Polisi ambalo Rais Magufuli amelisifu kwamba halijawahi kuonea mtu yeyote, na ambalo ameelekeza askari wake wasikamatwe pale wanapoua raia wetu.

Watanzania wenzangu,

Jeshi la Polisi halina ruhusa, kwa mujibu wa sheria za nchi yetu, ya kuua mtu yeyote yule. Na Rais wa nchi yetu hana ruhusa, kwa mujibu wa Katiba na sheria zetu, ya kuamuru mtu yeyote kuua ama kuuawa, kwa sababu yoyote ile, isipokuwa kwa kutekeleza adhabu ya kifo iliyotolewa na mahakama zetu kwa mujibu wa sheria. 

Kwa hiyo, 'Leseni ya Kuua' raia, ambayo Rais Magufuli ameitoa kwa Jeshi la Polisi, ni haramu na haina budi kupingwa na kila mmoja wetu, ikiwa ni pamoja na askari polisi wenyewe. 

Kwa mujibu wa Sheria ya Rome iliyounda Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC), vitendo vya wanajeshi kuua raia ni mojawapo ya makosa ya kivita na makosa dhidi ya ubinadamu yanayoadhibiwa na Mahakama hiyo. 

Kwenye makosa haya, hoja ya kutii amri za wakubwa au kutekeleza 'maagizo kutoka juu' sio utetezi dhidi ya mashtaka hayo.

ITAENDELEA WIKI IJAYO...



No comments :

Post a Comment