Maalim Seif amekutana na viongozi wa Jumuiya ya Makampuni ya waongozaji na watembezaji watalii Zanzibar (ZATO), na kusema kuwa serikali inazingatia sana suala la usalama kwa watalii.
Amesema sekta ya utalii ambayo kwa sasa ni sekta kiongozi katika upatikanaji wa fedha za kigeni Zanzibar ni muhimu, na kwamba inahitaji uangalizi na usalama wa hali ya juu, ili kuwaweka watalii katika mazingira salama. Aidha amesisitiza haja ya kutolewa elimu kwa wananchi, ili waweze kushiriki katika kuundeleza na kufikia dhamira ya kuwa na utalii kwa wote.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Khalifa Mohd Makame, ameelezea juu ya kuwepo kwa wimbi kubwa la watembezaji watalii wasio rasmi au kwa jina jengine “mapapasi” ambao kwa kiasi kikubwa wamekuwa wakileta athari katika sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kupotea kwa mapato ya serikali.
Ameshauri kuwepo utaratibu utakaowawezesha waongozaji na watembezaji watalii kufanya kazi zao kwa kuzingatia sheria zilizopo, ili kuhakikisha kuwa watalii wanakuwa salama na mapato ya serikali hayapotei.
Vile vile viongozi hao wameishauri serikali kuunda kamati maalum itakayokuwa ikitoa taarifa za kiuhalifu zinapotokea, ili kuepusha vyombo vya habari vya ndani na nje kutoa taarifa zisizo za uhakika.
Wamesema mara nyingi yanapotokea matukio ya kihalifu, serikali imekuwa ikichelewa kutoa taarifa, na kupelekea waandishi wa habari kutoa taarifa kwa mujibu wa maoni yao, jambo ambalo limekuwa likiichafua Zanzibar kimataifa na kuathiri sekta ya utalii.
Wamesema pia kuna haja kwa serikali kufikiria namna ya kuweka vifaa vya kiusalama “CCTV camera” katika maeneo ya Utalii likiwemo Mji Mkongwe, ili kudhibiti vitendo vya kihalifu vinavyoweza kutokea katika maeneo hayo.
Chanzo: ZanzibariYetu
No comments :
Post a Comment