Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema wawekezaji vitega uchumi kutoka China wana nafasi kubwa ya kufungua miradi yao hapa Zanzibar, ikiwemo katika sekta ya utalii wa kimazingira kisiwani Pemba.
Makamu wa Kwanza wa Rais amesema hayo alipokuwa na mazungumzo na Balozi mdogo wa China aliyepo Zanzibar, Xie Yun Liang ambaye alifika ofisini kwake Migomban, mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha, baada ya kupangiwa kazi hapa Zanzibar hivi karibuni.
Makamu wa Kwanza wa Rais amesema wawekezaji kutoka China wanakaribishwa kufungua miradi ya hoteli za daraja la juu Zanzibar, ambapo kwa upande wa Pemba kuna maeneo mazuri yanayoweza kutumiwa kwa utalii, bila ya kuathiri hali ya mazingira.Mbali na utalii, Maalim Seif alimueleza Balozi huyo kuwa eneo la uvuvi wa bahari kuu pia linaweza kutumiwa na wawekezaji kutoka nchi hiyo, kwa vile bahari ya Zanzibar ina maliasili nyingi, wakiwemo samaki na kwamba hadi sasa hakuna wawekezaji wengi walioingia katika eneo hilo.
Nae Balozi huyo mdogo wa China amesema nchi yake na Zanzibar zimekuwa na mashirikiano ya muda mrefu na atahakikisha mashirikiano hayo yanaendelezwa kwa faida ya pande mbili hizo.
Amesema upanuzi wa uwanja wa ndege Zanzibar unaofanyika kwa kujengwa eneo jengine la kuingia na kutokea abiria, utarahisisha wawekezaji na watalii wengi kutoka China kuja Zanzibar, kwa vile utatoa fursa kwa ndege za nchi hiyo kuja moja kwa moja hapa Zanzibar.
No comments :
Post a Comment