
Makamu wa Rais, Samia Hassan Suluhu akifagia katika barabara ya Karume Osyterbay Dar es Salaam wakati wa Maadhimisho ya MIaka 54 ya Uhuru wa Tanganyika jana. Picha na Salim Shao
Dar es Salaam. Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan ameziagiza manispaa za Dar es Salaam kuwachukulia hatua za kisheria makandarasi waliopewa zabuni za kufanya usafi wa mazingira katika maeneo ya jiji hilo na kushindwa kutekeleza wajibu wao.
Agizo hilo alilitoa jana wakati akifanya usafi na wakazi wa Manispaa ya Kinondoni katika mitaa ya Oysterbay na Morocco, kutekeleza agizo la Rais John Magufuli la kuadhimisha miaka 54 ya Uhuru wa Tanganyika kwa kufanya usafi.
“Nataka kuona haya yakifanyika, manispaa, wachukulieni hatua wazabuni wanaoshindwa kazi…narudia tena wachukulieni hatua wazabuni wanaoshindwa kazi.
“Maana wanawanyonya wananchi, pesa mnazowalipa ni kodi ya wananchi, tunategemea kuona kazi zao, ” alisema Suluhu.
Aliagiza mkandarasi yeyote anayepata zabuni, akashindwa kufanya kulingana na mkataba, anyang’anywe zabuni mara moja na akabidhiwe mtu anayeweza kufanya.
“Muda wa kuchekeana sasa umeisha, tunataka kuona, jiji la Dar es Salaam likimeremeta,” alisema.
Pia, alihimiza wananchi kuiunga mkono Serikali pale itakapotoa maelekezo ya kufanya jambo lolote kwa masilahi ya Taifa na kushirikiana na wakurugenzi kuendelea na usafi wakati wote.
“Tunataka kuona miaka 54 ya Uhuru, Tanzania haina shida ya umeme, maji, dawa hospitalini na uchafu bali iwe Tanzania ya maendeleo. Hivyo tufanye kazi kweli kweli,” alisema.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda, alisema wanaanza kuyafanyia kazi maagizo yote kwa kupitia mikataba ya wazabuni.
“ Tumeanza kampeni ya kufanya usafi kila mwisho wa mwezi ijulikanayo kama ‘Naona aibu kuishi na uchafu’ kampeni hii pia itaenda sambamba na kuwawajibisha makandarasi wasiotekeleza kazi zao kwa mujibu wa sheria,” alisema Makonda .
Mkurugenzi Manispaa ya Kinondoni, Mussa Natty aliwataka wananchi wasisubiri Rais atoe tamko ndipo wafanye usafi.
No comments :
Post a Comment