NA LEONCE ZIMBANDU
3rd September 2013
Rasimu hiyo imebainisha mambo saba ya msingi kuwapo kwenye uundwaji wa katiba mpya ili kushughulikia muungano mojawapo kati ya hayo ni suala la ulinzi na Usalama.
Pendekezo hilo lilitolewa na Ibrahimu Chambuso, mmoja wa wajumbe wa baraza la asasi za kiraia wilayani Bagamoyo (Bangonet), mkoani Pwani.
Alisema ikiwa Jeshi la kujenga Taifa (JKT) limekuwa la muungno na kuwa chini ya Wizara ya Ulinzi na JKT, hivyo inapaswa vikosi vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kuwa chini ya wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi au Ulinzi.
“Unajua rasimu imeandaliwa vizuri kwa serikali tatu, lakini mtazamo wangu nahitaji serikali mbili, bali mapungufu yaliyopo yarekebishwe tutapata katiba nzuri,”alisema.
Mwezeshaji wa kongamano la Bangonet, Emanuel Patuka, alisema yeye jukumu lake ni kuchukua mapendekezo yaliyotolewa na wajumbe wakati wa kuipitia rasimu na kuyawakilisha.
Alisema Baraza hilo limejadili mambo mengi ya msingi ikiwa ni pamoja na kupiga kura na kuchagua serikali mbili ziendelee kwa kuwa zitapunguza gharama kuliko kuongeza mzingo usiobebeka.
“Wakati wa kupiga kura kulikuwa na mvutano, wapo waliohitaji serikali tatu na wengine Serikali mbili ambao ndiyo walioibuka kuwa washindi,” alisema.
Katibu Mtendaji wa Bangonet, Leonard Bankuwia, alisema kongamano hilo limehudhuriwa na washiriki 100, kutoka kwenye asasi 50 zilizopo katika Wilaya ya Bagamoyo.
Alisema kwao ni fursa nzuri kukumbukwa kwani kipindi cha miaka ya nyuma, masuala kama hayo yalikuwa yakijadiliwa na wasomi, wanasheria na wataalamu wengine mbalimbali.
“Hii kwetu ni fursa nzuri, hivyo tunahitaji ushuru wa forodha kuwa jambo la muungano na katiba ijayo iruhusu uraia wa nchi mbili ili kukuza uchumi wa Taifa,” alisema Bankuwia.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment