dual citizenship

Pemba Paradise

Zanzibar Diaspora

Mwanakwerekwe shops ad

ZanzibarNiKwetuStoreBanner

ZNK Patreon

Scrolling news

************ KARIBUNI..................Contact us for any breaking news or for any information at: znzkwetu@gmail.com. You can also fax us at: 1.801.289.7713......................KARIBUNI

Saturday, February 13, 2016

UCHAMBUZI: Siku 100 za Dk Magufuli, ndoto ujenzi wa reli na viwanda


By Fidelis Butahe, Mwananchi
Niliwahi kusoma kitabu kimoja kilichoeleza yaliyojiri katika Mkutano Mkuu wa Tanu mwaka 1972. Katika kikao hicho moja ya mambo kuhusu maendeleo ya ujenzi wa reli ya Tazara, wakati huo ikiwa imefika mbali.
Halmashauri kuu iliagiza kuwa katika maeneo yote ilikopita reli hiyo kuanzishwe vijiji vya ujamaa na ikahimizwa kuwa vijiji hivyo visaidie kuanzisha shughuli za uchumi ambazo zingesababisha kuboresha mapato ya reli kwa kusafiririshia mizigo ya kibiashara.
Hii ina maana kuwa Tanu ilitambua kuwa bila kuwa na shughuli za uchumi zilizokuwa kubwa na endelevu, reli ile isingeweze kujiendesha.
Nakumbuka kitabu hicho wakati huu nikitafakari siku 100 za Rais John Magufuli tangu alipoapishwa Novemba 5, 2015 kuwa kiongozi mkuu wa nchi, mambo yaliyoibua mjadala mzito katika Mkutano wa Bunge uliomalizika hivi karibuni kuhusu ujenzi wa reli ya kisasa (standard gauge).
Wabunge walidiriki hadi kuunda Umoja wa Wabunge wa Reli (UWR), wakiongozwa na Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige huku wakisema wataendelea kushinikiza bila ya kuchoka ujenzi wa reli hiyo.
Ni ukweli ulio wazi kuwa reli iliyopo sasa ni ya zamani mno na imekuwa haimudu tena mikikimikiki, mvua ikinyesha nyingi tu mataruma hung’oka na kusababisha ajali.Kadhalika hivi sasa reli tuliyonayo hatuitumii kama ilivyodhamiriwa kuwa iwe njia kuu ya kusafirisha mizigo, hivi sasa mizigo mingi husafirishwa kwa njia ya barabara, jambo hilo limesababisha huduma hiyo isiwe mchangiaji mkubwa wa pato la taifa.
Ahadi ya ujenzi wa reli ya kati ni kubwa ambayo inaweza isilete muujiza wowote kiuchumi kama hatutaweza kutatua tatizo la msingi, ambalo ni kuanguka kwa uchumi wa nchi, hasa katika viwanda na biashara.
Hapa katikati tuliamua kuuza uendeshaji wa reli ya kati kwa wawekezaji wageni kutoka India na kuamua kuibadilisha reli ya kati na kuiita TRL.
Migogoro mingi ikaibuka, na kuwa zaidi ya kuendesha safari za abiria kwa ufanisi usio mkubwa sana, shughuli za kiuchumi za reli hazijaboreka na ukifika kwenye baadhi ya njia, zimeota nyasi na hatujui lini hali itaboreshwa.
Binafsi naona kama kweli tunataka kuifufua reli ya kati, kuna hatua za msingi ambazo tungepaswa kuzifuata na tena kwa uangalifu.
Kwanza ni kuhakikisha kuwa shughuli za viwanda katika vituo mbalimbali ambako reli inapitia, zianzishwe na ziimarishwe.
Hapo tuanze na kilimo ambacho kimekufa. Wakati ule shehena za kahawa kutoka mikoa ya kusini, pia tumbaku, katani na pamba zilisaidia sana kuongeza pato la reli.
Maeneo ya Morogoro, Dodoma, Shinyanga na Mwanza kulikuwa na viwanda ambavyo vilisaidia sana kuchangia pato, kwani shehena nyingi ilikuwa ikisafirishwa kwa reli.
Pato lingine lilitokana na kuwa na uchumi bora katika nchi tulizopakana nazo. Mabadiliko ya hali ya uchumi kuelekea kwenye kudorora, na kutokana na vita vya wenyewe huko DRC, Rwanda na Burundi, usafirishaji wa mizigo kutoka nchi hizo umepungua sana na kama sio kusita kabisa, na hasa kwa kutumia reli.
Uchumi wa DRC umepungua sana kutokana na vita, na nchi kama Rwanda sasa ina uhuru wa kusafirisha mizigo kutokeo na kupitia Mombasa.
Kwa sasa hkumeongezeka ushindani wa aina mbili. Kwanza wa reli kushindana na usafiri wa barabara. Uboreshaji wa safari za barabara umeipatia changamoto reli ambayo inaonekana ni gharama na pengine ni taratibu mno. Hii litasaidiwaje na kupanuka kwa reli? Wakati tunazungumzia kupanua reli yetu, Kenya na Rwanda zinasaini mkataba wa kujenga reli yao wenyewe. Haya ni mashindano.
Serikali ilipaswa kufikiria uboreshaji wa reli katika muktadha wa changamoto zinazoikabili nchi na uchumi kwa ujumla, kuona namna gani shughuli za kilimo, na hasa kilimo cha mashamba makubwa na cha mazao ya biashara, na viwanda zinavyoweza kuboreshwa.
Wachumi wangeanza na kukaa na kufikiri na kupanga kwa makini, nini hasa sababu ya kurudi nyuma kiuchumi na hivyo kufa kwa reli zetu, na hata Rais Magufuli anapokutana na viongozi wa mataifa makubwa ajenda yake iwe ni hiyo.
Hivi karibuni Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango alisema bungeni kuwa Serikali haiwezi kujenga reli hiyo kwa kutumia bajeti yake na kwamba iwapo itatumia fedha za Mfuko wa Reli ambazo ni Sh50 bilioni kila mwaka, maana yake ni kwamba kazi ya ujenzi huo itachukua miaka 320 kukamilika.
Gharama za kujenga reli hiyo ni kati ya dola bilioni saba mpaka tisa na nusu (Sh15 trilioni) ambazo kwa uchumi wa Tanzania ambao pato lake la Taifa la ndani kwa mwaka ni dola za Marekani 53 bilioni, zaidi ya Sh100 trilioni ni vigumu kuhimili gharama za ujenzi huo.
Endapo Serikali itatilia mkazo ujenzi wa reli, gharama za usafiri na usafirishaji kwa mamilioni ya wananchi na hata nchi jirani zitashuka na hivyo kutoa nafuu kwa maisha ya wananchi.
Wabia chini ya mpango wa ushirikishaji wa sekta binafsi na ya umma (PPP), ufanyike kwa umakini watapatikana na haitachukua muda kazi hiyo itaanza na kukamilika mapema, hilo lifanyike kwa kuzingatia uendelezaji na uanzishwaji wa viwanda na mashamba makubwa ya kilimo.

No comments :

Post a Comment